Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, Afungua Maonesho ya Kilimo Zanzibar.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Saba ina dhamiria kuendeleza sekta ya kilimo kwa gharama yoyote ile kutokana na umuhimu wa sekta hiyo.

Dk. Shein aliyasema hayo katika ufunguzi wa Maonyesho ya Nane Nane yaliyofanyika huko Langoni, Wilaya ya Magharibi “A” Mkoa wa Mjini Magharibi ambayo yalihudhuriwa na viongozi mbali mbali wa vyama vya siasa na Serikali akiwemo Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd pamoja na wananchi wengine.

Rais Dk. Shein alisema kuwa kwa kutekeleza dhamira hio, Serikali imechukua mkopo wa Dola za Kimarekani milioni 59 kutoka Exim Benki ya Jamhuri ya Korea kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji maji katika hekta 1,524 Unguja na Pemba.

Aliyataja mabonde yatakayohusika na mradi huo kuwa ni Makwararani, Mlemele kwa upande wa Pemba na Cheju, Kibokwa, Chaani, Kinyasini na Bumbwisudi kwa Unguja ambapo hivi sasa mkandarasi wa Kampuni ya KOLON kutoka Jamhuri ya Korea tayari ameshaanza ujenzi huo kwa bonde la Chaani na Kinyasini.

Alieleza kuwa lengo kuu ni kuimarisha kilimo cha kisasa kwa kuongeza zao la mpunga nchini na kupunguza kwa kiasi kikubwa kuutegemea mchele kutoka nje ya Zanzibar, huku akiiagiza Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi kuongeza maduka wanayouza mchele ambao unazalisha hapa Zanzibar.

Aliongeza kuwa Serikali imetenga Dola za Kimarekani Milioni 20 ambazo ni zaidi ya TZS milioni 40, ambapo Milioni 10 kutoka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Milioni 10 ni msaada wa Mfuko wa “Khalifa Fund” kutoka Umoja wa Nchi za Falme za Kiarabu (UAE) kwa kipindi cha miaka mitano kutoka 2019 hadi 2024.

Hii ni kwa ajili ya program ya kuwaendeleza vijana ambapo sekta ya Kilimo itakuwa ni sekta ya kipaumbele ambapo lengo kuu la hatua hii ni kutoa fursa nyingi za ajira kwa vijana, kuongeza uzalisjai na hatimae kukuza uchumi wa Zanzibar.

Alisisitiza kuwa katika mwaka wa fedha wa 2019/2020 bajeti ya kilimo imeongezeka  hadi kufikia TZS bilioni  88.17 kutoka TZS bilioni 62.62 zilizoingizwa mwaka 2018/2019 ambapo ongezeko hilo ni sawa na asilimia 29 ambalo ni kubwa kwa kipindi cha mwaka mmoja.

“Serikali itahakikisha kwamba inaendelea kuongeza bajeti ya kilimo kila mwaka, lisilobudi hutendwa kwa kuzingatia sheria na taratibu kwani sekta ya kilimo kwa ujumla wake ni miongoni mwa sekta zilizo muhimu sana kwa maendeleo ya nchi yetu” alisisitiza Rais Dk. Shein.

Aidha, Rais Dk. Shein alisema kuwa sekta ya kilimo ambayo kama inavyoeleweka kuwa inajumuisha mazao, mifugo, uvuvi, misitu na maliasili zisizorejesheka inaendelea kuwa ni tegemeo kubwa kwa uchumi wa Zanzibar na inachangia moja kwa moja kwa wananchi katika kujikimu maisha yao.

Rais Dk. Shein alisema kuwa kauli mbiu ya mwaka huu isemayo “Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa Ukuaji wa Uchumi wa Nchi Yetu” inakwenda sambamba na Mipango na Mikakati ya Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu ya mwaka 2015-2020, MKUZA III na Malengo Makuu ya Maendeleo Endelevu.

Alisema kuwa sekta ya kilimo, ufugaji na uvuvi zimepangiwa mikakati madhubuti inayohakikisha kwamba malengo ya Serikali yanatimizwa kwa mafanikio makubwa katika kuinua sekta hizo.

