RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa Maafisa Wadhamini wanadhima
kubwa ya kuwasimamia wale wote wanaovunja misingi ya kukuza uchumi hapa nchini.
Dk. Shein aliyasema hayo leo, huko katika
ukumbi wa Kiwanda cha Mafuta na Makonyo Wawi wakati alipokutana na
Watendaji na Viongozi Wakuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na
viongozi wa vikosi vya SMZ na SMT wanaofanya kazi zao kisiwani Pemba.
Rais Dk. Shein alieleza kuwa, kwa
mwaka jana kasi ya ukuaji wa uchumi wa Zanzibar ilifikia asilimia 7.1 na
matarajio ni kukua kwa uchumi huo mwaka hadi mwaka kutokana na kuongezeka kwa
shughuli za kiuchumi na kijamii.
Alisema kuwa mapato yanakusanywa kwa
ufanisi mzuri na kinachokusanywa ndicho kinachotumika na hakuna tatizo la
matumizi ndani ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa hivi sasa.
Alieleza kuwa kuhusiana na mapato Rais
Dk. Shein alisema kuwa wakati anaigia madarakani mwaka 2010 Serikali ilikuwa
ikikusanya TZS Bilioni 13.5 kwa mwezi ambapo kwa hivi sasa Zanzibar inakusanya
TZS Bilioni 65.7 kwa mwezi.
Aliongeza kuwa mambo mengi
yanayofanywa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar yanatekelezwa kutokana na
fedha zake wenyewe ambapo licha ya kukusanywa kiasi hicho cha fedha lakini bado
hakitoshi, hivyo juhudi zaidi zinahitajika.
Alieleza kuwa mbali ya juhudi hizo za
Seriakli lakini bado wapo wafanyabiashara wanaokwepa kulipa kodi na kusisitiza
kuwa Serikali zote duniani zinakwenda kwa kukusanywa kodi.
Alitumia fursa hiyo kusisitiza haja ya
kulipa kodi sambamba na kutoa risiti kwani bila ya kutoa ama kuchukua risiti
mapato makubwa ya Serikali yanapotea.
Kuhusiana na suala zima la mfumko wa
bei, Rais Dk. Shein alisema kuwa Zanzibar uko chini ambapo wakati anaingia
madarakani ulikuwa asilimi 18 na kila siku unashuka na hadi hivi leo uko chini
ya tarakimu moja huku bei ya bidhaa hivi sasa imepungua sana.
Licha ya baadhi ya wafanyabiashara
kupandisha bidhaa bei pamoja na kufanya magendo lakini hata hivyo, juhudi
zinaendelea kuchukuliwa kwa lengo la kuhakikisha wananchi wa Zanzibar wanaishi
vizuri.
Aidha, Rais Dk. Shein alisisitiza kuwa
kuna kila sababu ya wananchi wa Zanzibar kutibiwa bure sambamba na kupewa
huduma zote za uchunguzi wa afya na kuitaka Wizara ya Afya kusimamia kwa wale
wote watakaofanya hadaa washtakiwe kwa kuhujumu uchumi.
Rais Dk. Shein alieleza juhudi za
makusudi zitakazochukuliwa na Serikali katika kuhakikisha Wilaya ya Micheweni
inaongeza kiwango cha upatikanaji wa maji safi na salama huku akieleza kuwa
hadi mwishoni mwa mwaka huu katika Mji wa Zanzibar na vitongoji vyake ukiwemo
Mji Mkongwe tatizo la maji litakuwa historia.
Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein
aliwaeleza viongozi hao haja kuwasikiliza watu wanaokwenda maofisini mwao
kufuata huduma na kwamwe wasikatae kuwasikiliza kwani moja kati ya sifa ya
kiongozi ni kuwasikiliza wananchi na ndipo watakapofanya vyema kazi zao.
Pia, alieleza haja kwa Maafisa
Wadhamini kusimamia nidhamu sambamba na uhujumu wa mali ya umma ikiwa ni pamoja
na kutumia vyema fedha za Serikali kwa taratibu zilizowekwa.
Dk. Shein alisisitiza haja ya
kupambana na rushwa katika utendaji wao wa kazi na kusisitiza haja ya kushikamana
na kuwapongeza viongozi hao kwa kuendelea kushirikiana vyema katika utendaji
wao wa kazi.
Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein
alieleza haja kwa viongozi hao kusimamia vyema vitendo vinavyopelekea
kuporomoka kwa maadili, malezi na inswafu ya maisha.
Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein
alieleza mikakati iliyowekwa na Serikali katika kuhakikisha inatekeleza vyema
shughuli zake ikiwa ni pamoja na kupunguza safari za viongozi, semina na
mikutano, posho za vikao vya kazi sambamba na kufanya mikutano na semina hizo
katika kumbi za Wizara za Serikali badala ya kufanywa kwenye kumbi za hoteli
binafsi.
Pia, alitumia fursa hiyo akuwashukuru
viongozi na wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) pamoja na viongozi wa
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa mapokezi makubwa waliyomfanyia siku
aliyowasili kisiwani humo.
Rais Dk. Shein alimpongeza Waziri wa
Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi Mmanga Mjengo Mjawiri kwa kufanikisha vyema
Maonyesho ya Siku ya Chakula Duniani yanayoendeleo huko Chamanangwe Kisiwani
Pemba.
Vile vile, Rais Dk. Shein alieleza
matarajio yake kwa mikutano yake aliyoifanya na Wazee wa CCM wa Wilaya zote
Kisiwa humo.
Rais Dk. Shein alieleza kufurahishwa
na hali ya amani na utulivu iliyopo kisiwani Pemba na kutoa pongezi kwa
viongozi wote wenye majukumu ya kuisimamia hali hiyo huko Kiswani Pemba.
Alisema kuwa CCM inaidhibiti vizuri
hali ya siasa hapa nchini kwani uchumi ni siasa hivyo, chama hicho kusimamia
vyema siasa nchini kwani utulivu unategemea mahitaji ya wananchi na kuwataka
viongozi kuyaeleza hayo kwa wananchi.
Mapema Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Issa Ussi Haji Gavu alimkaribisha Rais
Dk.Shein kuzungumza na viongozi hao.
Nae Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais
Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ Haji Omar Kheir
alimpongeza Rais Dk. Shein kwa uwamuzi wake huo wa kuzungumza na watendaji
pamoja na viongozi hao na kuahidi kutekeleza yale yote aliyowaagiza kwa niaba
ya viongozi wote.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024
2231822
E-mail:
rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment