Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB), Mhe. Bahame Tom Nyanduga akiwa ameambatana na Kamishna wa Tume, Mhe. Ali Rajab (kushoto) na Katibu Mtendaji wa Tume, Bibi Mary Massay (kulia) akisoma tamko la Tume kuhusu zuio la polisi la mikutano na maandamano ya vyama vya siasa mbele ya vyombo vya habari leo (Agosti 10, 2016) mchana. Mkutano huo na vyombo vya habari ulifanyika Makao Makuu ya ofisi za Tume, Mtaa wa Luthuli jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya wanahabari wakimsikiliza Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB), Mhe. Bahame Tom Nyanduga akitoa tamko la Tume kuhusu zuio la polisi la mikutano na maandamano ya vyama vya siasa mbele ya vyombo vya habari leo (Agosti 10, 2016) mchana.
(Picha zote na Getrude Alex wa THBUB)
|
TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA
BORA
Kitalu Na. 8, Mtaa wa Luthuli
S.L.P 2643, DAR ES SALAAM
Simu: +255 22 2135747/8; 2137125;
2135222
Faksi: +255 22 2111281
Tovuti: www.chragg.go.tz
|
Agosti 10,
2016
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala
Bora, iliandaa mkutano leo tarehe 10/08/2016 ili kuzungumzia tamko la Jeshi la
Polisi la tarehe 07/06/2016 la kuzuia mikutano na maandamano ya vyama vya siasa
isiyo ya kiutendaji, na tamko la CHADEMA kuhusu “UKUTA” na mikutano wanayopanga
kufanya tarehe 1 Septemba, 2016.
Mkutano huu ulihudhuriwa pia na Mhe. Jaji
Francis Mutungi, Msajili wa Vyama vya siasa, Mhe. Vincent Mashinji, Katibu Mkuu
wa CHADEMA na washauri wake na Ndugu Daniel Loya, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Demokrasia
nchini (TCD).
Hivyo mkutano wa leo ulikuwa na lengo
la kuwakutanisha viongozi wa Serikali, Jeshi la Polisi na CHADEMA na kwa pamoja
kutafuta ufumbuzi wa kile Tume inachohofia kuhusu uvunjifu wa amani, haki za
binadamu na utawala bora.
Aidha baada ya tamko la CHADEMA la
kufanya maandamano nchi nzima, kumekuwa na matamko mbalimbali kutoka kwa
viongozi wa kitaifa, baadhi ya wakuu wa mikoa na wilaya, Makamanda wa mikoa wa
Jeshi la Polisi kukataza kufanyika kwa maandamano hayo na kwamba watakaokiuka
zuio hilo “watashughulikiwa.”
Ni katika mazingira haya, Tume imepata
wasiwasi kuwa endapo matamko haya yataachiwa yaendelee, yana viashiria vya
machafuko na uvunjifu mkubwa wa haki za binadamu unaoweza kutokea.
Mkutano huu kwa pamoja ulitaka
kujihakikishia iwapo Tume ina mamlaka ya kujadili hoja hizo mbili yaani
kujadili zuio la maandamano na mikutano ya vyama vya siasa, visiyokuwa vya
kiutendaji na kuhusu lugha na matamshi yasiyo stahiki.
Baada ya majadiliano Tume inapenda
kutamka yafuatayo:-
1. Wajumbe wote waliohudhuria kikao hicho
walikubaliana kuhusu umuhimu wa kudumisha amani nchini, na umuhimu wa kuwepo
majadiliano katika kutafuta maafikiano ya tofauti zozote kila mara
zinapojitokeza, na walipendekeza umuhimu wa kuendelea na majadiliano
yaliyoanzishwa na Tume.
2. Kwamba kuhusiana na mustakabali wa
maandamano na mikutano ya vyama vya siasa ilibainika kuwa kuna kesi mbili
zilizofunguliwa na CHADEMA katika Mahakama Kuu, Masijala ya Dar es Salaam na
Mwanza na kesi zote zinaendelea. Kwa
kuzingatia Ibara ya 131 (2)(a) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
1977, inaamini kwamba, tafsiri sahihi ya zuio lilitolewa na Polisi litapatikana
Mahakamani. Tume inaamini Mahakama itayapa
mashauri hayo kipaumbele, kama ilivyofanya wakati wa kusikiliza kesi ya mita
mia mbili hapo Oktoba, 2015 ili tafsiri yake ipatikane mapema.
3. Pamoja na uamuzi huo wa Tume, kwa
kuzingatia mamlaka ya Tume chini ya Ibara 130 (1) (g) na (h) ya Katiba ya nchi,
kuhusu kutoa ushauri na kutafuta maelewano kati ya viongozi wa Serikali na
Jeshi la Polisi kwa upande mmoja, na uongozi wa CHADEMA, Tume inawaasa viongozi
wa pande mbili kuzingatia yafuatayo:-
(i)
Kusitisha matumizi ya lugha au maneno yenye viashiria vya
uvunjifu wa amani, haki za binadamu na utawala bora kwani lugha hizi hazikidhi
matakwa ya haki za binadamu, wala utawala wa sheria.
(ii)
Jeshi la Polisi linashauriwa lisitumie neno
“tutawashughulikia wote watakao kaidi amri”, kwa kuwa Tume inaona kuwa maneno
hayo yanaweza kusababisha matumizi mabaya ya mamlaka ya Jeshi la Polisi.
(iii)
CHADEMA warekebishe msamiati wa mikutano wanayopanga na
kuondoa neno “UDIKITETA” katika mikakati yao ya kisiasa kwani Tanzania, ni nchi
yenye taasisi za kidemokrasia na inaheshimu utawala wa Sheria, na ndiyo sababu
CHADEMA wamekwenda Mahakamani.
(iv)
Kwa kuzingatia, ukweli kwamba kuna mashauri mawili yaliyoko
Mahakamani, ambayo yatawezesha Mahakama kutoa tafsiri ya uhalali wa zuio la Jeshi
la Polisi la tarehe 7 Juni, 2016 kuhusu maandamano na mikutano ya vyama vya
siasa, Tume inashauri kwamba, pande zote mbili ziheshimu Mahakama na ziache
kutoa matamko ambayo yanaendelea kuongeza joto kuhusu uwepo au kutokuwepo
maandamano na mikutano ya tarehe 1 Septemba, 2016.
(v)
Tume inaishauri CHADEMA kusitisha maandamano yake ili
kutoa nafasi kwa Mahakama kufanya kazi yake kwa umakini bila shinikizo la muda
kati ya sasa na tarehe 1 Septemba, 2016.
Iwapo ushauri huu hautazingatiwa, Tume
inatahadharisha kwamba kuna uwezekano mkubwa wa kuwepo na uvunjifu wa haki za
binadamu na iwapo itatokea hivyo wahusika wote pia itabidi wawajibike.
Imetolewa na:
(SIGNED)
Bahame Tom Nyanduga
Mwenyekiti
TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA
Agosti 10, 2016
No comments:
Post a Comment