Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Alhajj Ali Mohamed Shein, Ametowa Wito Kwa Wafanyabiashara Zanzibar Watumie Vema Azma ya Serikali ya Kuwapunguzia Ushuru wa Bidhaa.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Ali Mohamed Shein akitoa risala ya kuukaribisha Mwezi mtukufu wa Ramadhan kwa Wananchi wa zanzibar na tanzania kwa ujumla katika ukumbi wa Ikulu Mjini Zanzibar leo,pia amewataka waumini wa Dini ya Kiislamu na Wananchi kuwa na mashirikiano ya pamoja na kumcha Mwenyeezi Mungu

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Ali Mohamed Shein ametoa wito kwa wafanyabiashara wa jumla na reja reja waitumie vyema azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kuwapunguzia ushuru wa bidhaa za chakula katika mwezi wa Ramadhani, ili wananchi wapate bidhaa hizo kwa bei nafuu.

Alhaj Dk. Shein aliyasema hayo katika risala maalum aliyoitoa kwa wananchi kupitia vyombo vya habari katika kuukaribisha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani mwaka huu wa 1439 Hijria sawa na mwaka 2018 Miladia.

Katika risala yake hiyo, Alhaj Dk. Shein aliendelea kuwakumbusha wafanyabiashara kujitahidi kadri wawezavyo ili wasipandishe bei za bidhaa bila ya sababu za msingi au kuwauzia wananchi bidhaa zilizopita muda wake wa matumizi.

Alieleza kuwa wafanyabiashara wanapaswa kujitahidi kuwa waadilifu, waaminifu na kutenda haki katika kufanya biashara zao pamoja na kuhakikisha kuwa vipimo vyao vya kuuzia bidhaa ni vya halali kwani ni kinyume na sheria watu kudhulumiana katika vipimo.

Kutokana na hali hiyo, Alhaj Dk. Shein aliziagiza Taasisi zinazohusika kulisimamia  vyema jambo hilo na wasichelee kuwachukulia hatua za kisheria wale wote watakaobanika, kufanya biashara kinyume na sheria, kanuni na taratibu za nchi.

Aidha, Alhaj Dk. Shein aliwahimiza wananchi kujiandaa na Ramadhani kwa kufanya zaidi mambo mema na ibada za Saumu, Sala na utoaji Sadaka katika mwezi huo wote sambamba na kuzidisha kusoma Qur-an na kuielewa pamoja na Hadith za Bwana Mtume Muhammad (S.A.W), ili waweze kuzitekeleza ibada zao vizuri.

Pia, Alhaj Dk. Shein alisisitiza kuwa katika mwezi wa Ramadhani himizo linatolewa katika kuzidi kutendeana wema na ihsani na kusisitiza kuwa utoaji wa sadaka ni jambo la msingi ili wenye kipato kidogo nao wawe wenye furaha katika mwezi huo.
Alisisitiza haja ya kufanya mambo yatakayoleta faida, yatakayolinda maadili na kutoa mafunzo mema kwa watoto huku Alhaj Dk. Shein akihimiza ucha Mungu ili mwezi wa Ramadhani uache neema katika jamii pamoja na kuhudhuria kwa wingi katika darsa.

Pamoja na hayo, Alhaj Dk. Shein alieleza kuwa Ramadhani mwaka huu imekuja ikiwa bado msimu wa mvua za Masika unaendelea hivyo, aliwaomba wananchi kwa umoja wao washirikiane katika kuiweka miji yao katika usafi ili wajiepushe na janga la maradhi ya kipindupindu pamoja na maradhi mengine ya miripuko.

“Tutakapojitahidi kuchukua tahadhari ya kuweka mazingira yetu safi na kufuata taratibu zote za kinga, hapana shaka tutayaepuka mardhi mengi yanayotokana na uchafu, naamini kwamba Allah naye atatusaidia”,alisisitiza Alhaj Dk. Shein.

Aidha, Alhaj Dk. Shein aliwanasihi wananchi wasiowajibika na Saumu kama kawaida yao washirikiane na wenzao wanaofunga na waendelee kuwa wastahamilivu na kuitumia fursa hiyo vyema bila ya kufanya vitendo vya karaha ya kuwaudhi wengine.

Hivyo, Alhaj Dk. Shein alitoa wito kwa wananchi wanaomiliki mikahawa na nyumba za starehe wajitahidi kuzingatia sheria,taratibu na utamaduni uliopo ili kuzuia kero na maudhi kwa wananchi wenzao wenye kutekeleza ibada ya funga.

Pia Alhaj Dk. Shen, aliwataka madereva na watumiaji wa barabara kuzingatia sheria za usalama barabarani hasa wakati wa jioni ambapo watu wengi huwa wanakimbilia kufutari, huku akiahidi kuwa Jeshi la Polisi litaendelea kuimarisha ulinzi wa watu na mali zao kwa kushirikiana na vijana wa ulinzi shirikishi ili wananchi wapate utulivu na kutekeleza saumu kwa amani.

Kama kawaida yake Alhaj Dk. Shein aliwakumbusha viongozi wa Wizara ya Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati pamoja na uongozi wa Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) wachukue hatua ya kuwapelekea maji wananchi kwa magari kwenye maeneo yao wanayoishi ambayo huduma hizo zimepungua.

Pamoja na hayo, Alhaj Dk. Shein alitumia fursa hiyo kueleza jinsi uchumi wa Zanzibar ulivyoimarika sambamba na utoaji wa huduma na ustawi wa wananchi huku akiwapongeza wakulima wa karafuu kwa mafanikio makubwa yaliopatikana ambapo msimu uliopita jumla ya tani za karafuu 8,539.39 zenye thamani ya TZS bilioni 119.14 zimenunuliwa na Shirika la Biashara la Taifa la Zanzibar (ZSTC) hadi Mei 15 mwaka huu.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.