Habari za Punde

Zanzibar inakusanya TZS Bilioni 65.7 kwa mwezi.


RAIS  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa Maafisa Wadhamini wanadhima kubwa ya kuwasimamia wale wote wanaovunja misingi ya kukuza uchumi hapa nchini.

Dk. Shein aliyasema hayo leo, huko katika ukumbi wa Kiwanda cha Mafuta na Makonyo Wawi wakati alipokutana na Watendaji na Viongozi Wakuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na viongozi wa vikosi vya SMZ na SMT wanaofanya kazi zao kisiwani Pemba.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa, kwa mwaka jana kasi ya ukuaji wa uchumi wa Zanzibar ilifikia asilimia 7.1 na matarajio ni kukua kwa uchumi huo mwaka hadi mwaka kutokana na kuongezeka kwa shughuli za kiuchumi na kijamii.

Alisema kuwa mapato yanakusanywa kwa ufanisi mzuri na kinachokusanywa ndicho kinachotumika na hakuna tatizo la matumizi ndani ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa hivi sasa.

Alieleza kuwa kuhusiana na mapato Rais Dk. Shein alisema kuwa wakati anaigia madarakani mwaka 2010 Serikali ilikuwa ikikusanya TZS Bilioni 13.5 kwa mwezi ambapo kwa hivi sasa Zanzibar inakusanya TZS Bilioni 65.7 kwa mwezi.

Aliongeza kuwa mambo mengi yanayofanywa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar yanatekelezwa kutokana na fedha zake wenyewe ambapo licha ya kukusanywa kiasi hicho cha fedha lakini bado hakitoshi, hivyo juhudi zaidi zinahitajika.

Alieleza kuwa mbali ya juhudi hizo za Seriakli lakini bado wapo wafanyabiashara wanaokwepa kulipa kodi na kusisitiza kuwa Serikali zote duniani zinakwenda kwa kukusanywa kodi.

Alitumia fursa hiyo kusisitiza haja ya kulipa kodi sambamba na kutoa risiti kwani bila ya kutoa ama kuchukua risiti mapato makubwa ya Serikali yanapotea.

Kuhusiana na suala zima la mfumko wa bei, Rais Dk. Shein alisema kuwa Zanzibar uko chini ambapo wakati anaingia madarakani ulikuwa asilimi 18 na kila siku unashuka na hadi hivi leo uko chini ya tarakimu moja huku bei ya bidhaa hivi sasa imepungua sana.

Licha ya baadhi ya wafanyabiashara kupandisha bidhaa bei pamoja na kufanya magendo lakini hata hivyo, juhudi zinaendelea kuchukuliwa kwa lengo la kuhakikisha wananchi wa Zanzibar wanaishi vizuri.

Aidha, Rais Dk. Shein alisisitiza kuwa kuna kila sababu ya wananchi wa Zanzibar kutibiwa bure sambamba na kupewa huduma zote za uchunguzi wa afya na kuitaka Wizara ya Afya kusimamia kwa wale wote watakaofanya hadaa washtakiwe kwa kuhujumu uchumi.

Rais Dk. Shein alieleza juhudi za makusudi zitakazochukuliwa na Serikali katika kuhakikisha Wilaya ya Micheweni inaongeza kiwango cha upatikanaji wa maji safi na salama huku akieleza kuwa hadi mwishoni mwa mwaka huu katika Mji wa Zanzibar na vitongoji vyake ukiwemo Mji Mkongwe tatizo la maji litakuwa historia.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein aliwaeleza viongozi hao haja kuwasikiliza watu wanaokwenda maofisini mwao kufuata huduma na kwamwe wasikatae kuwasikiliza kwani moja kati ya sifa ya kiongozi ni kuwasikiliza wananchi na ndipo watakapofanya vyema kazi zao.

Pia, alieleza haja kwa Maafisa Wadhamini kusimamia nidhamu sambamba na uhujumu wa mali ya umma ikiwa ni pamoja na kutumia vyema fedha za Serikali kwa taratibu zilizowekwa.

Dk. Shein alisisitiza haja ya kupambana na rushwa katika utendaji wao wa kazi na kusisitiza haja ya kushikamana na kuwapongeza viongozi hao kwa kuendelea kushirikiana vyema katika utendaji wao wa kazi.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alieleza haja kwa viongozi hao kusimamia vyema vitendo vinavyopelekea kuporomoka kwa maadili, malezi na inswafu ya maisha.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alieleza mikakati iliyowekwa na Serikali katika kuhakikisha inatekeleza vyema shughuli zake ikiwa ni pamoja na kupunguza safari za viongozi, semina na mikutano, posho za vikao vya kazi sambamba na kufanya mikutano na semina hizo katika kumbi za Wizara za Serikali badala ya kufanywa kwenye kumbi za hoteli binafsi.

Pia, alitumia fursa hiyo akuwashukuru viongozi na wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) pamoja na viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa mapokezi makubwa waliyomfanyia siku aliyowasili kisiwani humo.

Rais Dk. Shein alimpongeza Waziri wa Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi Mmanga Mjengo Mjawiri kwa kufanikisha vyema Maonyesho ya Siku ya Chakula Duniani yanayoendeleo huko Chamanangwe Kisiwani Pemba.

Vile vile, Rais Dk. Shein alieleza matarajio yake kwa mikutano yake aliyoifanya na Wazee wa CCM wa Wilaya zote Kisiwa humo.

Rais Dk. Shein alieleza kufurahishwa na hali ya amani na utulivu iliyopo kisiwani Pemba na kutoa pongezi kwa viongozi wote wenye majukumu ya kuisimamia hali hiyo huko Kiswani Pemba.

Alisema kuwa CCM inaidhibiti vizuri hali ya siasa hapa nchini kwani uchumi ni siasa hivyo, chama hicho kusimamia vyema siasa nchini kwani utulivu unategemea mahitaji ya wananchi na kuwataka viongozi kuyaeleza hayo kwa wananchi.

Mapema Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Issa Ussi Haji Gavu alimkaribisha Rais Dk.Shein kuzungumza na viongozi hao.

Nae Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ Haji Omar Kheir alimpongeza Rais Dk. Shein kwa uwamuzi wake huo wa kuzungumza na watendaji pamoja na viongozi hao na kuahidi kutekeleza yale yote aliyowaagiza kwa niaba ya viongozi wote.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.