Habari za Punde

TRC yafufua Reli iliyokufa kwa Miaka Kumi.


Na. Immaculate Makilika – Maelezo.
Shirika la Reli tanzania (TRC) limefanikiwa kufufua reli inayounganisha Tanzania na Mji wa Kampala nchini Uganda,ambayo ilikufa kwa kipindi cha miaka kumi, ambayo imekuza kiwango cha biashara kati ya nchi hizi mbili kufikia asilimia 5.5 kutoka asilimia 1 ya awali.

Mafanikio haya ambayo ni moja ya mabadiliko yaliyotokea katika kipindi cha miaka mitatu ya serikali ya Awamu ya tano, ni muendelezo wa jitihada za serikalikatika kufufua mashirika ya Umma ambayo yalikuwa taabani.

Akizungumza Jijini Dar es Salaam leo, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Reli nchini (TRC)  Masanja Kadogosa amesema kuwa katika kipindi cha miaka miatatu, Shirika hilo 
limefanya maboresho kadhaa yaliyoongeza ufanisi wa utendaji kazi katika uendeshaji wa reli nchini.

“Njia ya reli kwenda Kampala tuliyoifufua  hivi karibuni baada ya kutotumika kwa miaka 10, imesadia kukuza biashara ya  kusafirisha mizigo  kutoka asilimia 1.5 hadi 5.5, na pia imeweza kupunguza muda wa safari kutoka siku siku nane hadi kufikia siku nne” Alisema.

Aliongeza kuwa maboresho hayo yaliyofanyika katika kipindi cha miaka mitatu  yamesaidia kuongezeka kwa kiwango cha mizigo kinachosafirishwa kutoka tani 150 hadi 180 na kufikia tani  100,002  katika kipindi cha robo ya kwanza ya mwaka, ambayo ni sawa na asilimia 60.

Kadogosa alitaja maboresho mengine yaliyofanyika  kuwa ni kufungua stesheni mbalimbali kama ya Tanga, pamoja na kuongeza njia za kupishana treni, pia kutandika upya  njia ya 
treni kutoka Dar es Salaam hadi Pugu yenye urefu wa km 20, sambamba na kuboresha njia ya Ubungo  ambayo imeongeza makusanyo kutoka shilingi milioni 1hadi  shilingi milioni 6.5.

Aidha, Mkurugenzi huyo wa TRC, alibainisha kuwa  Shirika lake lina  mradi wa kuboresha reli ya kati  yenye urefu wa km 2600, ambapo alisema ni njia muhimu inayoounganisha 
nchi kwa sasa, pamoja na kutumika kusafirishia vifaa vya ujenzi wa reli mpya ya kisasa yaani Standard Gauge.

Kuhusu ujenzi unaoendelea wa reli ya kisasa yaani Standard Gaude, Mkurugenzi Mtendaji huyo  wa TRC alisema kuwa, reli hiyo inayojengwa katika awamu mbili, kutoka Dar es salaam hadi Morogoro ikiwa ni awamu ya kwanza ina urefu wa kilometa 1219 na kutoka Morogoro hadi Makutupora yenye  urefu wa kilometa 722, imefikia wastani wa ujenzi wa 
asilimia 34 katika kipande cha Dar es salaam hadi Mororgoro.

Sambamba na hayo,  Mkurugenzi Kadogosa, alisema kuwa reli hiyo ya kisasa itakuwa na madaraja makubwa  26 na madogo 243 kati ya Dar es Salaam na Morogoro, na stesheni 
sita , kubwa mbili na ndogo nne.

Aidha, uendeshaji wa treni hiyo utategemea umeme kutoka Shirika la Umeme nchini TANESCO ambapo utaunganisha umeme kutoka kwenye gridi ya Taifa hadi kwenye stesheni za reli.

“Naomba niwatoe hofu kuwa tumechukua tahadhari zote kuhakikisha hakutakuwa na tatizo la umeme, kwa vile treni itatumia dizeli na umeme na hivyo tumehakikisha abiria wataweza kusafiri kwa saa 24, sambamba hilo kutakuwa na mawasiliano ya simu hata kwa kutumia mtandao yaani intaneti wakati wote wa safari”alisema.

Kadogosa Kuhusu malighafi zinazotumika pamoja na faida zinazopatikana wakati wa ujenzi wa reli hiyo, Kadogosa alisema kuwa tayari reli imetandikwa kwa kilometa 10, na malighafli zinazotumika mfano mataluma yanatengenezwa hapa nchini na viwanda hivyo vitaendelea kuwepo mara baada ya mradi kukamilika, na wafanyakazi wa mradi huo kwa asilimia 96 ni watanzania huku asilimia 4 tu ikiwa ni wageni.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.