Pia, Rais Dk. Shein alisema kuwa ili kuweza kupata mafanikio mazuri katika kuendeleza sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi, Serikali imeweka mkazo zaidi hivi sasa wa kuziendeleza sekta hizo kwa kutumia teknolojia na mbinu ya kisasa.

Kwa lengo la kuendeleza sekta ya uvuvi, Rais Dk. Shein alisema kuwa Serikali imetenga jumla ya TZS Bilioni 2.2 kwa ajili ya ununuzi wa boti mbili za uvuvi zenye uwezo wa kuchukua tani 43 za samaki na kuvua katika kina kirefu cha maji;

Dk. Shein alisema kuwa boti hizo zinatoka Srilanka na Maldives ambapo boti moja itafika nchini hivi karibuni huku Serikali ikiwa katika hatua za mwisho za matayarisho ya ujenzi wa jengo la Kampuni ya Uvuvi ya Zanzibar (ZAFICO) lenye thamani ya TZS Bilioni 6.0 ambapo pia, kitakuwepo kiwanda cha samaki.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa katika kuendeleza aukuaji wa biashara ya dagaa ambayo inakua kwa kasi hapa Zanzibar na kutoa ajira kwa makundi mbali mbali, Serikali imemamua kujenga ujenzi wa kiwanda cha kukaushia dagaa chenye thamani ya TZS milioni 500 chenye uwezo wa kutoa dagaa kavu tani 10 kwa siku.

Alieleza hatua zilizochukuliwa na Serikali kwa kupata msaada wa TZS Bilioni 18 kutoka Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Japan (JICA) na Serrikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imetenga TZS Bilioni 3.6 kwa ajili ya diko na soko la kisasa la samaki katika bandari ya Malindi, ambapo matayarisho ya ujenzi wa soko hilo yameshaanza na ujenzi utakapokamilika litaweza kutoa huduma kwa wananchi wapatao 6,500.

Rais Dk. Shein alisisitiza kuwa anachotaka hivi sasa vijana waandaliwe ipasavyo kimawazo, kimtizamo, na kimkakati ili wapende kujiajiri wenyewe katika Nyanja mbalimbali za kiuchumi.

Hivyo, alitoa agizo kwa Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi na Wizara ya Vijana, Utamaduni, Sanaa na Michezo zihakikishe kwamba katika siku hizo saba za maonyesho hayo mwaka huu inapeleka makundi mbalimbali ya wanafunzi hasa wa Taasisi ya elimu ya juu kwa utaratibu maalum.

Nae Kaimu Waziri wa Kilimo , Maliasili, Mifugo na Uvuvi ambaye pia ni Waziri wa Ujenzi, mawasiliano na Usafirishaji Dk. Sira Ubwa Mamboya alitoa shukurani kwa Rais Dk. Shein kwa miongozo na busara zake katika uongozi wake hatua ambayo pia imeleta maendeleo katika wizara hiyo sambamba na kufanyika kwa maonyesho hayo.

Mapema Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Mariam Abdalla Sadalla alieleza kuwa maonyesho hayo ya pili ya kilimo yaliyoanza mwaka 2017 yameweza kufanikiwa kwa kiasi kikubwa na kupelekea  jumla ya taasisi 172 kushiriki  ikilinganishwa na taasisi 83 zilizoshiriki mwaka huo wa 2017.

Alieleza kuwa matayarisho yake yalianza mwezi Mei mwaka huu ikizishirikisha Sekta za Serikali, binafsi na wajasiriamali ambapo  jumla ya TZS milioni 106 zimetumika ambapo Serikali imetoa TZS milioni 86 na zilizobaki zimetoka kwa sekta binafsi na wajasiriamali.

Mapema kabla ya kuyafungua maonyesho hayo Rais Dk. Shein alitembelea eneo la mabanda ya maonyesho na kupata maelezo kutoka kwa wahusika.
  
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.