Habari za Punde

Naibu Waziri Mhe.Kanyasu Awapa Ahueni Wadau wa Misitu Nchini.

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Constantine Kanyasu ( wa pili kulia) akizungumza na  baadhi ya watumishi wa Shamba la Miti la Longuza wakati mara baada ya kutembelea bustani ya shamba la miti aina ya misindano  wakati Naibu Waziri huyo alipofanya  jana ziara yake ya kikazi katika wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro, Wa kwanza kulia ni Meneja wa Shamba hilo, Ernest Madatta
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Constantine Kanyasu akiwa ameshika mche wa mti wa Msindano katika bustani ya Shamba la Miti la Longuza wakati Naibu Waziri huyo alipofanya  jana ziara yake ya kikazi katika wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro, Wengine ni baadhi ya watumishi wa shamaba hilo wakiwa na kamati ya ulinzi na usalama wa wilaya hiyo
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Constantine Kanyasu akiwa anapanda mti jana mara baada ya kutembelea bustani ya miche ya miti ya Misindano  katika shamba la miti la Longuza katika wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro.

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Constantine Kanyasu akimwagilia mara baada ya kupanda mti jana katika bustani ya miche ya miti ya Misindano  katika shamba la miti la Longuza katika wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro. 
( Picha na Lusungu Helela-WMU)


Na.Lusungu Helela - Kilimanjaro.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe.Constantine Kanyasu ameiagiza Wakala ya Huduma za Misitu Tanzania   (TFS) iendelee  kuwaruhusu Wadau wa Misitu nchini hususan  wenye viwanda vya kuchakata mbao  waendelee kutumia mashine za zamani za kuchakata magogo walizonazo huku wakiendelea kujipanga kununua mashine za kisasa  kulingana na mabadiliko ya teknolojia.

Hatua hiyo inakuja kufuatia zuio lililotolewa na Serikali kwa  wamiliki wa viwanda hivyo kuacha  kutumia mashine za zamani za kuchakata magogo ambazo zimekuwa zikizalisha taka nyingi na  kusababisha upotevu mkubwa wa mbao.

 Akizungumza na Wadau wa Misitu  wenye viwanda vya mbao katika shamba la Miti la Longuza katika wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro, Mhe. Kanyasu  amewataka  waendelee kununua  mashine hizo ili waweze  kwenda na  mabadiliko ya teknolojia itakayowawezesha kudhibiti kiwango cha upotevu wa mbao katika viwanda vyao.

Naibu Waziri huyo ameielekeza TFS kuendelea kutoa  leseni na  mgao wa vitalu vya miti  kwa wamiliki wa viwanda wenye mashine za zamani ili  kutoa fursa  kwao kujipanga kununua mashine ambazo zinazalisha  taka chache wakati wa uchakataji wa mbao.

Hata hivyo, Mhe. Kanyasu  amewaeleza Wadau hao kuwa hatua iliyochukuliwa haiondoi maamuzi yanayowataka  kuwa na  mashine za kisasa za  kupunguza  hasara  ya upotevu mkubwa wa  mbao.

Aidha, ameongeza kuwa maamuzi ya kuwataka wamiliki wa viwanda vya mbao kutumia mashine hizo mpya yanakwenda sambamba na zuio lililokuwa limetolewa siku za nyuma la kuzuia matumizi ya misumeno ya Dingdong ambayo nayo ilikuwa ikisababisha upotevu mkubwa wa mbao.

Pia, Ameagiza TFS itoe  mikataba ya miaka miwili kwa Wamiliki wa viwanda vya mbao hali itakayowasaidia kutoa uhakika kwa wamiliki wa viwanda hivyo kuweza kukopesheka katika mabenki nchini.

Mhe. Kanyasu amefafanua kuwa Benki zilizo nyingi zimekuwa zikitoa mkopo wa muda wa miezi 12 hali itakayowasaidia Wafanyabiashara hao kuwa na uwezo wa kurudisha pesa walizokuwa wamezikopa endapo wataweza kupewa mikataba ya muda wa miaka miwili.

Katika hatua nyingine, Mhe. Kanyasu amewataka wadau wa misitu nchini hasa wenye viwanda vya mbao wafungue mashamba makubwa ya miti ili badae waanze kuvuna miti katika mashamba yao hali itakayosaidia kupunguza utegemezi kutoka kwenye mashamba ya miti ya serikali akitoa mfano wa nchi ya Finland ambayo uchumi wake unategemea kwa kiasi kikubwa misitu na wamiliki wakubwa wa mashamba ya miti.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Wamiliki wa Viwanda vya mbao kwa mikoa ya Kaskazini, Ibrahimu Shoo meishukuru Serikali kwa kuendelea kuwapa muda wa kutosha ili waweze kwenda na mabadiliko ya teknolojia kwa  kununua mashine za kisasa za kuchakata mbao.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.