Habari za Punde

Rais Dk Shein aongoza maziko ya Profesa Ishau



 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Ali Mohamed Shein (katikati) alijumuika na Waislamu,Viongozi mbali mbali na Wananchi katika kumswalia Marehemu Mzee Prof.Ishau Abdalla Khamis katika Msikiti wa Ijumaa Donge jana,Marehemu aliwahi kushika nyazifa mbali mbali katika Serikalia ya Mapinduzi Zanzibar na Chama cha Mapinduzi,[Picha na Ikulu.
 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Ali Mohamed Shein (katikati) akifuatana na Mkuu wa Mkoa Kaskazini Unguja,(wa pili mkushoto) pamoja na Viongozi wengine wakielekea katika kaburi wakati wa mazishi ya  Marehemu Mzee Prof.Ishau Abdalla Khamis yaliyofanyika jana kijiji cha Donge,Wilaya ya Kaskazini BUnguja ,[Picha na Ikulu.
 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Ali Mohamed Shein (wa pili kushoto waliosimama) alijumuika na Waislamu,Viongozi mbali mbali na Wananchi katika mazishi ya Marehemu Mzee Prof.Ishau Abdalla Khamis katika kijiji cha Donge leo,[Picha na Ikulu.]




Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Ali Mohamed Shein  akitia udongo katika kaburi la Marehemu Mzee Prof.Ishau Abdalla Khamis aliyezikwa jana katika kijiji cha  Donge,Willaya ya Kaskazini B Unguja,[Picha na Ikulu.]


NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.

RAIS wa Zanzibar  na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein leo ameungana na mamia ya wananchi katika mazishi ya aliyewahi kuwa Mjumbe  wa Halmashauri Kuu na Afisa Mwandamizi (Mstaafu) wa Idara ya Organaizesheni CCM Zanzibar , Prof. Ishau  Abdullah Khamis huko kijijini kwao  Donge  Wilaya ya Kaskazini "B" Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Marehemu Prof. Ishau amefariki  jana (juzi) katika Hospitali ya Taifa Muhimbili alipokuwa akipatiwa matibabu baada ya kuuguwa kwa muda mrefu maradhi ya figo.

Katika mazishi hayo Dkt. Shein ameambatana na viongozi mbali mbali wa chama na serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar   wakiwemo Makamo wa  pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dkt. Abdulla  Juma  Saadalla “Mabodi”
,Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Vuai Mwinyi Mohamed, Naibu Kadhi Mkuu wa Zanzibar Sheikh Hassan Othman Ngwali, Katibu wa Mufti Sheikh Fadhil Suleiman Soraga.

Prof.Ishau amepata elimu yake ya  msingi  katika  Shule ya msingi Donge  na kusoma elimu ya Chuo Kikuu Makerere Uganda na baadae kwenda nchini Hungry alikopata kiwango cha elimu ya Uprofesa na kurudi nchini kwa ajili ya kufanya kazi za umma.

Aidha  Marehemu Prof. Ishau enzi za  uhai wake aliwahi kushika nyadhifa mbali mbali katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ikiwemo Mkuu wa Wilaya, Mkuu wa Mkoa, Ubunge,  Mwalimu katika Chuo cha Uchumi (Dar), Waziri wa Mawasiliano na Uchukuzi na  Waziri wa Utalii na Misitu.

Pia  Prof.Ishau hadi kufariki kwake alikuwa ni Mwenyekiti wa Bodi ya Ofisi ya Takwimu Zanzibar  nafasi  ambayo ameteuliwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein.

Kwa upande wa Chama marehemu aliwahi kuwa Mjumbe wa Halmashauri Kuu, Katibu wa Fedha, uendeshaji na Miradi ya Chama, Mkuu wa Kitengo cha Uchaguzi katika Idara ya Organaizesheni - Afisi Kuu ya CCM Zanzibar, cheo alichoshikilia hadi mwaka 2014, alipostaafu Utumishi wa Chama.

Chama Cha Mapinduzi kinaungana na wanafamilia, ndugu na marafiki wa marehemu Tunamuomba Mwenyezi Mungu muumba Mbingu na Ardhi na Vyote viliomo ndani aiweke roho ya marehemu mahali pema Peponi amin.


Marehemu mpaka  kufariki kwake ameacha  watoto Sita. 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.