Habari za Punde

DKT MWAKEMBYE AVITAKA VYOMBO VYA HABARI KUWEKA SERA MADHUBUTI KATIKA KUTETEA NA KUTANGAZA MAFANIKIO YA MAENDELEO YA AFRIKA

 Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe akipokewa na Rais wa Chama Cha Maafisa Uhusiano wa Sekta Binafsi Tanzania (PRST) Loth Makuza, mara baada ya kuwasili katika ukumbi wa Karimjee Jijini Dar es Salaam leo Ijumaa (Mei 24, 2019) kwa ajili ya kushiriki katika Kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Mawasiliano Barani Afrika. Kushoto ni Mratibu Mwenyekiti wa Bodi ya (PRST), Jossey Mwakasyuka.
 Mkurugenzi wa Idara ya Habari (MAELEZO) na Msemaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Hassan Abbasi akizungumza na wadau mbalimbali wa sekta ya habari na Mawasilino kutoka Taasisi za Umma na sekta binafsi wakati wa kilele cha maadhimisho ya ya Wiki ya Mawasiliano Barani Afrika iliyofanyika katika Ukumbi wa Karimjee Jijini Dar es Salaam 
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo,. Dkt. Harrison Mwakyembe akizungumza na wadau mbalimbali wa sekta ya habari na Mawasilino kutoka Taasisi za Umma na sekta binafsi wakati wa kilele cha maadhimisho ya ya Wiki ya Mawasiliano Barani Afrika iliyofanyika katika Ukumbi wa Karimjee Jijini Dar es Salaam 
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe akiwa katika picha ya pamoja na wadau mbalimbali wa sekta ya Habari na Mawasiliano pamoja na wadhamini wa Maadhimisho ya Wiki ya Wiki ya Mawasiliano Barani Afrika wakati wa kilele cha maadhimisho hayo yaliyofanyika Ijumaa 
  1. Waziri  Habari, UItamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe (kushoto) akibadilishana mawazo na Mstahiki Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Isaya Mwita (katikati) mara baada ya kufunga maadhimisho ya kilele cha Wiki ya Mawasiliano Afrika yaliyofanyika katika Ukumbi wa Karimjee Jijini Dar es Salaam leo Ijumaa (Mei 24, 2019). Kulia ni Mkurugenzi wa Idara ya Habari (MAELEZO) na Msemaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Hassan Abbasi.
(PICHA NA MAELEZO)Waziri 




Na Mwandishi Wetu,MAELEZO ,DAR ES SALAAM. 
WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe amevitaka vyombo ya habari vya Nchi za Bara la Afrika ikiwemo Tanzania kutangaza na kuandika habari za kweli ili kujitofautisha na vyombo vya Nje ya Bara hilo ambavyo upotosha na kubeza kwa makusudi mambo mazuri yanayotekelezwa na yaliyotekelezwa na Nchi za Afrika.
Akizungumza katika kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Mawasiliano Barani Afrika leo Ijumaa (Mei 24, 2019) Jijini Dar es Salaam, Dkt. Mwakyembe alisema vyombo vya Habari vya Afrika havina budi kuonyesha udhubuti kwa kuweka sera zinazoakisi maendeleo na kuyatangaza kwa Wananchi wake na wote waliopo nje ya Bara hilo.
Dkt. Mwakyembe alisema sehemu kubwa ya maudhui ya Vyombo vya Habari vilivyopo nje ya Bara la Afrika vinavyoongozwa na Wakoloni waliowahi kutawala katika Bara la Afrika hawapendi kuona Nchi za Afrika zinapiga hatua za Maendeleo kwa wananchi wake na badala yake hupenda kuripoti na kutangaza mambo mabaya yanayohusu Afrika ikiwemo njaa, magonjwa, vurugu za kisiasa, vita n.k.
Aidha Dkt. Mwakyembe alisema yapo mambo mazuri ya Maendeleo yanayofanyika katika Nchi za Bara la Afrika ikiwemo Tanzania ambayo zimepiga katika kipindi cha miaka minne imepiga hatua kubwa katika Maendeleo ya kiuchumi, na miundombinu, jambo ambalo baadhi ya vyombo vya habari vya Mataifa ya Nje ya Afrika yamekuwa hayapendi kuyatangaza, hivyo ni wajibu wa vyombo  vya habari kutumia majukwaa yao kutetea na kutangaza mafanikio hayo.
“Wakati Hayati Mwalimu Julius Nyerere na Kenneth Kaunda wa Zambia walipoamua kujenga Reli ya Tazara, walipingwa vikali sana Wakoloni waliotuwala na wengine waliita reli ile kuwa ni bamboo (mianzi) lakini ni taifa moja tu la Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China walitusaidia na leo hii reli ile ndiyo ndefu zaidi katika Bara la Afrika yenye urefu wa kilometa 1860” alisema Dkt. Mwakyembe.
Kwa mujibu wa Waziri Mwakyembe alisema Maendeleo ya Bara la Afrika yatatetewa na kupiganiwa na Wafrika wenyewe, hivyo ni wajibu wa vyombo vya habari vya Bara hilo kujitokeza na kutetea Maendeleo hayo na kamwe haitatokea siku moja chombo cha habari cha BBC au CNN vikatangaza mafanikio hayo kwani hawapendi kuona Mataifa waliyoyatawala yakifikia hatua kubwa za kimaendeleo.
Akifafanua zaidi Dkt. Mwakyembe aliwataka Vijana wa Nchi za Bara la Afrika ikiwemo Tanzania kujifunza historia ya Bara lao ili kuweza kufahamu wapi walipotoka na wapi wanapoelekea badala ya kupenda kulalamika pasipo na kuweka mikakati ya namna bora ya kupiga hatua za kujietea Maendeleo yao ya kijamii na kiuchumi.
Waziri Mwakyembe alisema ni wajibu wa Taasisi mbalimbali za Habari na Mawasiliano zilizopo katika Bara la Afrika kujenga mifumo imara ya mawasiliano ikiwemo kutumia vyema mitandao ya kijamii kwa ajili ya kuchapisha habari zinazohusu masuala ya maendeleo badala ya kutumia majukwaa hayo kuandika mambo yasiyo na faida wala tija kwa mataifa yao.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Idara ya Habari na Msemaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Hassan Abbasi, alisema Serikali imeendelea kuimarisha ushirikiano na taasisi za mawasiliano katika sekta binafsi ili kuhakikisha kuwa wanajenga daraja moja katika kusukuma mbele gurudumu la Maendeleo ya sekta ya habari na Mawasiliano nchini.
Naye Rais wa Chama cha Maafisa Uhusiano wa Sekta binafsi Tanzania (PRST) Loth Makuza alisema, taasisi hiyo ni jukwaa huru linalotoa fursa na nafasi ya kujadili masuala mbalimbali ya mawasiliano nchini ikiwemo changamoto na utatuzi wa masuala mbalimbali yanayohusu sekta ya habari na mawasiliano nchini.
Anaongeza kuwa Taasisi hiyo kwa kutumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano imeweza kutengeneza majukwaa mbalimbali yanayotangaza masuala mbalimbali ya kimaendeleo yaliyofikiwa katika Nchi za Bara la Afrika ikiwemo Tanzania, lengo likiwa ni kubadili mtazamo hasi wa Bara la Afrika katika nyanja za kiuchumi, kijamii kupitia ngazi ya kimataifa na duniani kwa ujumla.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.