Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhajj Dk.Hussein Ali Mwinyi Kuchangia Shilingi Milioni 10 kwa Ajili ya Umaliziaji wa Maduka Kwa Ajili ya Msikiti wa Paje Unguja

 
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Al hajj Dk. Hussein Ali Mwinyi, amechangia shilingi milioni 10 kwaajili ya ujenzi wa maduka matano, yanayokusudiwa kutoa gharama za uendeshaji wa msikiti mkuu wa Paje, Mkoa wa Kusini, Unguja.

Al hajj Dk. Mwinyi alitoa mchango huo alipofungua msikiti huo na kuiasa jamii na waumini msikitini hapo, kujitoa kwa hali na mali kuchangia ujenzi wa maduka hayo ili kukamilisha ujenzi.

Alisema ujenzi wa maduka hayo utachangia gharama za uendeshaji wa misikiti huko endapo utahitaji matengenezo na ukarabati, gharama za maji na umeme pamoja na gharama za kuwalipa masheikh na maimamu watakaouendesha msikiti huo.

Aidha, Al hajj Dk. Mwinyi aliwanasihi waumini na viongozi wa msikiti huo kuutumia vyema kwa mambo ya khairati na yenye kujenga jamii iliyobora, ikiwemo kusaliwa, kuwafundishia vijana maadili mema na kuwakataza mabaya, ili kuwanusuru na majanga ya kilimwengu ikiwemo athari za dawa za kilevya na masula ya udhalilishaji wa kijinsia.

Pia, aliwaeleza waumini hao lengo la kujengwa misikiti hiyo kwa waumini ni kusaliwa kwa wakati na kufanyiwa ibada kwa wingi, hivyo aliwaomba kujaza safu wakati wote wa kutekelezwa kwa ibada msikitini hapo.

Al hajj Rais Dk. Mwinyi, pia alitumia fursa hiyo kuwashukuru wafadhili wa ujenzi wa msikiti huo pamoja na kuwashukuru wazawa kwa weledi wa kujitoa kwao kuanza ujenzi wa msikiti huo kabla ya kupata wafadhili.

“Tunawashukuru sana wafadhili wetu kwa kujitoa na kuijenga misikiti mizuri na yenye hadhi kubwa kama huu, lakini ningependa zaidi niwashukuru, niwapongeze na niwatakie kila la kheir wale ndugu zetu walioanza ujenzi wa msikiti huu kabla ya kupata wafadhili, hawakukaa wakafunga mikono wakasema tunamsubiri mfadhili, walianza wao. Hii ni imani kubwa walioionesha kidogo walichokua nacho walianza nacho hadi walimaliza msingi wa jengo lote.” Alipongeza Al hajj Dk. Mwinyi.

Naye, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Haroun Ali Suleiman alisema, wananchi na waumini wa Mkoa wa Kusini Unguja wanaungamkono jitihada zinazofanywa na Rais Al hajj Dk. Mwinyi.

Akizungumza kwenye halfa ya ufunguzi wa msikiti huo, Mfadhili Dk. Maheer Bakari alieleza misikiti ni nyumba za Mwenyezi Mungu, hivyo aliwaomba waumini wazitukuze, wazitunze na kuziheshimu kwaajlili ya kimtaja Mwenyezi Mungu muda nyakati zote.

Pia alimshukuru Rais Al Hajj Dk. Mwinyi kwa harakati zake kwenye masuala ya dini.

Pia sheha wa Paje, Mohamed Rajab nae alieleza ujenzi wa msikiti huo ulianza mwaka 2021 kwa wananchi wa shehia hiyo kujitolea kuchimba msingi na kuutengeneza wote na mwaka jana walitokea wafadhali na kuujenga msikiti huo hadi kukamilika kwake.

Alitumia fursa hiyo kuwashukuru wafadhili hao kwa kuukamilisha ujenzi wa msikiti huo.

 IDARA YA MAWASILIANO, IKULU ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.