Habari za Punde

MBETO: AKUTANA NA BARAZA LA WAZEE CCM ZANZIBAR.

KATIBU wa Kamati Maalum ya NEC,Idara ya Itikadi,Uenezi na Mafunzo CCM Zanzibar Khamis Mbeto Khamis,akizungumza na Baraza la Wazee CCM Zanzibar  huko Ofisini kwao Kisiwandui Zanzibar.

Na.Mwandishi Wetu ZANZIBAR.

KATIBU wa Kamati Maalum ya NEC,Idara ya Itikadi,Uenezi na Mafunzo CCM Zanzibar Khamis Mbeto Khamis,amewasihi Wazee wa Chama Cha Mapinduzi nchini kuendelea kutoa ushauri,maoni na mapendekezo ya kuimarisha Chama na Jumuiya zake.

Hayo ameyasema wakati akizungumza na Baraza la Wazee wa CCM Zanzibar alipowatembelea ofisini kwao Kisiwandui Zanzibar,amesema Chama Cha Mapinduzi kinajivunia kuwa na Wazee wenye uwezo,uzoefu,busara na hekima za kuimarisha taasisi hiyo ya kisiasa.

Mbeto, alieleza kuwa mafanikio yaliyopatikana katika Chama Cha Mapinduzi na Serikali zake yametokana na ushauri wa kundi hilo muhimu lenye watu wenye uzoefu mkubwa katika sekta za umma na binafsi.

“Wazee wangu nyinyi ni kundi muhimun sana ndani ya Chama chetu kwani busara zenu ndio chachu ya mafanikio haya tuliyonayo hivi sasa, nakuombeni sana endeleeni kutushauri ili tuweze kufanya vizuri zaidi kwa kila jambo jema linalojitokeza mbele yetu.”, alisema Mbeto.

 Naye Mwenyekiti wa Baraza la Wazee Zanzibar Khadija Jabir Mohamed, amesema baraza hilo linaridhishwa na kasi ya utendaji wa viongozi na watendaji wa Chama Cha Mapinduzi Afisi Kuu ya CCM Zanzibar.

Katika maelezo yake Mbeto, alisema mafanikio yaliyofikiwa ni kutokana na utendaji uliotukuka wa Mwenyekiti wa CCM Taifa ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan pamoja na Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar ambaye pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Mwinyi na kwamba viongozi hao wamekuwa ni mfano wa kuigwa katika kuwatumikia wananchi kwa vitendo.

Khadija, aliwasihi viongozi hao kuendeleza kasi hiyo ili kufikia malengo ya utekelezaji wa Katiba ya CCM ya mwaka 1977 toleo la Disemba 2022 ibara ya 5 kuhakikisha CCM inashinda katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa pamoja na Uchaguzi Mkuu wa dola.

Nao baadhi ya Wajumbe wa Baraza hilo, wamesema kwa sasa Chama Cha Mapinduzi kipo salama kutokana na ufanisi wa utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2020/2025 inayotekelezwa kwa kasi kubwa katika sekta mbalimbali nchini.

Wasema kuwa matarajio yao ni kuona CCM inapata ushindi mkubwa kwa kila uchaguzi unaofanyika nchini ili Chama kiendeleze utamaduni wake wa kupata ushindi katika michakato ya chaguzi mbalimbali zinazoebndeshwa nchibni kwa misingi ya demokrasia.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.