Habari za Punde

Dk Shein aviagiza vyombo vya ulinzi na usalama kushirikiana kuwasaka wahalifu wa zao la karafuu

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
    Zanzibar                                              10 Septemba, 2016
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameviagiza vyombo vya ulinzi na usalama kushirikiana kwa pamoja kuhakikisha kuwa watu waliokuwa wakitaka kusafirisha karafuu nje ya nchi huko katika bandari ndogo ya kijiji cha Tondooni, Mkumbuu wilaya ya Micheweni, Mkoa wa Kaskazini Pemba hivi karibuni wanakamatwa mara moja na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.

Akizungumza wakati alipotembelea kituo kikuu cha karafuu cha Shirika la Taifa la Biashara Zanzibar (ZSTC) huko Wete leo kukagua karafuu hizo zilizokamatwa, Dk. Shein alisema uchunguzi ukifanywa kwa umakini watu hao watapatikana kwa kuwa wananchi wanawafahamu wanaofanya biashara ya magendo ya karafuu.

“Tukio hili limetushitua sote hivyo ni wajibu wetu sote kushirikiana kuwatafuta…hawa watu wana mtandao wao na naamini wananchi wanawafahamu” Dk. Shein alisema na kusisitiza kuwa hakuna simile katika kushughulikia suala hilo.

Taarifa ya Afisa Mdhamini wa shirika la ZSTC Pemba Abdullah Ussi ilieleza kuwa tarehe 03 Septemba, 2016 saa kumi na moja alfajiri askari wa Kikosi Maalum cha Kuzuia Magendo (KMKM) kilikamata vipolo 17 vya karafuu kavu na makonyo vipolo 4.

Taarifa hiyo ilibainisha kuwa baada ya uchunguzi ilibanika kuwa karafuu hizo zilikuwa zimechanganywa na unga wa makonyo yaliyosagwa na vipande vipande ambapo baada ya kupimwa karafuu zilikuwa na uzito wa kilo 549 wakati unga na uchafu mwingine huo ulikuwa na uzito wa kilo 200.

Baada ya kuona uchafu huo uliochanganywana karafuu hizo, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi alisema vitendo hivyo ni lazima vipigwe vita kwa nguvu zote kwa kuwa vinaharibu sifa za karafuu za Zanzibar.

“Huu ni uhalifu dhidi ya karafuu zetu na unahatarisha sifa ya karafuu zetu ambayo inatambulika ulimwenguni kote” Dk. Alisisitiza.

Dk. Shein alivitaka vyombo vya sheria kuwachukulia hatua zipasazo watu wanaothibitika kuhujumu zao hilo kwa kutumia Sheria ya Karafuu Namba 11 ya mwaka 2011ambayo imebainisha adhabu mbali mbali dhidi ya watu hao.

Akiwa pamoja na Mheshimiwa Rais, Waziri wa Biashara, Viwanda na Masoko Balozi Amina Salum Ali alionesha kutoridhishwa na kasi ya hatua zinazochukuliwa dhidi ya watu wanaoshukiwa kutenda uhalifu dhidi ya zao la karafuu.

“Ni lazima uchunguzi uharakishwe ili wanaopatikana na makosa wachukuliwe hatua za kisheria ili ujumbe ufike kwa wahalifu wengine” Balozi Amin alieleza.

Wakati huo huo Shirika la ZSTC limeeleza kuwa msimu huu linatarajia kununua kiasi cha tani 2,650 za karafuu kisiwani Pemba ambapo kati ya hizo tani 1,500 kutoka wilaya ya Mkoani, tani 800 wilaya ya Chake Chake, tani 300 wilaya ya Wete na tani 50 wilaya ya Micheweni.

Taarifa ya Afisa mdhamini wa ZSTC bwana Abdullah A. Ussi ilieleza kuwa hadi sasa wilaya ya Wete imeuza tani 134 sawa na asilimia 44.8 ambapo shirika hilo limekuwa na wasiwsi na kasi hiyo ndogo ya ununuzi hivyo wasi wasi huo unathibitishwa na kukamatwa kwa karafuu hizo.

Alibainisha kuwa karafuu zilizokamatwa kilo 549 ambazo baada ya kuchanbuliwa zilionekana kuwa ni za daraja la tatu zimeuzwa kwa shirika lake kwa jumla yahilingi 5,490,000/= ambazo zinashikiliwa na Jeshi la Polisi kama ushahidi katika kesi hiyo.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi yuko kisiwani Pemba kwa ziara ya siku tatu ambapo keshokutwa atakuwa mgeni rasmi katika Baraza la Eid litakalofanyika katika skuli mpya ya Mkanyageni iliyoko wilaya ya Mkoani, Mkoa wa Kusini Pemba.

Postal Address: 2422 Tel.+255 776 613 015, Fax: 024 2231822 
  E-mail: saidameir@ikuluzanzibar.go.tz

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.