Habari za Punde

Wanafunzi saba wafanya mtihani na kufaulu kupandishwa madaraja ya mkanda mweusi wa Goju Ryu karate

 Na Sultani Kipingo wa Globu ya Jamii
Wanafunzi waandamizi saba wa  shule za Karate (dojo) mtindo wa Okinawa Goju Ryu  za  Kaizen na Hekalu la Kujilinda  za jijini Dar es salaam na Dodoma wamefanya mitihani na kufaulu kupandishwa madaraja ya mkanda mweusi chini ya Sensei Rumadha Fundi  (BOFYA HAPA KUMJUA) usiku wa Jumatatu Januari 22, 2018.
Wanafunzi hao kutoka Kaizen dojo  iliyopo Shule ya Sekondari ya Jamhuri na dojo dada ya Hekalu la Kujilinda iliyopo katika shule ya msingi ya Zanaki ni pamoja na ma-Senpai Yusuf Kimvuli, Abdulwahud Aghfoul, Bilali Mtenga na Seif Soud ambao wamepanda kutoka mkanda mweusi daraja la kwanza (1st Dan)  kwenda la daraja la pili (2nd Dan) lijulikanalo kama "Nidan".
Wakati ma-Senpai Kimvuli, Maghfoul na Mtenga wanatoka dojo la Kaizen, Senpai Seif Soud anatoka Hekalu la Kujilinda.
Wanafunzi wengine watatu waliofaulu na kupanda daraja la kwanza (1st Dan) ama "Shodan" kutoka mkanda wa kahawia ni ma-Senpai Abdulmajid Khan wa Hekalu la Kujilinda pamoja na  Shaaban Yusuf na Galant Swai ambao wanatoka katika tawi la Hekalu la Kujilinda lililopo mjini Dodoma kwa jina la Miyagi dojo.
Hii ni mara ya kwanza kwa  Sensei Rumadha Fundi  mwenye Dan 4,“Yondan” na  mwenye uzoefu mkubwa wa  mafunzo ya Goju Ryu chini ya walimu wakuu wengi maarufu toka Okinawa, Japan, kuwafanyia mitihani na kuwapandisha madaraja wanafunzi wa Tanzania.
Sensei Rumadha, ambaye alianza mafunzo ya Okinawa Goju Ryu miaka 38 iliyopita  katika Hekalu la Kujilinda la Zanaki amesema anajisikia furaha na fahari kutimiza hilo jukumu lake kwa mara ya kwanza, na kwamba hajutii kufunga safari hii kutoka Houston, Marekani, anakoishi na kuja kuwasaidia ndugu zake.
Na hilo liliwezakana baada ya mwaka jana huko  nchini Poland  Sensei Rumadha kufanya  na kufaulu vizuri mitihani wake wa kupanda ngazi toka Dan ya tatu "Sandan" kwenda ngazi ya nne "Yondan"  chini ya waamuzi (masters) toka Okinawa wakiongozwa na Sensei Yoshihiro Kancho Miyazato, ambaye ni Master au mwalimu mkuu wa Okinawa Goju Ryu Jundokan So Honbu Karate-Do huko Okinawa.
Tokea hapo Sensei  Rumadha amekuwa na mamlaka ya kuwasaidia wanafunzi wake wa Tanzania na kuwafanyia mitihani na kuwapa wanafunzi  "Dan" hadi ngazi ya pili " Nidan" sababu katika Goju Ryu Karate  kuanzia Dan ya 3 na kuendelea hutolewa na Master Miyazato pekee.
"Hawa waliofaulu na kupanda daraja la pili hivi sasa wana mamlaka ya kufungua shule zao chini ya uangalizi wangu na wakiendelea kufanya vyema nitatoa idhini ya wao kuwa waalimu ("Sensei") wanaotambulika Okinawa  baada ya muda si mrefu ujao" amesema Sensei Rumadha.
Hakusita kutoa shukran zake nyingi kwa mlezi wake wa mafunzo tokea utotoni,  "Sensei Magoma Nyamuko Sarya akisema chini ya uongozi wake kitengo cha watoto kilichoitwa "Bomani Brigade"  kilichobuniwa  na mwanzilishi wa Okinawa Goju Ryu nchini Tanzania mwaka 1973,  hayati Sensei Nantambu Camara Bomani. 
