RAIS wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Al hajj Dk. Hussein Ali Mwinyi amewataka
wananchi wa Mkwajuni kuitumia na kuitunza vyema misikiti yao kwa kuendelea
kutoa sadaka mara kwa mara ili kuwapa nguvu wasimamizi wa misikiti hiyo.
Al hajj Dk. Mwinyi aliyasema hayo wakati wa ufunguzi
wa msikiti wa masjid Istiqama, uliopo Mkwajuni njia ya Matemwe, Mkoa wa Kaskazini
Unguja.
Alisema licha
ya uzuri wa misikiti na uimara wake lakini itafikia hatua misikiti itahitaji ukarabati,
huduma za maji na umeme ambavyo vyote vinahitaji usimamizi mzuri na gharama za
kuhudimiwa, hivyo aliwaasa wananchi na waumini wa Kiislamu kutoa sadaka ambazo
zitasaidia gharama za uendeshaji pamoja na kuwalipa wasimamizi wa misikiti hiyo
Aidha, aliwaasa
waumini hao kuitumia misikiti hiyo kwa sala na ibada nyengine pamoja na
kumshukuru mfadhili wa msikiti huo.
Akihutubu
kwenye sala ya Ijumaa msikitini hapo, Katibu Mtendaji kutoka Ofisi ya Mufti
Zanzibar, Khalid Ali Mfaume alizungumzia fadhila za sadaka kwa muumini mwenye
kuitoa na kueleza kuwa sadaka humuweka mtu huru kwa Mola wake.
Aidha,
aliongeza sadaka kuleta tahfifu na shifai kwa muumini mgonjwa na kueleza kwamba
swadaka huwa sababu ya mja kusamehewa makosa yake kwa Mwenyezi Mungu. Hivyo aliwanasihi
waumini hao kushajihika na kuendelea kutoa sana sadaka misikitini mwao.
Mapema, akisoma
risala ya ufunguzi wa msikiti huo, Ustadhi Maulid Nafasi Juma alisema ujenzi wa
msikiti huo ulitokana na uhitaji wa waumini wa eneo hilo ambao kwa mda mrefu
walitumia msikiti mdogo uliokua haukidhi haja ya mahitaji ya eneo hilo.
Ustadhi
Nafasi alieleza awali walikua na msikiti uliojengwa tokea mwaka 1983 lakini
kutokana na changamoto kadhaa walizokumbana nazo ikiwemo kuongezeka kwa waumini
kutokana na kutanuka kwa vijiji kwenye eneo lao, ndio iliwalazimu kutafuta
mfadhali kwaajili ya ujenzo mpya hadi kufunguliwa kwake mwaka huu.
IDARA YAMAWASILIANO,
IKULU
No comments:
Post a Comment