Waziri wa Nchi Ofisi ya
Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. George Simbachawene akiwasilisha
azimio la kuridhia Mkataba wa Minamata kuhusu zebaki mbele ya Bunge hii leo
mjini Dodoma. Bunge limeridhia Mkataba wa Minamata kuhusu zebaki na Serikali
imeandaa Mpango kazi wa Taifa wa kupunguza matumizi ya zebaki kwa wachimbaji
wadogo ambao umeainisha fursa mbalimbali.
Na. Lulu Mussa. Dodoma.
Waziri
wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. George
Simbachawene amesema inakadiriwa kuwa asilimia 25 hadi 33 ya wachimbaji
wadogo wa dhahabu hapa nchini, wameathiriwa na Zebaki kwa kupata magonjwa
yakiwemo yale ya mifumo ya neva za fahamu, uzazi, upumuaji, figo, moyo, na
udhaifu wa mwili.
Akiwasilisha
azimio la Bunge la kuridhia Mkataba wa Minamata kuhusu zebaki Simbachawene amesema,
baadhi ya athari kwa mazingira zilizobainika kutokana na matumizi ya zebaki ni
pamoja na kudhoofika kwa ukuaji wa viumbe hai wanaoishi ndani ya maji; uchafuzi
wa mfumo mfuatano wa mazao ya chakula, mifugo na samaki; na uchafuzi wa vyanzo
vya maji, hewa na udongo.
“Lengo
kuu la Mkataba huu ni kulinda afya ya binadamu na mazingira dhidi ya athari za
uchafuzi wa mazingira unaotokana na matumizi ya Zebaki katika hatua za uzalishaji,
matumizi na utupaji wake” Simbachawene alisisitiza.
Simbachawene
ameainisha sheria ambazo zinatoa mwongozo wa jumla kuhusu usimamizi wa Zebaki
ikiwa ni pamoja na Sheria ya Usimamizi wa Mazingira (2004); Sheria ya Udhibiti
na Usimamizi wa Kemikali za Viwandani na Majumbani (2003); Sheria ya Madini
(2010); Sheria ya Afya ya Jamii (2009); Sheria ya Usalama na Afya Mahali pa
Kazi (2003); na Sheria ya Chakula na Dawa (2003) na kusisitiza kuwa
zitaandaliwa kanuni za Usimamizi wa Zebaki chini ya Sheria ya Usimamizi wa
Mazingira (2004) ili kuwezesha utekelezaji wa Mkataba huu.
Tafiti
zinaonyesha kuwa zebaki hudumu katika mazingira kwa muda mrefu (miaka 2 hadi 20) na husafiri masafa marefu kwa njia ya hewa, maji (mito, maziwa
na bahari) na udongo umbali hadi kilomita 1,000
kutoka kwenye chanzo; na kuathiri afya ya binadamu, viumbe wengine na
mazingira. Athari hizi zinajitokeza zaidi katika nchi zinazoendelea
ukilinganisha na nchi zilizoendelea kutokana na nchi hizo kupunguza matumizi ya
Zebaki.
Awali
akiwasilisha hoja za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na
Mazingira Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Suleiman Ahmed Sadiq amesema Kamati
ianona umuhimu wa nchi kuridhia Mkataba huu kwa lengo la kushirikiana na nchi
nyingine kutafuta suluhisho la zebaki bila kuathiri shughuli za wachimbaji wadogo.
“Ushauri
wa Kamati ni kuwa Serikali ijitahidi kuhakikisha inapatikana teknolojia rahisi
na rafiki kwa wachimbaji wadogo kwa gharama nafuu” alisisitiza Mhe. Sadiq.
Zebaki ni
miongoni mwa kemikali zinazohatarisha zaidi afya ya jamii duniani kutokana na
kudumu katika mazingira kwa muda mrefu, kusafiri masafa marefu kwa njia ya
hewa, maji (mito, maziwa na bahari) na udongo na hivyo kuathiri afya ya
binadamu na mazingira. Jumla ya nchi 113
zimeridhia Mkataba huu ambao ulianza kutekelezwa rasmi tarehe 16 Agosti, 2017
mara baada ya Nchi 50 kuridhia kama
inavyotakiwa na Ibara ya 30 ya Mkataba wa Minamata.
No comments:
Post a Comment