Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Mfuko
wa Taifa wa Bima ya Afya Mhe. Anne Makinda akimpokea Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Mhe.
Albert Chalamila wakati wa hafla ya uzinduzi wa kampeni ya kuhamasisha wananchi
kujiunga na vifurushi vya Bima ya Afya, leo 16.12.2019 Mkoani Mbeya.
Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Mhe. Albert Chalamila akiongea
na wananchi wakati wa hafla ya uzinduzi wa kampeni ya kuhamasisha wananchi
kujiunga na vifurushi vya Bima ya Afya, ambapo aliwataka wananchi kujiunga na
vifurushi vya Bima ya Afya na kuacha kusikiliza maneno ya baadhi ya watu
wanaojaribu kupotosha kuhusu suala la vifurushi, Kushoto ni Mwenyekiti wa Bodi
ya Wakurugenzi wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya Mhe. Anne Makinda.
Wakazi wa Mbeya wakifuatilia matukio wakati
wa hafla ya uzinduzi wa kampeni ya kuhamasisha wananchi kujiunga na vifurushi
vya Bima ya Afya, 16.12.2019 Mkoani Mbeya.
Picha na Idara ya Habari Maelezo
Na Mwandishi Wetu-MBEYA
Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Mhe. Albert Chalamila
amewataka watanzania kujikatia Bima ya Afya kwa mpango wa vifurushi kuwapuuza
baadhi ya watu wanaohusisha siasa na mpango huu ulioletwa kuwafikia watanzania
wengi zaidi.
Mhe. Chalamila ameyasema hayo wakati wa
uzinduzi wa kampeni za kuhamasisha wananchi kujiunga na vifurushi vya Bima ya
Afya katika uwanja wa stendi ya Kabwe, Jijini Mbeya.
Mhe. Chalamila amesema kuwa nchi yoyote ili
iweze kujipatia maendeleo katika sekta zote ni muhimu kwa wananchi kuwa na afya
bora na ndio maana Serikali imeendelea kuwekeza katika sekta hii ikiwemo kuja
na vifurushi vya Bima ya Afya ili kuwafikia watanzania wengi zaidi.
“Ndugu zangu Afya haina siasa, Afya ni uhai
tusidanganywe, tujitenge na siasa za kupotoshwa juu ya mfumo huu wa bima, awali
kwa mtu mmoja ilikuwa ni lazima uwe na zaidi ya milioni moja ili kuwa na bima
ya afya, lakini kwa utaratibu huu wa vifurushi sasa unapata kadi ya bima ya
afya kwa shilingi laki moja na tisini na mbili tu”- Alisema Mhe. Chalamila.
Aidha Mhe. Chalamila aliongeza kuwa ugonjwa
hauna hodi ni vizuri kila mtanzania kufanya maamuzi ya kujikatia bima kwani
wapo watu wengi wamekuwa wakipoteza maisha kutokana na gharama kubwa za
matibabu, hivyo mfumo huu wa vifurushi ni suluhisho kwa changamoto hiyo.
Awali akiongea katika hafla hiyo Mwenyekiti
wa Bodi ya Wakurugenzi wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya Mhe. Anne Makinda
amesema kuwa tangu kuzinduliwa kwa mfuko huu muitikio wa watanzania umekuwa ni
mkubwa.
Mhe. Makinda amesema kuwa Mfuko upo katika
utaratibu wa kuanzisha mpango wa DUNDULIZA ambao utawawezesha watanzania
kujiwekeaa fedha kidogkidogo hadi
akamilishe kulipia bima yake.
Pia Mhe. Makinda aliwataka watoa huduma
kubadilika na kuwahudumia vizuri wananchi
aendapo kupata huduma za afya kwani mfuko hautotoa kibali kwa hospitali
yoyote ambayo itanyanyasa wanufaika wa Bima.
Naye Kaimu Mkurugenzi wa Mfuko wa Taifa wa
Bima ya Afya Bw. Christopher Mapunda amesema kuwa uanzishwaji wa Vifurushi ni
fursa kwa wananchi kujiunga na bima ya afya kuanzia kiwango cha 192,000 na
kuwawezesha kupata huduma ya uhakika ya matibabu hasa kutokana na kuongezeka
kwa gharama za matibabu siku hadi siku.
Akiongea baada ya kupatiwa kadi ya Bima ya
Afya Bw. Emanuel Mushi amesema kuwa
mpango huu ni mzuri kwani afya ni muhimu na mpango huu wa vifurushi ni mzuri
kutokana na kupungua kwa gharama kutoka Milioni moja na laki Tano hadi sasa
imepungua na kufikia Shilingi laki moja na tisini na mbili kwa mtu mmoja
No comments:
Post a Comment