Habari za Punde

Waziri Hamad Awataka Mabwana Shamba Pemba Kuwatembelea Wakulima Mashambani Kutowa Utaalamu Wao.

Na Salmin Juma. Pemba. 
Waziri wa Kilimo Maliasili Mifungo na Uvuvi Zanzibar Mh Hamad Rashid amewataka wataalamu wa kilimo kisiwani Pemba kuwatembelea wakulima mashambani ili kutambua changamoto zinazowakabili katika uzalishaji wao na hatimae kufikia lengo lililokusudiwa.
Amesema kuwa amebaini kwamba wakulima wengi kisiwani Pemba wanashindwa kuzalisha bidhaa zenye kiwango bora kutokana na kutokuwa na uwelewa wa kutosha juu ya ukulima bora.
Hayo ameyaeleza jana wakati alipofanya ziara ya kuwatembelea wakulima na wafugaji kwa lengo la kujua changamoto zinazowakabili pamoja na njia bora za kutumika katika kutatua changamoto hizo ili kupatikane tija kwa mkulima mwenyewe na taifa kwa ujumla.
Amesema wakulima wanakabiliwa na changamoto nyingi ambazo kwa namna moja ama nyengineyo huwakwaza kufikia malengo hivyo ni vyema mabibi na mabwana shamba kuwa karibu nao huku wakiwapatia elimu ambayo itawasaidia katika harakati zao hizo.
Katika hatua nyengine waziri Hamad Rashid amebahatika kutembelea katika mabwawa ya kuzalishia chumvi kangagani mkoa wa kusini Pemba ambapo amewataka wazalishaji hao kujitahid kuzalisha chumvi yenye kiwango na kuzingatia maelekezo wanayopata kutoka kwa wataalamu na wizara iko tayari kuwatafutia soko la uhakika la kuuzia bidhaa zao.
Mmoja miongoni mwa wazalishaji chumvi katika eneo hilo Ndg: Hamad Mohd Masoud ameonyesha kusikitishwa sana kwa kitendo cha baadhi ya watu wanaokata miti ya mikoko karibu na maeneo ya mabwawa yao na kuwasababishia uharibifu mkubwa ambao umepelekea hasara katika mabwawa yao huku akiitaka serikali kuwasaidia katika kuwadhibiti vijana hao.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.