Alitoa shukurani za pekee kwa viongozi wa sasa wa Hekalu la Kujilinda - Sensei Mohamed Murudker, Sensei Wilfred Melkia, Sensei Geofrey Sawayael “Shoo” na Sensei Rashid Almasi ambao amesema moyo wao wa  kuendeleza Goju Ryu bila kutetereka pale Zanaki ni wa kusifika, na kwamba anawapongeza sana.
Sensei Rumadha pia ameeleza kuwa kabahatika mwaka huu kualikwa kuiwakilisha Tanzania ambayo pamoja na na Angola ni nchi pekee za Afrika zilizoalikwa kuhudhuria maadhimisho ya miaka 65 tangu kuanzishwa kwa chama cha "Jundokan" na Master Eiichi Miyazato Sensei huko Naha City, Okinawa, mwezi wa Novemba 1918. 
Chama hicho kwa sasa kinaongozwa na mwanawe Yoshihiro Kancho Miyazato, ambaye pia ni Mwenyekiti mkuu dunia wa chama hicho na mwanae Master Eiichi Miyazato, ambaye amewafanyia mitihani ya mkanda mweusi zaidi ya walimu 15 toka ngazi ya pili" Nidan" hadi ngazi ya saba "Nandan". 
Kwa mujibu wa Sensei Rumadha, ngazi hizo zote kwa utamaduni wa mtindo wa Okinawa Goju Ryu Karate huchukua miaka mingi sana kupandishwa ngazi  tofauti na mitindo mingine. 
 Sensei Rumadha Fundi akiwafanyisha mazoezi wanafunzi saba hao kabla ya kuanza kufanya mtihani wao wa kupanda daraja katika Dojo la Hekalu la Kujilinda lililomo katika ukumbi wa Shule ya Msingi ya Zanaki jijini Dar es salaam Jumatatu usiku Januari 22, 2018
Viongozi wakuu wa  Dojo la Hekalu la Kujilinda lililomo katika ukumbi wa Shule ya Msingi ya Zanaki jijini Dar es salaam  wakishuhudia  wanafunzi saba wakifanya mazoezi kabla ya mtihani Jumatatu usiku Januari 22, 2018. Kutoka kulia ni Sensei Wilfred Malekia, Sensei Mohamed Murudker na Sensei Rashid Almasi
  Sensei Rumadha Fundi akiendelea kuwafanyisha  mazoezi wanafunzi saba hao kabla ya kuanza kufanya mtihani wao wa kupanda daraja katika Dojo la Hekalu la Kujilinda lililomo katika ukumbi wa Shule ya Msingi ya Zanaki jijini Dar es salaam Jumatatu usiku Januari 22, 2018
Sensei Rumadha Fundi akiendelea kuwafanyisha  mazoezi kwa vitendowanafunzi saba hao kabla ya kuanza kufanya mtihani wao wa kupanda daraja katika Dojo la Hekalu la Kujilinda lililomo katika ukumbi wa Shule ya Msingi ya Zanaki jijini Dar es salaam Jumatatu usiku Januari 22, 2018
 Sensei Rumadha Fundi akitoa mwongozo akiwa na uongozi wa dojo kabla ya  mtihani  wa kupanda daraja wa wanafunzi saba  katika Dojo la Hekalu la Kujilinda lililomo katika ukumbi wa Shule ya Msingi ya Zanaki jijini Dar es salaam Jumatatu usiku Januari 22, 2018
 Kutoka kushoto Ma-Senpai Abdulmajid Khan wa Hekalu la Kujilinda pamoja na  Shaaban Yusuf na Galant Swai ambao wanatoka katika tawi la Hekalu la Kujilinda lililopo mjini Dodoma kwa jina la Miyagi dojo wakifuatiwa na ma-Senpai Yusuf Kimvuli wa Kaizen dojo na Senpai Seif Soud wa Hekalu la Kujilinda.
Wanafunzi watatu waliofaulu na kupanda daraja la kwanza (1st Dan) ama "Shodan" kutoka mkanda wa kahawia ni  kutoka kushoto ma-Senpai Abdulmajid Khan wa Hekalu la Kujilinda pamoja na  Shaaban Yusuf na Galant Swai ambao wanatoka katika tawi la Hekalu la Kujilinda lililopo mjini Dodoma kwa jina la Miyagi dojo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.