Habari za Punde

Michuano ya Kombe la Dunia 2022 Kutimua Vumbi leo Nchini Qatar

Michuano ya kuwania ushindi wa Kombe la Dunia 2022 itaanza Novemba 20, wakati ambapo  timu 32 zitakuwa zinapigania kuingia kwenye fainali itakayofanyika Desemba 18.

Kwa sasa hivi, bila shaka timu zilizofuzu zinaendelea kujinoa katika masuala mbali mbali nyakati za mwisho mwisho huku waliojumuishwa kwenye timu husika wakijiweka sawa kujihakikishia ushindi.

Fahamu ni timu gani inayoweza kuwa mshindi wa Kombe la Dunia 2022 na kwa nani?

Kundi A: Qatar, Ecuador, Senegal na Uholanzi

Hili ni kundi ambalo litafungua michuano ya kuwania Kombe la Dunia.

Timu ya taifa ya nchi hii imeingia kwenye mashindano ya Kombe la Dunia mara tatu na mwaka huu 2022, itakuwa mara yake ya nne.

Hatua hii inaweza kuchukuliwa kama timu yenye uzoefu na wanaweza kujivunia bendera yao.

Kocha wa timu hiyo Gustavo Alfaro aliamua kuwaweka pembeni wachezaji wa zamani kama kina Antonio Valencia, na Felipe Caicedo na kufungua ukurusa mpya kwa vijana kama kina Moises Caicedo na Piero Hincapie.

Nikizungumza na Daniel Mlimuka mchanganuzi wa masuala ya michezo kuhusu timu zinazoshindana katika Kombe la Dunia alisema:

“Equador ni timu ambayo inaweza kuingia uwanjani ikiwa na  wachezaji nyota au ambão sio nyota.”

Hata hivyo, Equador, haikuwa na uhakika wa kushiriki Kombe la Dunia baada ya kushtakiwa katika Mahakama ya Usuluhishi wa Michezo (CAS) na nchi ya Chile iliyodai kwamba mchezaji wa Equador, Byron Castillo, hakustahili kucheza wakati wa mechi za kufuzu kwa madai eti sio raia wa nchi hiyo.

Hata hivyo, mahakama ilitupilia mbali madai hayo, lakini ikasema Shirikisho la Soka la Ecuador (FEF) lilikiuka Kifungu cha 21 cha Kanuni za Nidhamu za FIFA kwa matumizi ya hati yenye taarifa za uongo.

‘’Ingawa hati ya kusafiria ya mchezaji wa Ecuador ilikuwa ya kweli, baadhi ya taarifa zilizotolewa humo zilikuwa za uongo,’’ mahakama hiyo iliongeza.

Na kutokana na hilo, Ecuador, imepunguziwa pointi tatu katika kampeni ya kufuzu kwa Kombe la Dunia la 2026.

Qatar ndio mwenyeji wa michuano ya Kombe la Dunia na kwa michuano kuchezwa kwao, hii imekuwa fursa ya wao kuonyesha maendeleo ya soka ya Qatar.

Pia kuna Senegal timu ya Afrika ambãyo ni mabigwa wa Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON), na inayoonekana kutoa matumaini makubwa kwa mashabiki zake ya kufanya vizuri katika kundi hili.   

Daniel Mlimuka mchanganuzi wa masuala ya michezo anasema “Uholanzi ndio vinara wa kundi hilo. Wana kocha mwenye uzoefu na kupata matokeo bora, pia wana nyota wa soka na hilo linawaongezea fursa ya kuibuka kidedea katika kundi hili.”

Kundi B: England, Iran, Marekani na Wales

Tuanze na England ambayo imeonekana kunufaika kwa kiasi kikubwa na uwekezaji wa nguvu kubwa kwa soka ya vijana.

Wachezaji chipukizi kama vile Philip Walter Foden na Trent Alexander-Arnold wote hao ni uzao wa timu za vijana ambapo England iliamua kuweka nguvu zake kuanzia mwaka 2012.

Ndio maana imekuwa ikifanya vizuri kuanzia kwa Kombe la Dunia la mwaka 2016, mashindano ya EURO 2020, kunakotokana na matunda ya uchezaji wao kwa vijana. 

