Habari za Punde

Ushindi wa Dk Shein ni kielelezo cha kuimarika kwa demokrasia Zanzibar - UVCCM


Na Mwandishi Wetu , Zanzibar 


Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi  (UVCCM ) umesema ushindi alioupata mgombea wa CCM Rais Dk Ali Mohamed Shein kwamba ni kielelezo cha kuimarika kwa msingi ya demokrasia Zanzibar na kukubalika kwa mgombea huyo kwa wapiga kura na wananchi wa Zanzibar . 



Umesema ushindi huo sasa umehitimisha mvutano na maneno yaliyokuwepo ambayo yalikuwa yakienezwa kwa makusudi ,  kupotoshwa na baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani visiwani humu. 



Kaimu Katibu mkuu wa UVCCM Shaka Hamdu Shaka ameeleza hayo Afisi kuu ya UVCCM Kikwajuni wakati akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kumaliza kwa maandamano makubwa yaliyoandaliwa na UVCCM kusherehekea ushindi wa CCM uliotangazwa  na Mwenyekiti wa Tume ya uchaguzi Zanzibar  Jecha Salim Jecha kulitangaza jina la Dk shein mshindi wa uchaguzi huo. 



Alisema ushindi alioupata Dk shein kwa kupata jumla ya kura  299,982 sawa na asilimia 91.4 kumeidhihirisha dunia jinsi ya kukubalika kwa kiongozi huyo katika aina ya utawala na uongozi wake. 




"Ameonyesha umahiri, upeo na uwezo mkubwa  katika kuongoza serikali ya umoja wa kitaifa kwa miaka mitano iliopita; amekuwa mstahamilivu na nguzo muhimu ili jamii isiendelee kugawanyika "alisema shaka 



Kaimu Katibu Mkuu alisema aina ya uongozi wa Rais Dk Shein ni wa kipekee na kwamba kama angekuwa si mtawala mwenye maarifa mapana na uvumilivu wa kisiasa serikali hiyo anaamini ingevunjika mapema. 



Shaka alisema serikai za mseto za Zimbabwe na Kenya ziliweza kuyumba  na kwamba hazikudumu kutokana na baadhi ya viongozi wake kukosa kuaminiana, kuvumiliana na kustahamiiiana .



"Ushindi huu ni pigo jipya kwa chama cha CUF ambacho kimesusia uchaguzi wa marudio bila sababu za msingi, ushindi wa Dk shein  naamini utaleta mageuzi makubwa ya kiuchumi  na kuishangaza dunia katika maendeleo ya demokrasia "alisems Shaka 



Aidha alisema anatarajia serikali mpya ijayo haitakuwa na viongozi wababaishaji na badala yake watateuliwa wazalendo, wachapa kazi na watu wenye uchungu wa kiyatetea Mapinduzi bila kushiriki usaliti. 



Hata hivyo Shaka alisema anaamini kuwa chini ya uongozi wa kipindi cha pili cha utawala Dk Shein na sera makini za ccm ,ataendelea kusimamia uadilifu serikalini,  kujenga umoja wa kitaifa nchini  pamoja na kuwatumikia wananchi ipasavyo na kudumisha huduma za jamii .



"UVCCM tuna matumaini makubwa na na Dk shein katika awamu mpya ya ushindi wake; ataunda baraza la mawaziri makini, na hatutosita kumpongeza kila atakapofanya vizuri  pia hatutakaa kimya pale tutakapoona mambo  hayaendi ipasavyo "alisema .



Shaka anewahimiza vijana mahali popote walipo kumuunga mkono Dk shein na kuisaidia serikali yake ili iweze kupiga hatua za kimaendeleo na kwamba hatawaangusha katika uongozi wake.



"Tunahitaji kutoka mahali tulipo na kufika tunakotarajia, tungependa kuona uwajibikaji mpya,utendaji wenye kubeba dhamira na utekelezaji wa malengo na sera hivyo ni wazi kuwa   wapatikane watu wenye uwezo na upeo ya kukwamua nchi mahali ilipo sasa" 

1 comment:

  1. ndugu muandishi tunaomba khabari za umeya dar, sisi ndio gazeti letu hili au unachaguwa cha kutukhabarisha?

    ReplyDelete

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.