Habari za Punde

Mkurugenzi TAMWA ZNZ awashukuru wadau kufanikisha zoezi la utoaji tuzo kwa waandishi wa habari 2024.

KURUGENZI Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania, TAMWA ZNZ kwa niaba ya ZAFELA na PEGAO ametoa shukrani za dhati kwa wote waliochangia kufanikisha hafla ya utoaji tuzo kwa waandishi wa habari iliyofanyika Jumamosi, Machi 9, 2024, katika Ukumbi wa SHAA mjini Unguja.

Akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari huko ofisi za TAMWA ZNZ Tunguu, Mkurugenzi wa TAMWA ZNZ, Dkt. Mzuri Issa ametoa pongezi kwa waandishi wote waliowasilisha kazi zao kwa ajili ya kushiriki tunzo za umahiri wa waandishi wa habari za wanawake na uongozi.

Tuzo hizo zilitolewa katika vipengele vinne tofauti ikiwemo Radio Jamii, Radio za kitaifa, magazeti pamoja na mitandao ya kijamii ambapo habari zilizowasilishwa zilikua zikiangazia maeneo mbalimbali ya kupigania haki za wanawake na mabadiliko.

Washindi wa tuzo hizo walizawadiwa zawadi ya vyeti, ngao pamoja na fedha taslim ambapo mshindi wa jumla ni Amina Masoud aliyezawadiwa hundi yenye thamani ya shilingi milioni moja na laki tatu za Kitanzania, ikionesha kutambuliwa kwa mchango wake wa kipekee katika tasnia hiyo.

Akizungumza wakati wa mkutano huo Jaji Mkuu wa Tuzo hizo Dkt. Abdalla Mohammed Juma alisema waandishi wa habari wanawake wameonesha muamko mkubwa katika kuwasilisha kazi zao ambapo katika waandishi wote walioleta kazi wanawake walikua ni 379.

Dkt. Abdalla aliongeza kuwa kazi hiyo ya kuwatafuta washindi wameifanya kwa uadilifu mkubwa kuhakikisha washindi waliopatikana ni wale waliowasilisha kazi zenye ubora.

“Kazi tuliyopewa tumeifanya kwa uadilifu mkubwa, na kama kuna mapungufu ni sisi majaji tunayabeba mapungufu hayo kwa asilimia 100”, Dr. Abdalla Mohammed alisema Jaji.

Bi Nasra Mohammed, mwandishi wa habari mkongwe ambae pia alikua ni miongni mwa majaji amewahimiza waandishi kuandika kazi zao katika viwango vya juu ili kuweza kuisaidia jamii katika masuala hayo ya takwimu.

"Sisi waandishi wa habari tufanye kazi kwa bora na zenye viwango kila siku ili kuweza kuipasha jamii taarifa sahihi zilizoshiba na kuleta tija katika jamii." Alisema Bi Nasra

Mwisho Dkt Mzuri alitoa wito kwa waandishi wa habari kuendelea kuandika habari zinazohusiana na wanawake, ikiwa ni pamoja na changamoto zinazokwamisha upatikanaji wa nafasi za uongozi.

Huu ni mwaka wa tatu mfululizo kufanyika kwa tuzo hizi, na kwa mwaka huu kumekua na ongezeko kubwa la idadi ya kazi zilizowasilishwa ambapo jumla ya kazi 529 kutoka vyombo vya habari mbalimbali Zanzibar ziliwasilishwa.

Tuzo hizi zinafanyika ikiwa ni utekelezaji wa mradi wa kuongeza ushiriki wa  wanawake katika nafasi za uongozi ambao unatekelezwa na TAMWA ZNZ, ZAFELA na PEGAO kwa ushirikiano mkubwa na ubalozi wa Norway ambapo Kaulimbiu ya Tuzo hizi ni "Kalamu Yangu, Mchango Wangu kwa Wanawake" inayoakisi dhamira endelevu ya waandishi wa habari kuongeza sauti za wanawake na kuchangia katika maendeleo yao.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.