Na Maelezo Zanzibar 23.03.2026
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imeanzisha mfumo wa kidijitali unaowezesha Wizara na Taasisi kusimamia na kuweka taarifa za huduma za Serikali kidijitali (Zanzibar Government Services Directory - ZGSD) ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma.
Akizungumza katika ukumbi wa Idara ya Habari Maelezo Zanzibar wakati akizungumza na waandishi wa habari katika siku 100 za Mafanikio za Uongozi wa Dk. Mwinyi, Wazir wa Mawasiliano, Teknolojia ya habari na Ubunifu Mhe. Mudrik Ramadhan Soraga amesema Serikali imeimarisha upatikanaji na matumizi ya teknolojia za kidijitali katika uendeshaji wa shughuli zake kwa ajili ya kutoa huduma bora.
Amesema Mamlaka ya Serikali Mtandao Zanzibar (eGAZ) imetekeleza mpango wa kupunguza matumizi ya karatasi kwa kuanzisha na kusimamia mifumo ya kielektroniki ikiwemo e-Office, BAMAS, HR-PayMIS, kwa Taasisi zote za Serikali pamoja na ERMS kwa Taasisi 16 zinazojitegemea, ZanVibali na ZanAjira.
“Mbali na kuongeza ufanisi, mifumo hii vile vile imelenga kuondoa utegemezi wa utumiaji wa karatasi, kupunguza gharama za uendesahaji, na kuongeza tija katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku” ameeleza Mhe. Soraga.
Aidha Waziri Soraga, amefahamisha kuwa kupitia mfumo huo huduma 42 zinatarajiwa kutolewa, hadi sasa Wizara na taasisi 17 tayari zimeshawasilisha taarifa zao kwa ajili ya kuingizwa katika mfumo huo.
Waziri Soraga amesema Serikali ina mpango wa kuanzisha mji wa kidijitali (Smart City) katika maeneo ya uwekezaji wa TEHAMA, Fumba ambapo Shirika la Mawasiliano Zanzibar (ZICTIA) imeendelea na kazi ya kutafuta wawekezaji kupitia ZIPA ili kutekeleza azma ya kuimarisha uchumi wa kidigitali.
“Pia kuiunganisha Zanzibar na mkonga wa kimataifa (International Gateway) kwa lengo la kuongeza ufanisi katika upatikanaji wa huduma za mtandao ambapo ZICTIA imeendelea na taratibu za manunuzi kwa lengo la kutangaza zabuni kwa ajili ya kumpata mkandarasi na mshauri elekezi (contractor na consultancy) pamoja na kuimarisha mfumo wa Serikali mtandao (e-Governance) katika utendaji wa Serikali ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa jamii” amefafanua Waziri huyo.
Akizungumzia sekta ya ubunifu Mhe. Soraga amesema kuwa Serikali imeanza maandalizi ya kujenga kituo cha ubunifu (Innovation Hub) katika eneo la Bwefum ambapo mradi huu unalenga kuanzisha mazingira rafiki yatakayowawezesha vijana kukuza vipaji vyao, kubuni teknolojia na kuendeleza mawazo ya ubunifu yatakayochangia ajira na uchumi wa kidijitali.
Aidha ameeleza kuwa Wizara imeweza kusaidia wasanii, wajasiriamali na wabunifu wa kitamaduni kuingia katika soko la kimataifa kupitia majukwaa ya kidijitali ili kuwawezesha vijana kujiajiri na kuchangia uchumi wa Zanzibar pamoja na kuendeleza tasnia ya ubunifu ili kuchangia ukuaji wa uchumi wa Zanzibar kupitia bidhaa za kitamaduni.
0 Comments