Habari za Punde

Awataka Madereva wa Magari Kuwa Waangalifu na Kufuata Kanuni na Sheria za Usalama Barabarani.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein,akiwa katika mahojiano na Mtoto Nabir Mohammed na Ummukurthum kutoka (ZBC TV) wakiwa katika Ukumbi wa Ikulu Zanzibar wakati wa hafla ya kutoa Mkono wa Eid El Fitry kwa Watoto na Wananchi waliofika katika Viwanja vya Ikulu Zanzibar.  

MADEREVA wa gari nchini wametakiwa kutoendesha gari zao kwa mwendo wa kasi na badala yake waendeleze furaha ya Sikukuu ya Id El Fitri kwa salama na amani ili kuepuka kusababisha ajali zisizo za lazima hasa kwa watoto wadogo.

Dk. Shein aliyasema hayo  katika mahojiano ya kipindi maalum cha “Watoto na Mheshimiwa Rais” kinachotayarishwa na Televisheni ya Shirika la Utangazaji la Zanzibar (ZBC), mahojiano yaliofanyika Ikulu mjini Zanzibar.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein aliwataka madereva wa gari kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za barabarani hasa katika kipindi hichi cha Sikukuu na kuacha kuendesha gari kwa mwendo wa kasi ili kuepusha ajali kwa watu wanaopita barabarani wakiwemo watoto wadogo.

Aliongeza kuwa katika kipindi hichi cha Sikukuu kwa kawaida barabara huwa zinatumiwa na watu wengi wakiwemo watoto wadogo ambao wanahitaji uangalizi mkubwa wakati wakitembea barabarani hivyo, aliwanasihi madereva kuwa makini wanapoendesha gari zao. 

Rais Dk. Shein alisema kuwa Zanzibar hivi sasa gari zimekuwa nyingi hivyo, ni vyema watoto wakachua hadhari kwa kujikinga wenyewe sambamba na kuwa makini katika kutembea barabarani. “muwe waangalifu na muepushe kupisha gari kwa vipega ni hatari ” alisisitiza Alhaj Dk. Shein.

Aidha, Rais Dk. Shein aliwataka watoto kusikiliza nasaha za wazazi wao kwani wamewazaa na wanaendelea kuwalea hivyo ni vyema wakawa wasikivu hasa katika kipindi hichi cha Sikukuu pale wanapoambiwa kurudi mapema wafanye hivyo pamoja na kuvaa vizuri kama ilivyo desturi yao katika kipindi hichi cha Sikukuu.

Alhaj Dk. Shein aliwataka watoto kutambua kuwa hakuna watu wazuri tu katika mitaa yao bali pia, kuna na watu wabaya hivyo, ni vyema wakazingatia nasaha za wazazi wao pamoja na nasaha anazowapa yeye kwa upande wake huku akiwasisitiza kurudi nyumbani mapema ili kujiepusha na vitendo viovu katika kipindi hichi cha Sikukuu.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein pia, aliwataka wazazi kwa upande wao kuendelea kuwalea, kuwatunza  na kuwaamuru watoto wao maneno mazuri pamoja na watoto wa majirani zao kwani nao pia ni watoto wao huku akiwataka kuzidisha urafiki miongoni mwao kwani Uislamu unasisitiza hivyo.

Aliwanasihi watoto kuzingatia nasaha za wazazi na wazee wao na kuwataka wasivuke mipaka katika kufurahia sikukuu hiyo ya Id El Fitr.

Dk. Shein pia, alieleza kuwa Zanzibar ni miongoni mwa nchi nyingi  katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati iliyotoa wanazuoni kadhaa, hapo siku za nyuma ambapo pia, watu wengi kutoka ukanda huo walikuja kusoma elimu ya dini ya Kiislamu Zanzibar.

Hivyo, Rais Dk. Shein aliwataka Vijana waendelee kusoma zaidi elimu ya dini ya Kiislamu ili wafike hatua waliyofika wazee wao hapo siku za nyuma.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alieleza miongoni mwa faida za funga kiafya na kueleza kuwa wataalamu wa afya waliobobea walifanya utafiti wa kuthibitisha ukweli kwamba funga ya Ramadhani inaimarisha afya kwa kiasi kikubwa kwa mtu aliefunga.

Alieleza kuwa kiafya miili yote inahitaji mazoezi hivyo ipo haja ya kufanya mazoezi kwani bila ya kufanya mazoezi mwili hubaki na mafuta mengi ambayo hatimae kusababisha maradhi kadhaa yakiwemo maradi ya moyo na kisukari.

Alisisitiza kuwa kuna  haja ya kufanya mazoezi kwani watu walio wengi wanaona maradhi ya moyo na sukari yako mengi hivi sasa lakini hiyo imekuja kutokana na watu wengi kujiangalia afya zao kinyume na ilivyokuwa hapo siku za nyuma lakini hata hivyo, maradhi hayo yalikuwepo tokea zamani.

Alhaj Dk. Shein pia, alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa vijana wa Zanzibar wanaoshiriki mashidano ya kuhifadhi Qur-an na kupata nafasi za juu katika mashidano hayo yanayofanyika ndani na nje ya nchi na kuweza kuijengea sifa nchi yao kama ilivyokuwa hapo  siku za nyuma.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.