Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzani katika Umoja wa Mataifa, Balozi Tuvako Manongi, akichangia majadiliano kuhusu upokonyaji wa silaha na usalama wa kimataifa mwishoni mwa wiki, ambapo ametoa wito wa jumuiya ya kimataifa kushirikiana katika kuhakikisha kuwa silaha za maangamizi haziishii mikononi mwa makundi ya kihalifu.
Na
MwandishiMaalum, New York
Tanzania imetoa wito Kwa
Jumuiya ya Kimataifa kuhakikisha inashirikiana kuhakikisha kwamba silaha za maangamizi zikiwamo za nyukilia haziangukii mikononi mwa makundi ya kihalifu.
Wito huo umetelewa mwishoni mwa wiki
na Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Balozi Tuvako Manongi, wakati wa Mkutano kuhusu masuala ya uponyaji wa silaha na usalama wa kimataifa.
Katika mkutano huo wa kuzungumzia wengi walieleza wasiwasi wao kuwa ushirikiano wa karibu kati ya nchi ambazo zina silaha za nyukilia na zile ambazo hazina,
lakini huku zile ambazo zinamiliki silaha hizo zikiendelea kuziboresha na kujilimbikizia.
“Ni jambo la kusikitisha, badala ya kuzipunguza silaha hizi na hatimaye kuzitokomeza kabisa, nchi zinazomiliki silaha za nyukilia zinaendelea na kasi ya kuziboresha,
kuzifufua na kujilimbikiza”. Akasema Balozi Manongi.
Akabainisha kuwa mbaya Zaidi
hata zile nchi ambazo hazina
silaha hizo nazo sasa zinatafuta kila maarifa ya kuwa nazo.
Jamba oambalo amesema ni tishio kwa usalama wa
mwanadamu.
Amesisitiza kuwa ingawa ni miongo saba imekwisha kupita
lakini madhara ya matukio ya
Hiroshima na Nagasaki bado
yanaendelea na yapo hai miongoni mwetu.
Balozi Manongi akaongeza kuwa ni muhimu basi
utokomezaji wa silaha za nyukilia na teknolojia
inayoambatana nazo likaendelea kupewa kipaumbele pamoja
na kuwa na mikataba ya kisheria itakayosimamia jambo hilo.
Akasema kutokana na ongezeko la ulimbikizaji wa silaha za nyukilia,
Jumuia ya kimataifa inawajibu wa kushirikiana kuhakikisha kwamba silaha hizo na nyingine za maangamizi haziangukii mikononi mwa makundi ya kigaidi na kihalifu.
Pamoja na ukweli kwamba silaha za nyukilia na zingine za maangamizi bado ni tishio kubwa kwa uhai wa mwanadamu.
Balozi Manongi akasema kwa nchi zinazoendelea tatizo la
usambazaji na matumizi holela ya silaha ndogo na nyepesi zinaendelea kuwa janga kubwa kwa ustawi na maendeleo ya
bara hili na kwingineko.
Akimnukuu Katibu Mkuu wa zamani wa Umoja wa Mataifa Kofi Annan
kwamba madhara yatokanayo na matumizi holela ya silaha ndogo na nyepesi yameendelea kuwa makubwa sana na madhara yake ni makubwa pengine kuzidi mabomu ya
atomic yaliyoiangamizia Hiroshima
na Nagasaki.
Akizungumzia zidi kuhusu matumizi holela ya silaha ndogo na nyepesi, Mwakilishi huyo wa Tanzania anasema mirindimo ya risasi na hata matumizi ya silaha kali
zikiwamo za maangamizi, haiwezi au haitamhakikishia mwananchi maisha yenye hadhi,
utu, ustawi na maendeleo.
Akasema kuna uhusiano mkubwa baina ya Amani, usalama na utekelezaji wa Malengo ya maendeleo endelevu
ya (Agenda 2030) malengo yanayojikita katika kumaliza umaskini pasipo kumwacha yoyote nyuma pamoja na kuilinda sayari ya dunia.
Akasema itakuwa vigumu kuyatekeleza malengo mapya ya maendeleo kama kiwango
cha gharama za kujilimbikizia silaha kitaendelea ambapo inakadiriwa kuwa mataifa hasa yale makubwa yanatumia
Zaidi ya dola za kimarekani trillion 1.7 kwa mwaka kwa matumizi ya silaha.
Akasema matumizi ya kiasi hicho cha
fedha kujilimbikizia silaha katika maghala mbali mbali duniani huku mamilioni ya watu wakiendelea kuishi katika umaskini uliopindukia,
na maelfu ya watoto wakiathirika kwa utapia mlo na wengine wakipoteza maisha kwa kukosa chakula na huduma nyingine za msingi ni jambo lisilokubalika.

0 Comments