6/recent/ticker-posts

Dk Shein kuendelea kuwainua Wasanii


  
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                               14.10.2015
---
MGOMBEA Urais kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Dk. Ali Mohammed Shein ameeleza azma yake ya kuendelea kuwainua wasanii hapa nchini kwa kutekeleza ahadi yake ya ujenzi wa studio za kisasa ambazo tayari zimekamilika na kuwekwa vifaa vyenye sifa na ubora wa pekee kwa shughuli za kurikodia.

Dk. Shein aliwataka wasanii hao kukaa mkao wa kula kwani lengo lake la kuwainua wasanii limefikiwa ambapo tayari ujenzi wa studio hizo za kisasa za kurikodi nyimbo na michezo ya kuigiza umekamilika na wakati wowote shughuli za kurikodi zitaanza.

Hayo aliyasema wakati alipokuwa akizungumza na wananchi pamoja na WanaCCM waliohudhuria katika mkutano wa Kampeni za uchaguzi kwa upande wa CCM uliofanyika katika uwanja wa mpira Chwaka, Jimbo la Chwaka, Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini Unguja.

Katika maelezo yake, Dk. Shein alisema kuwa studio hizo zimejengwa kwenye jengo jipya la zamani la Utangazaji la Sauti ya Tanzania Zanzibar, baada ya kufayiwa matengenezo makubwa na kuwekewa vifaa  hivyo vya kisasa.

Alisema kuwa lengo na madhumuni ya ujenzi wa studio hizo ni kuhakikisha wasanii wanaimarisha kazi zao za sanaa zao na kwenda na wakati uliopo kutokana na vifaa vya kisasa vilivyomo ndani ya studio hizo.

Dk. Shein alisisitiza kuwa wasanii watafaidika na huduma zitakazotolewa na studio hizo ambazo zitawasaidia kuondokana na usumbufu wanaoupata hivi sasa katika kurikodi kazi zao.

Studio hizo ni za kisasa ambazo ni za pekee kwa nchi za Afrika Mashariki ambapo vifaa vyake vinatoka nchini Uingereza na tayari vifaa hivyo vimeshafanyiwa majaribio na wakati wowote shughuli za kurikodi kazi za wasanii zinatarajiwa kuanza.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

Post a Comment

0 Comments