Habari za Punde

Indonesia Imeahidi Kuimarisha Zaio la Mwani Zanzibar ni Miongoni ya Mwa Zao la Biashara Visiwani Vya Zanzibar.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akizungumza na Mkurugenzi Mkuu wa kampuni ya Mwani Hendrico Soewardjono alipowasili katika kiwanda cha kampuni hiyo leo na Ujumbe wake akimalizia ziara yake ya mualiko wa Makamo wa Rais wa Indonesia Dkt.Mohamed Jusuf Kalla,[Picha na Ikulu.] 


INDONESIA imeahidi kushirikiana na Zanzibar katika kuliimarisha zao la mwani ambalo limekuwa ni miongoni mwa zao la biashara katika visiwa vya Zanzibar.

Uongozi wa Kampuni ya mwani ya ‘AGAR Swallow’ ya nchini Indonesia umeeleza hayo ulipofanya mazunguzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein katika ofisi za Kampuni hiyo zilizopo mjini Jakarta wakati alipokitembelea kiwanda hicho.

Akitoa maelezo katika mazungumzo hayo, Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni hiyo Hendrico Soewardjono alimueleza Rais Dk. Shein azma ya Kampuni hiyo ya  kushirikiana na Zanzibar katika kuliendeleza zao la mwani.

Alieleza kuwa Kampuni hiyo tayari imepata mafanikio makubwa ambapo aina ya bidhaa yake ya unga wa mwani ambayo hutengenezewa bidhaa mbali mbali za vyakula na dawa imekuwa na soko kubwa na bidhaa zake huzisafirisha nchi mbali mbali duniani.

Aliongeza kuwa kutokana na Zanzibar kuliendeleza zao hilo la mwani na kulimwa kwa wingi Kampuni yake iko tayari kutoa ushirikiano unaohitajika ikiwa ni pamoja na kutoa mafunzo juu ya uendelezaji wa  zao hilo pamoja na utafutaji wa masoko.

Mkurugenzi Mkuu huyo alimueleza Dk. Shein kuwa aina ya unga anaotokana na mwani wa aina ya grasilarias unaotengenezwa kiwandani hapo umekuwa ukitumika sana kwa kutengenezea bidhaa mbalimbali ambazo zimekuwa maarufu duniani.

Alieleza jinsi wanavyolisarifu zao la mwani huku akieleza kuwa miongoni mwa bidhaa zinazotengenezewa unga huo ni pamoja na kutengenezea baadhi ya vyakula, vipodozi, dawa zikiwemo dawa za mswaki pamoja na kutengeneze bidhaa nyengine mbali mbali.

Aidha, kiongozi huyo wa Kampuni ya AGAR alieleza namna Serikali ya Indonesia kupitia Kampuni hiyo inavyoliendeleza na kulisimamia zao la mwani pamoja na kushirikiana na kampuni ndogo ndogo zinazofanya biashara ya zao hilo.

Nae Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein aliipongeza azma ya Kampuni hiyo ya kushirikiana na Zanzibar katika kuliimarisha na kuliendeleza zao la mwani.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa hatua hiyo itaendelea kuimarisha uhusiano na ushirikiano uliopo ambao ni wa kihistoria kati ya Indonesia na Zanzibar.

Alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iko tayari kushirikiana na Indonesia katika kuhakikisha zao hilo linaimarika kwani Zanzibar ni miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa zao hilo duniani.

Dk. Shein pia, aliueleza uongozi huo kuwa ziara yake ya kukitembelea kiwanda hicho ni azma moja wapo ya kujifunza sambamba na kuangalia utaalamu uanaofanyika kutoka kwa kampuni hiyo kwa lengo la kupanua wigo.

Nao viongozi aliofuatana nao Rais Dk. Shein katika ujumbe wake wakichangia katika mazungumzo hayo walieleza kuwa ni biashara ya zao la mwani kwa upande wa Zanzibar inahitaji mashirikiano ya kutosha kwani tayari wananchi wameshajenga matumaini makubwa kwa zao lao hilo.

Walieleza kuwa miongozi mwa changamoto kubwa iliyopo katika uimarishaji na uendelezaji wa zao hilo ni pamoja kutokuwepo kwa soko la uhakika la mwani visiwani Zanzibar.

Pia, viongozi hao waliongeza kuwa kutokana na Kampuni hiyo kupata mafanikio makubwa itakuwa ni jambo la busara katika kushirikiana kuliimarisha zao hilo pamoja na kuonesha uzoefu na mafanikio waliyoyapata kwa wakulima wa mwani wa Zanzibar

Wakati huo huo, baadhi ya viongozi na watendaji wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar walitembelea na kufanya mazungumzo yenye lengo la kujifunza katika kiwanda maarufu nchini Indonesia na duniani kwa ujumla cha INDESSO kilichopo nje kidogo ya mji wa Bali.

Katika maelezo yao viongozi wao wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar walieleza kufurahishwa kwao na mapokezi mazuri yaliyoyanywa na Kampuni hiyo sambamba na azma ya ushirikiano walio ahidi kuutoa kwa Zanzibar.

Katika maelezo yake, Mkurugenzi Uzalishaji wa Kampuni hiyo Dk. Efendi Aroma alieleza kuwa Kampuni ya mafuta ambayo imeanzishwa 1968 imeweza kuimarika sana kutokana na mikakati maalum iliyojiwekea katika uzalishaji ambayo kampuni kubwa inayozalisha mafuta ya mimea yakiwemo ya karafuu.

Kampuni hiyo hutoa mafuta ya mimea mbali mbali ambayo hutumika kwa manukato katika utenegezaji wa bidhaa  za manukato, mafuta ya mimea na aina mbali mbali za unga unaotumika katika utengenezaji na upishi wa vyakula.

Kampuni hiyo imepata mafanukio makubwa kutokana na soko la uhakika kutoka kwa nchi za Marekani, Ulaya na Asia kutokana na bidhaa za mafuta wanazozizalisha yakiwemo mafuta ya karafuu kuwa na soko kubwa.

Sambamba na hayo, viongozi wa Kampuni hiyo ya INDESSO walieleza kufarajika kwao kwa kutembelewa pamoja na kukaa pamoja na kubadilishana mawazo kati yao na viongozi na watendaji wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar jambo ambalo walieleza kuwa limewapa faraja na matumaini makubwa ya mashirikiano.

Pamoja na hayo, viongozi hao wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar walitumia fursa  hiyo kwa kutembelea sehemu mbali mbali za kiwanda hicho ambacho kina mitambo ya kisasa.
Dk. Shein anatarajiwa kurejea nchini hapo kesho Jumatatu ya tarehe 6 Agosti, 2018 baada ya kumaliza ziara yake nchini Indonesia  ambapo katika ziara hiyo alifuatana na viongozi mbali mbali akiwemo Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwema Shein pamoja na Mawaziri na watendaji wengine wa Serikali.
Ziara hiyo ya Dk. Shein aliifanya kufuatia mwaliko wa Makamo wa Rais wa Indonesia Muhammad Jusuf Kalla ambapo mbali ya kutembelea na kufanya mazungumzo na viongozi mbali mbali wa Indonesia katika mji wa Jakarta pia, alitembeleaa kisiwa cha utalii cha Bali na kufanya mazungumzo na viongozi wa kisiwa hicho pamoja na kutembelea maeneo mbali mbali ya maendeleo ya kitalii, kihistoria, utamaduni na sanaa.

 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.