Walimu wa Skuli za Maandalizi wakifuatilia mafunzo ya kuwajengea uwezo juu ya mbinu bora za kufundishia lugha ya kiengereza kwa wanafunzi yaliyofanyika Chuo cha Universal Polytecnic College Mchina mwanzo Zanzibar.PICHA NA FAUZIA MUSSA
Na Fauzia Mussa
MKUU WA Wilaya ya Mjini Rashid Simai Msaraka amevitaka Vyuo vidogo vidogo kuhakikisha wanatoa elimu bora kwa Vijana yenye sifa na vigezo vya kuweza kujiajiri na kuajirika.
Ameyasema hayo huko Chuo cha Universal Polytechnic College wakati alipotembelea mafunzo ya walimu wa Msingi na Maandalizi yaliolenga kuwajengea uwezo wa mbinu bora za kufundishia lugha ya kiengereza kwa wanafunzi wachanga
Amesema kuwa ndani ya Jamii zetu kuna wimbi kubwa la Vijana waliokosa vigezo vya kuendelea na kidato cha tano, cha sita hadi kujiunga na vyuo Vikuu hivyo uwepo wa vyuo hivyo ni Mkombozi wa Vijana hao na kuutaka uongozi wa Chuo hicho kuhamasisha vijana kujiunga na vyuo kama hivyo ili kujiongeza kielimu.
Alieleza kuwa uwepo wa Vyuo vidogo vidogo ni muhimu sana kwani kunaunga mkono juhudi za Serikali za kuendeleza Sekta ya Elimu Nchini.
Alifahamisha kuwa Nchi nyingi zilizoendelea zilifanikiwa kwa kushirikiana na Sekta Binafsi katika nyanja mbalimbali ikiwemo za elimu na zimekua na mchango mkubwa wa kuisaidia Serikali katika kutoa ajira hivyoSerikali itaendelea kuweka Mashirikiano na Sekta Binafsi ili kuleta Mabadiliko katika nyanja mbalimbali ikiwemo za Elimu.
Aliongezea kuwa mwanafunzi bora huanza kuandaliwa katika hatua za awali hivyo aliwashauri walimu hao kuhakikisha wanawajenga wanafunzi mwanzoni ili kuwa bora katika maisha ya Baadae na kuleta tija kwao na Taifa kwa Ujumla.
Mkuu huyo aliwataka walimu waliyopatiwa mafunzo hayo kuyafanyia kazi mara watakapoanza majukumu yao na kutumia lugha nzuri za fundishia hasa kwa wanafunzi wa maandalizi kwa faida ya Vizazi vyetu na Taifa kwa ujumla .
Nae Afisa Uratibu Mahusiano ya Vyuo kutoka Wizara ya Elimu kitengo cha Uratibu wa Elimu ya Juu Shehe Othman Haji amesema lengo la kuanzishwa kwa vyuo vidogo vidogo ni kuisaidia Wizara ya Elimu kupambana na juhudi zakupunguza idadi ya Vijana wasiosoma katika jamii,
Hata hivyo alivishauri Vyuo hivyo kuhakikisha wanachukua wanafunzi wenye sifa na vigezo vya kujiunga na chuo kulingana na Matakwa ya Wizara ya elimu ili kuondoa usumbufu kwa Baraza la Mitihani kuweza kuwatambua.
Kwa upande wake Kaimu Mkuu wa Chuo cha Universal Polytecnic Collage Rahma Soud amesema lengo la mafunzo hayo kwa Walimu wa Msingi na Maandalizi ni kisaidia serikali kutatua changamoto ya kuimarisha elimu katika ngazi za Chini.
Jumla ya Walimu 40 kutoka Skuli mbali mbali za Binafsi na Serikali wamepatiwa mafunzo ya kuwajengea uwezo juu ya mbinu bora za kufundishia lugha ya kiengereza(Jolly Phonics and English Proficiency) kwa Wanafunzi wa Skuli za Maandalizi.
No comments:
Post a Comment