Habari za Punde

Matokeo ya mitihani ya kidato cha pili, darasa la sita na saba hadharani

Na Miza Kona/Rahma Khamis Maelezo-Zanzibar 

Jumla ya wanafunzi 16,744 wamechaguliwa kuendelea masomo ya kidatu cha tatu kati ya wanafunzi 24,051 walioandikishwa  kufanya mtihani wa kidato cha pili katika skuli  za Unguja na Pemba  mwaka  jana.

Akitoa taarifa kwa waandishi wa Habari Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Ali Juma Shamhuna amesema  kiwango hicho cha ufaulu ni sawa na asilimia 69.6 ikiwa ni ongezeko la asilimia 4.0 ukilinganisha na matokeo ya mwaka jana.

Waziri Shamhuna  amesema  idadi ya wanafunzi wa kike waliofaulu ni  kubwa zaidi ukilinganisha na wanaume  ambapo  wanawake ni 9,794 na wanaume 6,950.

Kwa upande wa matokeo ya Darasa la saba Waziri Shamhuna amesema  jumla ya wanafunzi 24,235  kati ya wanafunzi 30,179 walioandikishwa wamechaguliwa kuingia kidato cha kwanza  sawa na asilimia 84.5, wanafunzi 51 wamechaguliwa kujiunga na madarasa ya vipawa  na wanafunzi 621 wamechaguliwa kujiunga na madarasa ya michepuo

Akitoa tathmini kwa wanafunzi wa Darasa la sita Waziri wa Elimu amesema kuwa jumla ya wanafunzi 25,773 wamechaguliwa kuiungia kidato cha kwanza  sawa na asilimia 99.6 ambapo wanafunzi 44 wamechaguliwa kujiunga  na madarasa ya vipawa.


Akitaja Skuli zilizofanya vizuri  zaidi kidato cha pili   Waziri Shamhuna amesema ni pamoja na Madungu ‘A’,  Mauwani na Mahonda . Darasa   la saba  ni Skuli ya Alikhamis Camp, Mjimbini na Kangani   na  darasa la sita ni Kibweni, Mkunazini na Konde.

Amezitaja Skuli zilizofanya vibaya  kitaifa kwa  kidato cha pili ni Mfurumatonga, Uzi, na Mchangani, skuli ya Chambani, Kandwi , Mwambe shamiani, Mfurumatonga, Chambani na Mahonda wamefanya vibaya darasa la sita na saba .

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali amesema katika mitihani hiyo kesi nne za udanganyifu zilijitokeza zote kwa wanafunzi wa darasa la  sita.

Aliwataja wanafunzi waliofanya vizuri zaidi  kidato cha pili ni Philip William Panduka kutoka Skuli ya Mikunguni, darasa la saba ni Farid Ali Hamad kutoka Ziwani na darasa la sita ni Seif Khamis Nassor kutoka Skuli ya Madungu ‘A’.

Waziri Shamhuna  amewataka wazazi na walezi wa wanafunzi ambao hawakufaulu mitihani hiyo kutovunjika moyo na badala yake amewashauri kuwapeleka vituo vya kujiendeleza. 

Waziri huyo wa Elimu ameahidi kufanya utafiti na kuzifuatilia skuli zilivyofanya vibaya ili kuweza kufahamu  tatizo  na kulitafutia  ufumbuzi unaofaa.
                      

2 comments:

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.