Habari za Punde

Waziri wa Elimu Mhe. Ndalichako Atembelea Shule ya Sekondari ya Magufuli, Aridhishwa na Utekelezaji wa Miradi ya Lipa Kwa Matokeo (P4R).

Waziri wa Elimu Profesa Joyce Ndalichako Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia akiwa na viongozi wa Mkoa wa Geita wakati wa kukagua vyumba vya madarasa mwenye miwani kulia ni Mhandisi Robert Gabriel Mkuu wa Mkoa Geita. 

Profesa Joyce Ndalichako Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia akikagua ujenzi wa vyumba vya madarasa shule ya sekondari Magufuli, wakwanza kulia ni Mkuu wa shule hiyo na wapili kulia ni Shaban Ntarambe Mkuu wa Wilaya Chato.
Mheshimiwa Shaban Ntarambe Mkuu wa Wilaya ya Chato akizungumza na wananchi (awapo kwenye picha) wakati wa ziara ya Waziri wa Elimu Wilayani Chato. 
Mhandisi Robert Gabriel Luhumbi Mkuu wa Mkoa wa Geita akizungumza jambo wakati wa ziara ya Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Magufuli Sekondari.
Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akizungumza na wananchi wa kijiji cha Bwanga wakati wa Ziara yake Magufuli Sekondari.
Bwana Exvery Nkanga kaimu Afisa Elimu Mkoa wa Geita akisoma taarifa ya maendeleo ya elimu Mkoa wa Geita kwa Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia.


Na: Magesa Jumapili
Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Pro.Joyce Ndalichako amefanya ziara fupi Wilayani Chato kwa kuitembelea Shule ya Sekondari Magufuli na kukagua utekelezaji wa miradi ya lipa kulingana na matokeo(P4R) shuleni hapo.

Akizungumza baada ya kufanya ukaguzi wa miradi ya ujenzi wa mabweni, Bwalo, vyoo na vyumba vya madarasa Profesa Joyce Ndalichako ameupongeza Uongozi wa Mkoa, Halmashauri ya Chato na Shule ya Sekondari Magufuli kwa kusimamia vizuri fedha za utekelezaji wa miradi hiyo kwa ubora na kiwango kinachotakiwa.

''Nafurahi kuona fedha za P4R zinatumika kwa matumizi yaliyokusudiwa kama tulivyokagua na kujionea kiwango kilichojengwa ndio haswa kinachotakiwa ambacho darasa lazima liwe na silling bodi, umeme lakini pia liwe na madirisha tofauti na madarasa tuliyokuwa tunajenga zamani hivyo nawapongeza kwa dhati kabisa viongozi mmefanya kazi kubwa thamani ya fedha inaonekana''.

Profesa Ndalichako amesema Serikali ya awamu ya tano inajukumu kubwa la kuhakikisha kunakuwa na mazingira bora katika utoaji wa elimu hivyo miradi ya namna hii inatekelezwa katika Halmashauri nchi nzima.

Amesema mwezi desemba 2017 serikali imetoa kwa halmashauri zote shilingi bilioni 15 na milioni 900 za kuendeleza jitihda za kuimarisha miundombinu ya sekta ya elimu ili kuongeza na kuimarisha majengo kwa ajili ya kupokea wanafunzi wa darasa la kwanza ambapo zitajenga jumla ya madarasa 415, mabweni 46, matundu ya vyoo 814 na mabwalo 7.

Aidha, Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhandisi Robert Gabriel Luhumbi amempongeza Waziri wa elimu kwa kutembelea shule hiyo ili kujionea kazi nzuri iliyofanyika  licha ya kuwa na majukumu mengi ya kitaifa.

Amewashukuru wananchi wa Mkoa wa Geita kwa jitihada zao za kushiriki katika ujenzi wa nyumba vya madarasa 8000  kwa shule za msingi na Sekondari ambapo tangu mkoa uzindue kampeni ya ujenzi huo zaidi ya vyumba 900 vya shule za msingi na zaidi ya 130 vya Sekondari vipo katika hatua tofauti.

Amesisitiza kuendelea kuunga mkono jitihada zao kwa kuhakikisha kunakuwa na uwazi katika michango inayotolewa na wananchi.

Mhandisi Robert Gabriel amemhakikishia Waziri wa Elimu kuwa pamoja na kuwa na idadi kubwa ya wanafunzi walioandikishwa kujiunda na elimu ya awali, darasa la kwanza na Sekondari hakutakuwa na mwanafunzi atakaye kaa nje ya darasa kwa kuwa jitihada za zinafanyika kwa haraka ili kukabiliana na hali hiyo.

Akiwa katika shule hiyo Mheshimiwa Waziri wa elimu alikagua ujenzi wa vyumba 8 vya madarasa, matundu 20 ya vyoo, mabweni 2 ya kulala wanafunzi na bwalo  miradi yote hii imetekelezwa na Serikali kupitia mpango wa lipa kulingana na matokeo kwa gharama ya shilingi 570,500,000/=.

Na: Magesa Jumapili
Afisa Habari
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Geita


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.