Habari za Punde

Rais Magufuli Mgeni Rasmi Maadhimisho ya Sherehe za Miaka 58 ya Uhuru Jijini Mwanza

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. John Mongella akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maadhimisho ya miaka 58 ya Uhuru wa Tanzania Bara itakayofanyika Jijini Mwanza, maadhimisho hayo yanafanyika Mkoani humo kwa mara ya kwanza.
Sehemu ya Waandishi wa Habari wakifuatilia mkutano wa Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. John Mongella na waandishi wa habari kuhusu maadhimisho ya miaka 58 ya Uhuru wa Tanzania  Bara yatakayofanyika Jijini Mwanza, maadhimisho hayo yanafanyika mkoani humo kwa mara ya kwanza.


Na Mwandishi Wetu- Mwanza.                                                                                                               
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya sherehe za miaka 58 ya Uhuru wa Tanzania Bara na miaka 57 ya Jamhuri  zinazotarajiwa kufanyika Kitaifa mkoani Mwanza.

Akizungumza na waandishi wa habari Mkuu wa Mkoa huo Mhe. John Mongella amesema kuwa maadhimisho hayo yatafanyika Disemba 9, 2019 kwa mara ya kwanza katika mkoa huo katika uwanja wa CCM Kirumba.

Kauli mbiu ya sherehe hizo ni “ Miaka 58 ya Uhuru na miaka57 ya Jamhuri:Uzalendo, Uwajibikaji na Ubunifu ni Msingi wa Ujenzi wa Uchumi wa Taifa Letu,” Alisistiza Mhe. Mongella.

Akifafanua amesema kuwa Shughuli zitakazofanyika wakati wa madhimisho hayo ni pamoja na gwaride maalum, burudani kutoka kwa wasanii wa kizazi kipya,ngoma za asili kutoka mikoa ya Mwanza, Kagera na Mara.

Aidha Mhe. Mongella amesema kuwa kutakuwa na shughuli mbalimbali kuelekea maadhimisho hayo ikiwemo Mashindano ya ngonjera, Maigizo,Kwaya,Mashairi, Mashindano ya mbio za mitumbwi,Bonanza la michezo, mchezo wa bao, na mechi ya mpira wa miguu.

Shughuli za kikanda zitakazofanyika ni pamoja  Kongamano la Wanafunzi wa vyuo vya Elimu ya Juu litakalofanyika tarehe 6, Disemba, 2019 Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino Mwanza.

Alibainisha kuwa baadhi ya viongozi wanaotarajiwa kuhudhuria sherehe hizo ni pamoja na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan,Waziri mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa na Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe Dkt. Ali Mohamed Shein.

Viongozi wastaafu wakiwemo Marais, Makamu wa Rais na Mawaziri Wakuu ni miongoni mwa waalikwa wa sherehe hizo,Aidha , Mawaziri, Makatibu Wakuu, Wakuu wa Taasisi mbalimbali za Serikali na Mabalozi wanaowakilisha nchi zao nchini ni miongoni mwa waalikwa wa sherehe hizo.

Juma la kilele cha maadhimisho hayo litakuwa na shughuli mbalimbali zitakazofanyika kikanda kuanzia Disemba 2, 2019 hadi tarehe 8 Disemba, 2019 kwenye mikoa ya Kagera, Mara, Geita, Simiyu, Shinyanga na Mwanza.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.