Sheha wa Shehia ya Tomondo Wilaya ya Magharibi Mkoa Mjini Magharibi Bwana Mohd Omar Said { Maarufu Kidevu } akielezea mkasa uliompata wa kumwagiwa Tindi kali { Acid } mbele ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi aliyefika Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja kumfariji.
Picha na Hassan Issa wa –OMPR – ZNZ.
Na Othman Khamis Ame, OMPR
Sheha wa Shehia ya Tomondo Wilaya ya Magharibi Bwana Mohd Omar Said { Maarufu Kidevu } anaendelea kupatiwa huduma za matibabu katika Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja baada ya kumwagiwa Tindi kali { Acid } na mtu asiyejuilikana.
Mkasa huo umempata jana usiku mara baada ya kurejea ibada ya sala ya Isha wakati akiendelea na harakati za kutafuta huduma za maji na kumwagiwa tindi kali hiyo iliyoathiri eneo la kifua chake, Bega pamoja na sehemu za jicho la kulia.
Hili ni tukio la tatu kutokea ndani ya mkoa wa mjini Magharibi likiwahusisha aliyewahi kuwa Mkurugenzi wa Baraza la Manispaa Ndugu Rashid Ali Juma pamoja na Katibu wa Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Fadhil Suleiman Soraga.
Sheha huyo wa Tomondo Bwana Mohd Omar Kidevu akizungumza na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi aliyefika Hospitali hapo kumfariji pamoja na kumpa pole alisema alijikuta akimwagiwa tindi kali majira ya saa 2.00 za usiku na mtu asiyemfahamu.














