Na Maryam Talib, Pemba
MKUU wa mkoa wa Kaskazini Pemba, Dadi Faki Dadi amezindua mradi wa serikali ya mtandao (e - government) kisiwani Pemba na kusema mradi huo utasaidia kurahisisha shughuli za kiutendaji serikalini.
Uzinduzi
huo ulifanyika skuli ya Utaani Wete ambapo alifanya mazungumzo ya moja kwa moja
kwa njia video kupitia kompyuta na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi, D. Ali Mohamed Shein aliyekuweko Mazizini Unguja.
Alisema
utaratibu huo wa kiutawala unatoa fursa kwa watendaji walioko mbali kijeografia
kuwasiliana kwa urahisi, kupeana maagizo, na mrejesho wa utekelezaji kwa
shughuli ambazo zinahitaji mwitikio wa haraka.
Akizungumza
katika mahojiano nje ya uzinduzi huo, Dadi alisema kwa kuanzia Mkoa wake
umejipanga kutumia utaratibu wa e- government kupambana na matatizo ya ubakaji
wa watoto, unyanyasaji wa wanawake, kilimo, usalama na magendo ya karafuu.
Alisema
kwa sasa kuna ugumu mkubwa kupata taarifa za mambo hayo hasa yale yanayohusiana
na ubakaji na unyanyasaji wa wanawake hali ambayo huchelewesha kupatikana kwa
ushahidi na kuchukuliwa hatua za kufaa.
Mapema
akimkaribisha Mkuu huyo wa Mkoa, Ofisa Mdhamini Ofisi ya Raisi Utumishi wa Umma
na Utawala bora, Maua Mohammed Salim alisema kuanzishwa
mpango huo ni sehemu ya utekelezaji wa mikakati ya wizara yake ya kuimarisha
utawala bora katika visiwa vya Zanzibar.
Alisema
uzinduzi uliofanyika ni hatua ya awali tu ya utekelezaji wa mkakati huo na
katika hatua zinazofuata mpango huo utaimarishwa zaidi kivifaa ili uweze kutumika
katika shule za msingi na sekondari na kuboresha utoaji wa elimu.
Mmoja
wa wanafunzi wa skuli ya Utaani aliehudhuria hafla hiyo, Mohammed Khamis aliipongeza
serikali kwa hatua hiyo muhimu akisema utawasaidia wanafunzi wa kisiwani Pemba kutafuta taarifa za kielimu na kuwasiliana na
walimu na wataalamu wengine walioko nje ya
kisiwa hicho.
Alisema
kwa sasa wanafunzi kisiwani Pemba wengi wao
wanategemea maktaba pekee kwa kupata vitabu vya kujifunzia na hawana fursa ya
kutumia mtandao kutafuta taarifa zaidi za kielimu.
Mradi
wa e- government umetekelezwa kwa mkopo nafuu kutoka serikali ya watu wa China
kwa gharama ya dola za Marekani milioni 19.
No comments:
Post a Comment