Habari za Punde

Dk.Shein: Amani, Utulivu Uliopo Usichezewe

Na Rajab Mkasaba, Ikulu

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, amesema kuwa amani na utulivu iliyopo nchini isifanyiwe mzaha na kutowaruhusu watu wachache kuirejesha Zanzibar katika hali ya mifarakano iliyokuwepo kabla.

Dk. Shein aliyasema hayo jana katika nyakati tofauti katika ziara yake ya Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Dk. Shein alisema kuwa Zanzibar tayari imeshajijengea sifa kubwa sana katika kuendeleza amani na utulivu na kwamba Mataifa mengi duniani yameelezea nia ya kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar katika kuleta maendeleo ya Zanzibar.

Amesema kuwa kila mwananchi hana budi kulinda amani na utulivu iliyopo ambayo imepatikana kwa jitihada kubwa kati ya viongozi na wananchi wa Zanzibar, hivyo kujitokeza watu wachache kuanza kutaka kuiondoa hali hiyo siyo jambo la busara.

Alisema wananchi wa Zanzibar wanaishi kwa umoja na mshikamano na hitilafu ziliondolewa ili Wazanzibari waishi vizuri kwa amani na utulivu na kamwe asitokee mtu akiwa na lengo la kuivunja amani iliyopo. “Jambo muhimu ni kuilinda imani na utulivu iliyopo na visitokee vishawishi vya aina yoyote vikataka kuoindosha amani iliyopo”,alisema Dk. Shein

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa Zazibar inahitaji amani na utulivu na vyama vya siasa visiwagawe wananchi na kufikia hatua ya kuvunja amani na utulivu nchini.

Dk. Shein alisema vyama vipo na vyama vikubwa viwili vilivyounda serikali ya Umoja wa Kitaifa ni CCM na CUF na vipo pale pale kubwa alilosisitiza ni kuendelea kushirikiana na kuaminiana hali ambayo inaenda vizuri huku akiwaeleza wananchi kuwa serikali ndiyo yenye muundo wa pamoja lakini vyama havijaunganishwa.

Pamoja na hayo Dk. Shein alisisitiza kuwa Zanzibar inaongozwa na Sheria na Katiba na kueleza kuwa lazima taratibu za nchi zikafuatwa na kuepukana na watu wachache ambao hufanya mambo bila ya wakati wake kufika.

Alisisitiza kuwa kama kuna jambo la serikali basi litasema na serikali na wala asitokee mtu akajifanya yeye bingwa na kuanza kuisemea serikali.

Wakati huo huo akiwa kijijini Matemwe Kigomani, Dk. Shein aliiagiza Wizara ya Ardhi, Makaazi Maji na Nishati ndani ya miezi sita iwe tayari imeshawapelekea huduma ya maji wananchi wa kijiji hicho cha Kigomani.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi Zazibar itaendelea kuimarisha sekta ya elimu na kuwapongeza wananchi wa kijiji hicho pamoja na wawekezaji waliokiunga mkono kwa asilimia sabini ujenzi wa madarasa mapya aliyoweka jiwe la msingi katika skuli ya Kigomani.

Mapema Dk. Shein alipokea taarifa ya Mkoa wa Kaskazini Unguja iliyosomwa mbele yake pamoja na kukabidhiwa taarifa ya utafiti wa Ubakaji katika Mkoa huo huko katika ukumbi wa chuo cha Amali Mkokotoni.

Taarifa hiyo pia, ilieleza kuwa tatizo la ardhi ndani ya Mkoa huo kama ilivyo katika mikoa mingine linaendelea kushughulikiwa na kutafutiwa ufumbuzi kwa njia muwafaka za kutatuliwa.

Ilieleza kuwa jumla ya migogoro 15 ya ardhi imeripotiwa ndani ya Mkoa huo wa Kaskazini ambapo Majimbo yanayoongoza ni Nungwi, Mkwajuni, Matemwe, Donge na Bumbwini na kuelezwa kuwa katika kutatua migogoro hiyo baadhi imeshatatuliwa Wilayani na baadhi ya kesi ziko Mahakamani na baadhi ziko katika ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais.

Katika ziara hiyo pia, Dk. Shein alifungua njia ya fusi huko Bwekunduni na mara baada ya ufunguzi huo alizungumza na wananchi huko katika soko la samaki Bwekunduni na kuwaeleza kuwa serikali ya Mapinduzi Zanzibar itaendelea kuwaunga mkono katika kuimarisha miradi yao ya maendeleo.

Dk. Shein alitoa pongezi kwa Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini A kwa ujenzi wa barabara hiyo, UUB paoja na Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano kwa mashirikiano ya pamoja katika ujenzi huo na kueleza kuwa barabara ni chachu ya maendeleo

Wakati huo huo Dk. Shein pia alifanya mazungumzo na wazee wa Tazari na Kilimani katika skuli ya Maandalizi ya Tazari na kuwaeleza wazee hao kuwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar itaendelea kuwaenzi na kuwatunza wazee wake na kueleza kuwa ataendelea kuziunga mkono shughuli zao za maulid na kusisitiza kuwa amani na utulivu ndio ngao ya maendeleo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.