Sio tu kwamba England wanaweza kuwa vinara katika kundi hili kwasababu ya vipaji vyao, lakini wanaweza kusonga mbele na kufiki hata nusu fainali ama pia fainali,” anasema Daniel Mlimuka.

Aidha, England wamekuwa na historia nzuri, mwaka 1966 ndiyo ilishinda Kombe la Dunia.

Na katika kundi hilo, timu inayoweza kuipa ushindani ni Iran na Wales. Iran siku za nyuma imekuwa na mchezo mzuri katika ukanda wa nchi za Kiarabu na Wales nayo imejumuisha nyota wake kama vile Gareth Bale na Aaron Ramsey.

Kocha wa Marekani kwa upande wake akuwatema wachezaji vigogo wa zamani kama mlinzi  Tim Ream, Ricardo Pepi, na Jordan Morris na kujumuisha akina Haji Wright na Josh Sargent.

Ukweli ni kwamba Marekani imeshuhudia wakati mgumu kuingia kwenye Kombe la Dunia na bila shaka yoyote mabadiliko katika kikosi chake ambayo yameshangaza wengi, ni kwa matumaini ya kufanya vizuri.AGES

Kundi C: Argentina, Saudi Arabia, Mexico na Poland

Argentina ndiyo ambayo inaonekana kuwa na uwezo mkubwa wa kuibuka kidedea katika kundi hili lakini kwa bahati mbaya ubora unaotarajiwa kutoka kwao haujajitokeza kiuhalisia.    

Bwana Mlimuka anasema, “kuna maswali ambayo wanaibua, mfano, je wao ni bora bila nyota Lionel Messi. Iwapo wataingia uwanjani bila Messi, je wachezaji wanaomzungumza wataweza kutumia fursa hiyo kuonyesha uwezo wao. Ama kutokuwa na Messi uwanjani kutawaathiri kwa namna moja au nyengine.”

Ukiangalia Poland, katika michuano ya hivi karibuni, wameonyesha wanaweza kujikakamua hasa kwenye kundi ambalo wapo.

Wachezaji wake wamekuwa na mchezo mzuri kama vile nyota Robert Lewandowski ambaye amejiunga na Barcelona msimu uliopita baada ya miaka minane ya kuitumikia Bayern Munich.

Mexico, hata hivyo, mchezo wake umeonekana kudorora wakati Kombe la Dunia linakaribia.

Lakini Mchambuzi wetu Bwana Mlimuka anaonekana kuwa na mawazo tofauti.

“Ni kundi ambalo lipo kimtego. Huwezi kusema moja kwa moja timu fulani inaweza kuwa mshindi. Utakumbuka kuwa katika Kombe la Dunia Urusi, hakuna aliyetegemea kuwa Argentina wangeibuka washindi.”

Kundi D: Ufaransa, Australia, Denmark na Tunisia

Kwa kundi hili mshindi anaweza kuwa Ufaransa. Hii ni kwasababu ina wachezaji wa kimataifa katika kila eneo na wenye machaguo mengi.

Hata hivyo, Mlimuka anasema wanaweza kukumbana na changamoto.  

“Kukosekana kwa Paul Pogba na N'Golo Kanté wachezaji ambão walikuwa muhimu kwa Ufaransa kushinda Kombe la Dunia lililopita, kunaweza kuwa pigo kwao.”

Kante alikuwa akiziba mapungufu mengi ya Ufaransa yaliyojitokeza mara kwa mara.

Lakini pia inaweza kukabiliana nayo kwenye aina ya kundi walipo kwa sasa ila hali hii ikaendelea kuwa kibarua kigumu kadri hatua inavyosonga mbele, watakapokutana na Brazil, England na Ujerumani.

Upande mwingine Denmark inaweza kuwapa ushindani mkali kwani wana wachezaji wengi wa soka ya miguu ambao wapo kwenye Ligi tofauti tofauti za Ulaya ukilinganisha na Tunisia na Australia ambão hawana wachezaji wenye uzoefu.

Kundi E: Uhispania, Costa Rica, Ujerumani na Japani

Kundi hili lina ushindani mkali na hapa kuna wawili ambao wana uwezo wa kuchukua Kombe la Dunia. Uhispania na Ujerumani ambao wote wamerejea kufufua soka yao.  

