Habari za Punde

CCM Z'bar yasema haitowavumilia watu wanaopora mali zake

Na Is-haka Omar, Zanzibar.

CHAMA cha Mapinduzi Zanzibar kimesema hakitowavumilia baadhi ya watu wachache  wanaotumia hati bandia  kupora mali za chama hicho kwa makusudi.

Hayo ameyasema Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar katika mwendelezo wa ziara ya kuhakiki na kukagua mali za Chama na Jumuiya zake huko katika jengo la mradi wa UVCCM  Zanzibar uliopo darajani Unguja.

Vuai alieleza kwamba CCM itawachulilia hatua za kisheria baadhi ya watu watakaobainika kupora mali zake, kwani watakuwa sio watu wema wanaotaka chama hicho kisonge mbele kimaendeleo.

Alisema  CCM italinda mali zake kwa gharama yoyote ili kuhakikisha hazihujumiwi na baadhi ya watu wachache wasiokitakia mema chama hicho.

Alieleza kwamba chama hicho kitapambana na watu wanaohujumu mali za chama  hata kama watakuwa wanatoka ndani ya chama hicho.

Aliwataka viongozi wa CCM na jumuiya zake kuhakikisha wanalinda na kusimamia vizuri mali za chama hicho ili zibakie kuwa katika ulinzi wa kudumu.


Vuai alisema bila ya kuweka mikakati endelevu ya kulinda rasilimali za chama hicho zitapotea kidogo kidogo na kumalizika kabisa na kumilikiwa na watu wachache wasiopenda kuona CCM inapata maendeleo.

“ Mali hizi hazikubatikana kirahisi kama ambavyo baadhi ya watu wanaojimilikisha rasilimali zetu kinyume na sheria wanavyodhani, mimi nawambia waache tabia hiyo na ambao tayari wameshachukua wazirejeshe mapema vinginevyo watapambana na mkono wa sheria.’, alisema Vuai.

Naye Kaimu Naibu Katibu Mkuu wa UVCCM Zanzibar, Abdulghafar Idrissa alisema mradi huo unaosimamiwa na umoja huo kwa kushirikiana na mwekezaji mzalendo wa Kampuni ya Mishely Co. LTD unaendelea vizuri licha ya kuwepo kwa changamoto za kiutendaji zinazokwamisha mradi huo kutokamilika kwa wakati.

Alisema endapo Chama na jumuiya kwa kushirikiana na mwekezaji huyo watakaa pamoja kwa kujadiliana  ili wapate maamuzi ya pamoja yatakayosaidia kutatua changamoto hizo kwa haraka.      

Idrissa alikiahidi chama hicho kuendelea kulinda mali za umoja huo ili zisiingie katika mikono ya watu wenye tabia za kitapeli.

Wakati huo huo alitembelea eneo la chama hicho lililopo makontena  Vikokotoni  Zanzibar , alisema CCM inakusudia kuanzisha mradi wa kujenga majengo  ya kisasa yatakayojumuisha maduka na ofisi  ili kuwatengenezea mazingira mazuri  wafanyabiasha wa maeneo hayo.

Aliwasihi  wafanyabiashara wa eneo hilo kutoa ushirikiano wakati chama hicho kitakapohitaji eneo hilo kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya kisasa.

Alisema lengo la CCM ni kuunga mkono juhudi za serikali za kuhakikisha Zanzibar inakuwa na majengo ya kisasa na yenye hadhi yatakayowavutia wafanyabiashara wakubwa kuwekeza katika eneo hilo .

Naibu Katibu Mkuu huyo alisema muonekano wa eneo hilo linalofanyiwa biashara kwa sasa umepitwa na wakati unahitaji uimarishwaji wa miundo mbinu unaoendana na mazingira ya sasa kibiashara.

Naye Mwenyekiti wa  Jumuiya ya Wafanyabiashara  wa Vikokotoni Zanzibar  Juma Said, alikipongeza Chama cha Mapinduzi  kwa kuendelea kushirikiana vizuri na wafanyabiashara wa eneo hilo na kuahidi kutoa ushirikiano kwa  Chama hicho.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.