SERIKALI
ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema ni jambo muhimu kwa Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) kusimamia na
kudhibiti matumizi salama ya vyanzo vya mionzi nchini, ili vitoe mchango zaidi
katika maendeleo ya Taifa.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti
wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi aliyasema hayo alipoweka jiwe la
msingi la ofisi na maabara ya Tume hiyo kwa Zanzibar, huko Dunga Zuze Wilaya
ya Kati, Mkoa wa Kusini Unguja.
Dk. Mwinyi alisema Taifa
linatumia teknolojia ya nyuklia katika nyanja mbalimbali na kueleza kuwa sayansi
na teknolojia ya nyuklia ina manufaa makubwa ikitumiwa vizuri, itasaidia
kuongeza kasi ya ukuaji wa sekta mbalimbali za uchumi ikiwemo kilimo, mifugo,
nishati na afya.
Alisema
Zanzibar imepata mafaniko makubwa kutokana na kutumika kwa teknolojia ikiwemo
kutokomeza wadudu aina ya mbung’o ambao walikuwa wakiathiri afya na uzalishaji
wa mifugo hususan ng’ombe.
Alieleza
Tume iliwezesha upatikanaji wa mbegu bora ya mpunga aina ya “SUPA BC”, yenye sifa
ya kustahamili ukame na maradhi na kuongeza sasa mkulima anaweza kupata tani
saba badala ya nne za awali kwa hekta moja.
Akizungumzia
faida ya atomu kwa sekta ya elimu, Rais Dk. Mwinyi alieleza Serikali ya
Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania imesaidia kuimarisha uwezo na utaamu wa
kudhibiti na kuongeza wigo wa matumizi ya teknolojia ya nyuklia nchini.
“Wizara ya
Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania,
inakamilisha utaratibu wa kufadhili vijana wa Kitanzania kwenda kusoma masuala
ya Sayansi na Teknolojia ya Nyuklia katika vyuo bora duniani” alieleza Dk.
Mwinyi.
Aidha, Rais
Dk. Mwinyi aliwataka wadau na wafanyakazi wa Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania
kujituma kwa bidii na maarifa ili kuleta mchango mkubwa kwa Taifa.
Akizungumza
kwenye hafla hiyo, Naibu Waziri Elimu, Sayansi na Teknolojia wa Jamuhuri ya
Muungano wa Tanzania, Omar Juma Kipanga kwa niaba ya Waziri wa Wizara hiyo, Prof.
Adolf Mkenda alieleza mipango ya wizara hiyo kuongeza uwekezaji kwenye eneo
hilo.
Alisema Serikali
ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Elimu imedhamiria
kuongeza wataalamu zaidi kwenye eneo hilo na kuongeza kwamba tayari
imekamilisha mitaala ya shahada tatu za uzamili kwenye Teknolojia ya nyuklia
zitakazo tolewa kupitia taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Afrika Nelson
Mandela, Arusha
Akizungumzia
ufadhili wa masomo kupitia mpango wa (Samia Scholarship) Naibu Waziri huyo,
alieleza Serikali inawahamisisha vijana kubobea kwenye masomo ya sayansi ili
kunufaika na fursa nyengine za ufadhili za ndani na nje ya nchi. Pia alieleza
juhudi nyengine zinazochukuliwa na Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania
ni kuweka msukumo wa kutanua wigo wa matuizi ya sayansi na teknolojia ya
nyuklia nchini.
Naye, Waziri
wa Afya Ahmed Nassor Mazrui amesema, sekta ya afya Zanzibar inafanyakazi kwa
karibu na Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania, kutokana na miradi yake mingi kuhusisha
mionzi.
Tume ya
Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) ilianzishwa chini ya sheria ya bunge la Jamuhuri
ya Muungano wa Tanzania nambari 7 ya mwaka 2003 kwa lengo la kusiumamia na
kudhibiti matumizi salama ya mionzi pamoja na kusimamia vyanzo vyote dhidi ya
madhara yanayoweza kusababishwa na vyanzo hivyo. Pia ina jukumu la kuhamasisha
na kuendeleza matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia nchini.
Ujenzi wa
ofisi ya Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania kwa Zanzibar, utahusisha ofisi 27,
maabara sita, kumbi tatu za mikutano, ukumbi mkubwa wenye uwezo wa kuchukua
watu 100, jiko na sehemu ya kulia, ukumbi wa bodi, ukumbi mwengine wa mikutano
wenye uwezo wa kuchukua watu 21 pamoja na eneo la walinzi.
IDARA YA MAWASILINO, IKULU ZANZIBAR
No comments:
Post a Comment