“Kuna wakati Uhispania ilivuma kweli kweli kabla ya kuanza kudhalilika kwenye michuano ya dunia lakini siku za hivi karibuni kocha wao Luis Enrique Martínez García ameonekana kufanya kila analoweza kurudisha hadhi ya soka ya taifa hilo,” mchanganuzi Daniel Mlimuka anasema.

Kocha wao ana uwezo wa kuunganisha vipaji kwenye timu ya taifa na kupata matokeo mazuri.

Ujerumani nayo pia imeweza kujititimua kurejesha hadhi yao.

Japani nayo imejaribu kuwekeza pakubwa na kushindana na timu kubwa za soka kwenye Kombe la Dunia.

Hata hivyo, Japani ya sasa sio ile ya 2010 ya wachezaji kama kina Keisuke Honda miaka minane iliyopita.

Kundi F: Morocco, Canada, Belgium na Croatia

Hili nalo sio kundi rahisi kwamba unaweza kusema kwa haraka haraka nani anaweza kuibuka kidedea.

Croatia wachezaji wao wengi bado wapo kwenye ubora ambão unaweza kusaidia timu.

Kocha Zlatko Dalic amechagua wachezaji kadhaa wa Premier League, akiwemo mshambuliaji wa Tottenham Ivan Perisic na kiungo wa Chelsea Mateo Kovacic.

Croatia itawania kufanya vyema katika michuano hiyo baada ya kushika nafasi ya pili kwenye Kombe la Dunia la 2018 nchini Urusi.

Mlimuka anasema “Morocco ambão nilikuwa nikiwapa nafasi ya kufanya vizuri kwa timu za Afrika, pengine huenda hapa wamebanwa zaidi ukilinganisha na Senegal. Lakini bado wapo vizuri kwenda kwenye hatua ijayo.”

Canada wanaingia kwa mara ya kwanza tangu mwaka 1986. Hii inaweza kuwapa afueni Morocco pengine kwasababu ya wachezaji wengi ambao hawana uzoefu wa Kombe la Dunia au michuano mikubwa lakini pia ina uwezo mkubwa wa kuonyesha wengine kivumbi kwa kuwa wachezaji wake wengi ni wa asili ya nchi tofauti tofauti.

Cha msingi kinachojitokeza kwa timu ya Canada ni kwamba wamekuwa wajanja na kukusanya vipaji katika siku za hivi karibuni na inaweza kushangaza wengi kwa kupiga hatua pengine hata kufika nusu fainali.  

Kundi G: Brazil, Serbia, Swizerland na Cameroon

Brazil ndio wanatazamiwa kuwa kinara wa kundi hili.

Baada ya miaka mingi sasa timu ya taifa ya Brazil inaweza kuwekwa kwa mizani sawa na zingine zenye uwezo mkubwa wa kushinda Kombe la Dunia.

Wachezaji wengi wapo kwenye ubora wao, mfano Gabriel Jesus yupo Arsenal, Neymar mshambuliaji wa PSG, Antony mshambuliaji wa Manchester United.

Wana wachezaji wengi sana wenye vipaji na hilo linafanya inakuwa rahisi kwao kusakata mchezo wa kiwango cha juu.

Kundi H: Ghana, Portugal, Urugay na Korea Kusini

Portugal watakuwa wanashiriki kwa mara ya nane katika Kombe la Dunia.

Cristiano Ronaldo amejumuishwa kwenye kikosi na kuongeza matumaini zaidi kwa kikosi hicho kusonga mbele hasa ukizingatia kuwa sio kundi rahisi.

“Kocha wao Fernando Santos amekuwa mwalimu mzuri mwenye uwezo lakini upande wa mbinu ya kukusanya pamoja vipaji ili waweze kung’ara zaidi kwenye soka kidogo inamlemea,” anasema Daniel Mlimuka.

Ghana inayowakilisha Afrika nayo inaingia na kikosi cha wachezaji wengi wapya.

Washambulizi wakongwe Luis Suarez na Edinson Cavani wamejumuishwa katika kikosi cha wachezaji 26 cha Uruguay kwa ajili ya michuano hiyo nchini Qatar.

Korea Kusini imekuwa ikiingia kwenye Kombe la Dunia lakini haijakuwa na matokeo ya kuridhisha kwenda mbali.

Chanzo cha Habari BBC.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.