Habari za Punde

Waziri Mhagama aipongeza Sukos Kova foundation kwa Kuandaa mafunzo ya Uokoaji

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama akiwa na Kamishna Mstaafu Suleiman Kova, wakati akifungua mafunzo ya pamoja ya uokoaji kwenye maji mbele ya boti, kwa vikosi vya Jeshi la Polisi Wanamaji, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji pamoja na vikundi mbalimbali vya uokoaji katika ngazi ya jamii.

Na Mwandishi wetu

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama amepongeza taasisi ya Sukos Kova Foundation na taasisi ya Peaceland Foundation kwa pamoja kwa kushirikiana taasisi za uokoaji Serikalini kwa kuandaa mafunzo maalumu ya uokoaji kwenye maji.

Ametoa pongezi hizo wakati wa hafla ya kufungua mafunzo hayo yaliyohusisha vikosi vya Jeshi la Polisi Wanamaji, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji pamoja na vikundi mbalimbali vya uokoaji katika ngazi ya jamii iliyofanyika tarehe 09Juni, 2024 Sawasawa Bay Mikocheni, Dar es salaam.

Amesema boti iliyokabidhiwa Ofisi ya Waziri Mkuu itaenda kwenye maziwa mito na maeneo mbalimbali ili ikakutane na taasisi za uokoaji na vikundi vya jamii ambavyo vitakuwa tayari kwa mafunzo.

Waziri Mhagama amesema, “maamuzi hayo ni ya kizalendo na tutaendelea kuheshimu uwepo wa taasisi hizo binafsi, ikiwa ni pamoja na utaratibu ambao zitakuwa zimejiwekea katika kuleta tija kubwa kwa taifa na ustawi wa Watanzania.”

Aliongezea kuwa matumizi ya uokoaji yanaenda sambamba na matumizi ya vifaa hivyo na kutoa wito juu ya utoaji wa elimu kuhusu matumizi sahihi ya vifaa, kwa wakati sahihi na mahali sahihi pale ambapo vitahitajika ili viweze kukabiliana na maafa pindi yanapotokea.

"Boti iliyokabidhiwa ni boti ya kisasa na kwa sababu mambo ya uokoaji ni mambo mtambuka yataenda sambamba na uzuiaji wa uhalifu, na inaweza kutumika pia kuzuia uhalifu kwenye maeneo ya maji katika Taifa letu.”alisema Mhe. Mhagama

Ofisi ya Waziri Mkuu itaendelea kushirikiana na taasisi nyingine za kiraia ili kuweza kufika maeneo mbalimbali yenye uhitaji wa kupata mafunzo ya uokoaji.

Aidha alitoa rai kwa taasisi za uokoaji na vikundi vya uokoaji kuhakikisha wanatunza vifaa vilivyotolewa ili viweze kudumu kwa muda mrefu huku vikiendelea kutoa msaada wa uokoaji .

Watakaopokea mafunzo watumie vizuri maarifa hayo ili waweze kufunza wengine na kusaidia kundi kubwa  kunufaika na mafunzo hayo ambayo yatatolewa kwa muda wa wiki mbili, alisistiza

Waziri amesema, “ni vyema taasisi za uokoaji na vikundi vya uokoaji vikatumia elimu itakayotolewa kwa uzalendo mkubwa pindi tutakapokutana na majanga ya maafa.”

Waziri Mhagama alizikumbusha taasisi Sukos Kova Foundation kuendelea kufungua milango ili taasisi nyingine ambazo zinapenda kufanya ushirikiano na taasisi hiyo kwenye masuala ya uokoaji wawe tayari kushirikiana.

Kwa upande wake Katibu Tawala wa Mkoa wa Dar es Salaam Dkt, Koba Nguvila amesema Mkoa wa Dar es salaam unaguswa kwenye habari ya uokoaji na mafaa kwa sababu Mkoa huo unapata mafuriko na madhila ya kuchafuka kwa bahari.

Amesema kuwa hili ni jambo la faraja kwa taifa, pindi inapotokea jamii imezungukwa na maji unatumia vifaa vya kisasa vya uokoaji hivyo kusaidia kuimarisha usalama  wa kuokoa watu.

Naye Kamishna Mstaafu Suleiman Kova, amesema ya Sukos Kova Foundation kwa kushirikiana taasisi ya Peaceland Foundation wametoa boti Moja ili liweze kuogeza nguvu katika miundombinu iliyopo kazini.

"Tumeona tumpatie Jaketi la Uokoaji (Life JacketRais) Dkt. Samia Suluhu Hassani kwa sababu amekuwa mstari wa mbele kutoa maelekezo makubwa wakati Maafa yanapotokea," alisema

Awali Mkuu wa Wajumbe kutoka Peaceland Foundation Bi. Jing Ping, amesema nchi ya China na Tanzania wamekuwa na ushirikiano na mshikamano wa karibu kwa zaidi ya miongo sita sasa.

"Nchi zetu zimekuwa zikisaidiana katika mambo mbalimbali na tukio la leo ni moja ya ushahidi wa ushirikiano wetu, na katika hili taasisi yangu kwa kushirikiana na Sukos Kova Foundation zimejikita katika kuimarisha juhudi za kukabiliana maafa kwa kutoa vifaa mbalimbali vya kusaidia uokoaji.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama akizungumza na vikosi vya Jeshi la Polisi Wanamaji, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji pamoja na vikundi mbalimbali vya uokoaji katika ngazi ya jamii kabla ya Ufunguzi wa mafunzo ya uokoaji kwenye maji.
Watendaji wa Ofisi ya Mkoa wa Dar es salaam na Maafisa kutoka vyombo vya usalama pamoja na vikundi mbalimbali vya uokoaji katika ngazi ya jamii katika picha wakiwa katika hafla ya kufungua mafunzo ya pamoja ya uokoaji kwenye maji kwa vikosi vya Jeshi la Polisi Wanamaji, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji pamoja na vikundi mbalimbali vya uokoaji katika ngazi ya jamii.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama akipokea jaketi la uokoaji (Life Jacket) Kutoka kwa Kamishina Mstaafu Selemani Komba lilotolewa Maalumu kwa ajili ya Mheshimiwa Rais Dkt.  Samia Suluhu Hassan.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.