Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhaj. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesema Serikali imejipanga kikamilifu kumaliza tatizo la usafiri na usafirishaji wa mizigo katika Kisiwa cha Pemba.
Akizungumza leo tarehe 17 Februari 2026 wakati wa ufunguzi wa Msikiti mpya wa Chachani, uliopo Chake Chake, Mkoa wa Kusini Pemba uliojengwa na mfanyabiashara Ndg. Said Nassor Bopar, Rais Dkt.Mwinyi amesema Serikali imeandaa meli mbili za mwendo kasi na ipo katika hatua za kutafuta meli maalum ya mizigo kwa safari za Unguja na Pemba.
Aidha, ameeleza kuwa Serikali imeliagiza Shirika la Meli la Zanzibar kuimarisha huduma zake na kubainisha kuwa meli ya MV Mapinduzi II itaanza kazi hivi karibuni baada ya matengenezo. Ameongeza kuwa uimarishaji wa bandari za Pemba utahamasisha sekta binafsi kuongeza vyombo vya usafiri.
Rais Dkt. Mwinyi amewahimiza waumini kuitumia misikiti kujadili changamoto za kijamii, akiwapongeza wafadhili wa msikiti huo kwa mchango wao.
Vilevile, amewasisitiza wafanyabiashara kutopandisha bei za vyakula wakati wa Ramadhan na kuwataka waumini kuongeza ibada na mshikamano.




0 Comments