Na Munir Shemweta, MLELE.
Mkuu wa wilaya ya Mlele mkoani Katavi Alhaji Majid Mwanga
amesema wahusika wote wa ubadhilifu wa fedha shilingi
39,501, 665 katika kijiji cha Kibaoni halmashauri ya Mpimbwe
wilaya ya Mlele mkoa wa Katavi watachukuliwa hatua kwa
mujibu wa sheria.
Alhaji Mwanga ametoa kauli hiyo katika mkutano wa hadhara
na wananchi wa kijiji cha Kibaoni wakati wa uwasilishaji
taarifa ya uchunguzi wa mapato na matumizi iliyotokana na
migogoro ya ardhi katika kijiji cha Kibaoni iliyosomwa na
Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri ya Mpimbwe Bi.
Shamim Daud.
‘’Hatutamfumbia macho mtu hata tone moja, baadhi ya
viongozi wa kijiji na wao wamehusika kwenye upotevu wa
milioni 39, 501, 665 wote hao walihusika lakini na watu
ambao ni nje ya serikali ya kijiji walihusika kama ilivyosemwa
mmoja wa watumishi yuko kampuni hiyo’’. Alisema Alhaji
Majid Mwanga.
Akiwasilisha taarifa ya uchunguzi wa mapato na matumizi
iliyotokana na migogoro ya ardhi kwenye kijiji cha Kibaoni,
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mpimbwe wilaya ya
Mlele Bi. Shamim Daud amesema, maeneo yaliyohusika
katika ubadhilifu ni pamoja na eneo la shule mpya ya Kibaoni
ambapo wakati wa kupatikana kwake ilipunguzwa ekari 3 na
kuwa 15 badala ya ekari 18.
Eneo lingine kwa mujibu wa Mkurugenzi huyo Mtendaji wa
halmashauri ya Mpimbwe Bi.Shamim ni la Viwanda Vidogo la
SIDO ambapo fedha kiasi cha shilingi milioni 8.8 kwa ajili ya
mauzo ya viwanja 48 hazikupelekwa benki na hakuna
matumizi yoyote yaliyoonekana ya shughuli za serikali.
Aidha, makusanyo ya mapato ya shilingi 21,240,000 kutoka
vyanzo vya mapato mbalimbali ya kijiji cha Kibaoni
yanayojumuisha michango ya jamii, kukodisha mashamba,
tozo na faini mbalimbali kiasi kilichopelekwa benki kati ya
jumla ya milioni 21,240,000 ni shilingi milioni 2 tu huku
kisichopelekwa benki ni 1,9210,000.
‘’Kumetokea pia ubadhilifu wa fedha za kijiji kutoka katika
akaunti yake ya jumla ya milioni 2.80 zilizotolewa katika
kaunti kwa ajili ya kurejesha kwa watu 39 wakati hakuna
fedha yoyote iliyoingizwa kutokana na tukio hilo’’. Alisema Bi.
Shamim.
Kuhusu malipo ya fidia kwa serikali ya kibaoni kutokana na
maeneo ya wananchi kuchukuliwa kwa ajili ya kuchimba
vifusi na kuchukua udongo kwa ajili ya ujenzi wa barabra ya
kibaoni- Sitalike, amesema pamoja na kijiji cha Kibaoni
kupokea shilingi milioni 21 kutoka kampuni ya RSG Ltd na
wananchi wawili nao kufidiwa lakini pesa zote hazikupelekwa
benki. Kwa mujibu wa ripoti ya uchunguzi baadhi ya viongozi
wa kata, watendaji wa vijiji na watumishi wa kampuni ya RSG
walishiriki kugawana fredha za fidia.
Baadhi ya wananchi wa kijiji cha Kibaoni wametaka hatua za
kisheria zichukuliwe kwa wote waliohusika kwenye ubadhilifu
wa fedha ikiwemo kurejesha fedha walizochukua.
‘’Hizi pesa zote zirudi ili kupunguza msongamano wa mizigo
iwe kuuzwa nyumba, iwe kiwanja au kufanya nini pesa zote ili
anayekuja leo kibaoni ajue anapodokoa hata hata mia tano ya
kula ya wizi ajue hii ni pesa inayoweza kuniunguza’’ alisema
Mathelius Matabula.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na
Maendeleo ya Makazi na Mbunge wa jimbo la Kavuu Mhe,
Geophrey Pinda ametaka sheria ifuate mkondo wake huku
akisisitiza kutaka fedha iliyoibwa kurudi kwa wananchi kwa
kuwa tangu fedha hizo zipotee miradi mingi imesimama.
Mkuu wa wilaya ya Mlele
Alhaji Majid Mwanga amemuelekeza mkurugenzi kuchukua
hatua kwa watumishi wote waliohusika sambamba na kuiarifu
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa
(TAKUKURU) pamoja na Jeshi la Polisi ili hatua za
kuwakamata waliohusika wote ifanyike.
Tarehe 3 Novemba 2023 Mkurugenzi mtendaji wa
halmashauri ya Mpimbwe alielekeza ufanyike ukaguzi wa
mapato na matumizi ya kijiji cha Kibaoni ikiwa ni pamoja na
kuhakiki hoja zilizoibuliwa kwenye taarifa ya Kamati huru ya
uchunguzi wa migogoro ya ardhi kijiji cha kibaoni ambapo
kazi ya ukaguzi ilianza 9 Novemba 2023 na kukamilika
25/3/2024. Miongoni mwa mambo yaliyobainika ni kuwepo
kwa ubadhilifu wa fedha za umma na matumizi mabaya ya
madaraka yaliyosababisha baadhi ya viongozi wa kata,
viongozi na wajumbe wa serikali ya kijiji kuwa ni pamoja na
watumishi kujinufaisha kwa kujigawia viwanja bila kufuata
taratibu.
No comments:
Post a Comment