Habari za Punde

Misamaha ya VAT kwa Sekta ya Viwanda ni kwa Mujibu wa Sheria

Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Hamad Hassan Chande akijibu swali bungeni jijini Dodoma.
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Hamad Hassan Chande akizungumza na Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Oliver Semuguruka, bungeni jijini Dodoma.

Na. Farida Ramadhani, WFM                                                                                                                     

Serikali imeeleza kuwa utaratibu wa Msamaha wa Kodi ya Ongezeko la Thamani(VAT) hususani kwenye Sekta ya Viwanda umewekwa kwa mujibu wa Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani.

Hayo yameelezwa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Hamad Hassan Chande alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Jimbo la Konde Mhe. Mohammed Said Issa aliyetaka kujua vigezo vinavyotumiwa na Serikali kusamehe kodi ya VAT kwa Sekta ya viwanda nchini ili kuleta usawa kwa wote.

Mhe. Chande alisema kuwa katika SURA 148 ya Sheria hiyo imeeleza kwa kina vigezo vinavyotumika kutoa msamaha wa VAT katika Sekta ya viwanda kuwa ni pamoja na uagizaji na usambazaji wa bidhaa au huduma kwa Serikali zitakazotumika kwenye miradi inayotekelezwa kwa fedha za Serikali, mikopo na misaada kutoka kwa Washirika wa Maendeleo.

Alisema vigezo vingine ni usambazaji wa bidhaa au huduma kwa ajili ya unafuu wa majanga ya asili na uagizaji wa malighafi zinazotumika kutengenezea vyandarua.

Mhe. Chande alibainisha  kuwa uagizaji na usambazaji wa bidhaa au huduma kwa kampuni yenye makubaliano na Serikali katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati pia ni kigezo cha utoaji wa VAT.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.