Habari za Punde

WANANCHI WAASWA KUTUMIA NAMBA YA MALIPO WANAPOLIPIA HUDUMA ZA SERIK

Afisa Mwandamizi kutoka Idara ya Usimamizi wa Mifumo ya Fedha na TEHAMA wa Wizara ya Fedha, Bw. Charles Maganga (kulia), akitoa maelezo kuhusu umuhimu wa mwananchi kudai Namba ya Malipo (Control Number) pindi wanapotaka kufanya malipo ya Huduma za Serikali, kwa baadhi ya wananchi waliotembelea Banda la Wizara ya Fedha kwenye Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara Dar Es salaam (Sabasaba) yenye kaulimbiu ya “Maonesho ya Kibiashara ya Kimataifa Sabasaba, Fahari ya Tanzania” ambayo yameanza  tarehe 28 Juni na kutarajiwa kuhitimishwa Julai 13 mwaka huu.

Na.Peter Haule na Joseph Mahumi, WF, Dar es Salaam

Wananchi wametakiwa kutumia Namba ya malipo (Control Number) kila wanapofanya malipo ya Serikali ili kuwa na uhakika wa malipo waliyofanya yanafika mahali sahihi kwa ajili ya kutumika katika shughuli mbalimbali za maendeleo zikiwemo za ujenzi wa miundombinu ya afya, elimu na maji.

Hayo yamesemwa na Afisa Mwandamizi kutoka Idara ya Usimamizi wa Mifumo ya Fedha na TEHAMA wa Wizara ya Fedha, Bw. Charles Maganga, alipokuwa akitoa elimu ya matumizi ya namba ya malipo (Control Number) kwa malipo ya Serikali kwa wananchi waliotembelea Banda la Wizara ya Fedha kwenye Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara Dar Es salaam (Sabasaba) yenye kaulimbiu ya “Maonesho ya Kibiashara ya Kimataifa Sabasaba, Fahari ya Tanzania” ambayo yameanza  tarehe 28 Juni na kutarajiwa kuhitimishwa Julai 13 mwaka huu.
 
Alisema kuwa mwananchi mwenye  Simu Janja, anaweza kufanya malipo kwa njia ya kupakua GePG App ambayo itampa mwongozo wa ulipaji ambao unaambatana na faida lukuki zikiwemo kuwa na kumbukumbu za malipo na kuweza kupata risiti ya malipo.

Pia Bw. Maganga alisema kuwa kwa wale wanaotumia simu za kawaida wanaweza kufanya malipo kwa kutumia Namba ya Malipo kwa kubonyeza *152*00# kisha kufuata maelekezo  njia ambayo ni rahisi kwa watanzania wengi kufanya malipo kwa usahihi.

Alisema Taasisi za Umma, Mashirika  na Kampuni zimeunganishwa na Mfumo wa GePG ili kurahisisha ufanyaji wa malipo ya Serikali kwa urahisi, uhakika na uwazi.

Alisema utaratibu wa malipo ni rafiki na hupunguza muda wa kupata huduma kwa kukaa muda mrefu kwenye foleni, utaratibu huo pia unadhibiti mapato, unasaidia kupata taarifa sahihi za mapato ya Serikali kwa wakati.

Bw. Maganga amewahakikishia wananchi kuwa pindi wafanyapo malipo kwa kutumia Namba ya Malipo wawe na uhakika kuwa fedha zao zinafika sehemu iliyokusudiwa kwa ajili ya kutekeleza masuala mbalimbali ya maendeleo yenye kulenga ustawi wa Wananchi na Taifa kwa ujumla.

Amewatahadharisha wananchi kuepuka kufanya malipo ya huduma za Serikali nje ya Namba ya malipo kwa kuwa kunatengeneza mazingira ya watu wasio waadilifu kutumia mwanya huo kutumia fedha kinyume na kusudio la Serikali.

Aidha  Bw. Maganga amewataka wananchi kutembelea Banda la Wizara ya Fedha katika Maonesho ya Sabasaba ambapo watapata elimu kwa kina kuhusu matumizi ya Namba ya Malipo na GePG App.

Banda la Wizara ya Fedha katika Maonesho ya Sabasaba limesheheni wataalamu kutoka Idara na Vitengo vya Wizara hiyo na Taasisi zake ikiwa ni pamoja na Bodi ya Wataalam wa Ununuzi na Ugavi (PSPTB), Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu (NBAA), Mfuko wa Dhamana na Uwekezaji Tanzania (UTT AMIS), Mfuko wa Self Microfinance, Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) na Soko la Bidhaa Tanzania (TMX).

Taasisi nyingine ni pamoja na Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), Baraza la Masoko ya Mitaji (CMT), Benki ya Maendeleo TIB na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), Hazina SACCOS, Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA), Mamlaka ya Rufaa za Zabuni za Umma (PPAA) na Wakala wa Huduma ya Ununuzi Serikalini (GPSA).
 
Mwisho.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.