Habari za Punde

Ndg.Mussa : Anena Mazito Miaka 59 ya Muungano wa Tanzania

NAIBU Katibu Mkuu wa UVCCM Zanzibar Mussa Haji Mussa, akizungumza hoja mbalimbali kuhusu miaka 59 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

(Picha na Hamad Khamis Sharif).

NA IS-HAKA OMAR,ZANZIBAR.

NAIBU Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Zanzibar Mussa Haji Mussa,amewasihi vijana nchini kuenzi na kuthamini Muungano wa Serikali mbili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Zanzibar.

Rai hiyo ameitoa wakati akizungumza katika mahojiano maalum    huko Afisi kuu ya Umoja huo uliopo Gymkhana Zanzibar, alisema vijana wana dhamana kubwa ya kulinda muungano huo uliorithiwa kutoka kwa waasisi wa ASP na TANU.

Alisema miaka 59 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ni kipindi kirefu ambacho nchi hizo mbili zimepitia mabadiliko makubwa ya kimaendeleo katika nyanja za kisiasa,kiuchumi na kijamii.

Alieleza kuwa Zanzibar imeendelea kunufaika kupitia fursa mbalimbali zikiwemo sekta za ajira,elimu,afya,siasa,uwekezaji na miundombinu mbalimbali katika sekta ya usafirishaji na uchukuzi.

“ Wito wangu kwa vijana wote nchini bila kujali tofauti zetu za kisiasa,kidini na kikabila, kwa umri wetu tunatakiwa kuweka mbele uzalendo wa nchi kwa kuhakikisha tunathamini na kulinda Muungano huu wa Serikali mbili tuliorithishwa na wazee wetu.

Tunanufaika na mambo mengi kupitia Muungano huu mfano fedha za mikopo ya elimu ya juu,fedha za mfuko wa IMF za UVIKO-19 zimetumika kujenga hospitali za kisasa nchini kila Wilaya yapo mengi yanaendelea kufanyika”, alisema Naibu Katibu Mkuu huyo wa UVCCM Zanzibar Mussa.

Pamoja na hayo alieleza kuwa Umoja huo utaendelea kufanya makongamano na kutoa elimu kwa vijana mbalimbali nchini kuanzia ngazi za maandalizi hadi vyuo vikuu kwa dhamira ya kuwajengea uwezo wa kujua historia halisi ya Muungano.

Mussa, alifafanua kuwa maendeleo yaliyofikiwa chini ya Serikali ya awamu ya sita ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan pamoja na Serikali ya awamu ya nane ya Zanzibar inayoongozwa na Rais wa Zanzibar Dk.Hussein Mwinyi, zimepiga hatua kubwa ya maendeleo kiuchumi,kisiasa,kiutamaduni,michezo na diplomasia kwa kipindi kifupi toka wameingia madarakani.

Katika maelezo yake Naibu Katibu Mkuu huyo, aliongeza kwamba njia pekee ya kulinda tunu hiyo ya Muungano ni kudumisha amani,mshikamano na utulivu sambamba na kufanya kazi kwa bidii ili nchini iendelee kuimarika kiuchumi.

Sambamba na hayo aliwasihi vijana nchini hasa wa UVCCM kuchangamkia fursa zinazopatikana katika sekta ya Muungamo kwa pande zote mbili za nchini kwa tutafsiri kwa vitendo falsafa za Royal Tour na Uchumi wa buluu kuhakikisha wanajiajiri wenyewe kupitia sekta za utalii,uvuvi,kilimo,uvuvi na uwekezaji.

Pamoja na hayo aliwapongeza Rais wa Zanzibar Dk.Hussein Mwinyi pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan, kwa kasi ya utendaji wao katika kutekeleza Ilani ya uchaguzi ya CCM ya mwaka 2020/2025.

Aidha, Naibu Katibu Mkuu huyo, alifafanua kwamba katika historia ya Tanzania Marais hao wawili ambao ni Dk.Hussrin na Dkt.Samia katika utawala wao wa miaka miwili toka waingie madarakani wamevunja rekodi katika kutatua kero za muda mrefu za Muungano ambazo zilikuwa ni 25 hadi hivi sasa tayari zimetafutiwa ufumbuzi wa kudumu kero 22.

CAPTIONS

Picha no.01-NAIBU Katibu Mkuu wa UVCCM Zanzibar Mussa Haji Mussa, akizungumza hoja mbalimbali kuhusu miaka 59 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar(Picha na Hamad Khamis Sharif).

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.