Habari za Punde

Wazazi na Walezi Watakiwa Kusimamia Vijana Wao Kuwalea Katika Malezi Bora - Alhajj Hemed

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Alhajj Hemed Suleiman Abdulla amewataka Wazazi na walezi kuwasimamia vijana wao na kuwalea kwa kufata misingi ya kitabu kitukufu cha Qur – an ili kupata viongozi waliobora wa baadae.

Alhajj Hemed ameyasema hayo alipokuwa akiwasalimia Waumini wa Masjid IMANI uliopo MIGOMBANI CHINI mara baada ya kumaliza  Ibada ya Sala ya Ijumaa.

Amesema kuwa wazazi na walezi wana jukumu kubwa la kuwasimamia vijana wao pamoja na kuwapatia elimu zote mbili ya dunia na akhera kwa manufaa yao wenyewe na Taifa kwa ujumla jambo ambalo litapelekea kupata viongozi bora wa Serikali pamoja na wanazuoni wenye kuisimamia dini ya kiislamu. 

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amesema ni lazima kwa kila mzazi na mlezi kuhakikisha anawasimamia vijana wake ili kuwakinga na matendo maovu na machafu yatakayosababisha uvunjifu wa amani sambamba na kuwakinga na matendo ya uzalilishaji na madawa ya kulevya. 

Alhajj Hemed amesema kuwa  dunia imekumbwa na mambo mabaya na maovu  mengi ambayo  husababisha kuwepo kwa mmong’onyoko wa maadili hivyo ni wajibu wa kila mzazi na mlezi kumpatia kijana wake elimu ili kumuwekea msingi nzuri wa kimaisha hapo baadae. 

Sambamba na hayo Alhajj Hemed amewashukuru Watanzania wote pamoja na Wazanzibari kwa kuendelea kudumisha amani, upendo na mshikamano baina yao jambo ambalo linaipelekea Serikali kufikia malengo yake iliyojiwekea ya kuwaletea maendeleleo endelevu wananchi wake. 

Amesema ni lazima wananchi kuunga mkono jitihada zinazochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Nane (8) inayoongozwa na Rais Dkt. Hussein Ali Mwinyi  katika kuwaletea maendeleo wananchi wake pamoja na kuwatatulia chongamoto mbali mbali zilizokuwa ziwakabili bila ya ubaguzi wa aina yoyote. 

Mapema akitoa Khutba katika Sala ya Ijumaa, Maalim ABDI  ZUBEIR   amewataka waumini wa dini ya Kiislam na Wazanzibari kwa ujumla kuhakikisha wanawapatia watoto haki zao za msingi jambo ambalo litapelekea kupata watoto walio wema pamoja na viongozi wazuri wa baadae. 

Amesema kuwa  kila mzazi na mlezi ni dhamana kwa anaemuongoza na ndio masuuli mkubwa kesho mbele ya haki hivyo ni lazima kuhakikisha anamsimamia vyema mtoto wake pamoja na anaowaongoza ili kupata radhi za Allah (S.W). 

Imetolewa na Kitengo cha Habari (OMPR)

Leo tarehe..29.12.2023

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.