Habari za Punde

JUISI ZA AZAM YAJA KIVINGINE 'AFRICAN FRUTI'

Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage akiwa na Afisa Mtendaji Mkuu wa kampuni ya Bakhresa Foods and Beverages Ltd wakionyesha juisi ya African Fruti iliyokuwa ikijulikana kama Azam juisi kwenye hafla ya uzinduzi wa juisi hiyo uliofanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage akionja utamu wa juisi ya African Fruti baada ya kuzindua rasmi juisi hiyo.
Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage akizungumza kwenye hafla ya uzinduzi wa juisi ya African Fruti.
Mkuu wa Uhusiano na Masuala ya ndani wa kampuni ya Bakhresa Group, Hussein Sufian akizungumza machache kwenye hafla ya uzinduzi wa juisi ya African Fruti.
Baadhi ya wageni waalikwa kwenye hafla ya uzinduzi wa juisi ya African Fruti.
Baadhi ya wafanyakazi na wageni waalikwa wakifurahia juisi ya African Fruti. Kampuni ya Bakhresa Food Products Ltd imetangaza kubadili chapa za bidhaa zake za juisi za Azam zinazotamba kwenye soko nchini, kuanzia sasa zitajulikana kama ‘African Fruti’.

 Mabadiliko haya yanaenda sambamba na kubadilika kwa muonekano wa nje wa bidhaa hizo, isipokuwa ladha na ubora wa bidhaa hizo utabaki palepale hivyo wateja wataendelea kufurahia juisi zenye viwango vya kimataifa zinazozalishwa na kampuni ya Bakhera Food Products Ltd, kampuni tanzu ya Bakhresa Group. 

Akizungumza kwenye hafla ya uzinduzi wa juisi za African Fruti, Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Mhe Charles Mwijage aliipongeza kampuni ya Bakhresa kwa kutengeneza bidhaa bora na kufikia lengo la kusafirisha bidhaa hiyo nje ya nchi.

“Kwa niaba ya serikali, napenda kuipongeza kampuni ya Bakhresa Group kwa uwekezaji na ubunifu mkubwa ambao imekuwa ikiufanya katika jitihada za kukuza sekta ya viwanda nchini kwa kuzalisha bidhaa za aina mbalimbali zenye viwango na serikali itaendelea kuunga mkono jitihada zenu,” alisema Mwijage.

Kwa upande wake Afisa Mtendaji Mkuu wa kampuni ya Bakhresa Foods, Salim Aziz alisema, “baada ya bidhaa za juisi kufanikiwa kwenye soko kutokana na ubora wake, kampuni ikaamua kuja na mkakati utakaofanya juisi hizi zitambulike kirahisi kama bidhaa halisi za Tanzania hivyo kuzipa jina la “African Fruti”

 Aliongeza “Licha ya kulenga masoko ya nchi za Afrika ambako tayari tumeanza kuuza juisi zetu, hivi sasa tuko kwenye mchakato wa kusambaza bidhaa hizi katika nchi za China na Nchi za Kiarabu,” alisema Bakhresa.

Kwa upande wake Mkuu wa Uhusiano na Masuala ya ndani wa kampuni ya Bakhresa Group, Hussein Sufian alisema walifikia hatua ya kubadilisha muonekano wa juisi ili kuzipa hadhi ya kimataifa, ikiwa ni namna ya kuwashukuru wateja wake ambao wengi wao ni watanzania wa kawaida kwa kuendelea kuwa mstari wa mbele kuzinunua.

“Tumetaka tuwape wateja wetu fursa ya kutumia bidhaa halisi za kitanzania zenye muonekano na hadhi ya kimataifa, vivyo hivyo, hii inadhihirisha kuwa Bakhresa imefanikiwa kujiendeleza katika sekta ya viwanda hapa nchini na ndio maana tuko kwenye mkakati wa kuuza juisi zetu nje ya Tanzania na tunaamini zinaweza kushindana kwenye soko la kimataifa,” alisema Sufian.

Aliongeza kuwa kuptia mkakati huu wa kusafirisha juisi za ‘African Fruti’ nchi za nje, wakulima wengi zaidi wa matunda nchini wataendelea kunufaika.

“Tunawashukuru wateja wetu ambao siku zote wamekuwa wakituunga mkono nasi tunawahakikishia kuwa tutaendelea kuwaletea bidhaa bora zaidi zikiwa kwenye ujazo tofauti tofauti ili kukidhi mahitaji yao,” aliongeza.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.