Habari za Punde

BODI YA URATIBU WA NGOs YATOA MAAGIZO MAZITO KWA BARAZA LA NGOs

Mwenyekiti wa Bodi ya Uratibu wa Mashirika Yasiyo Ya kiserikali Dkt. Richard Faustine Sambaiga akitoa maagizo kwa Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali akiwataka kufanya marekebisho muhimu ya uendeshaji wa Chombo hicho na kutoa taarifa ya uzingatiaji wa maagizo kuhuisha utendaji wao ndani ya kipindi cha siku 30 wakati alipokutana na wajumbe wa Baraza hilo na baadhi ya waandishi wa habari kwenye kikao kilichofanyika ukumbi wa NIMR jijini Dar es salaam kulia ni Mwenyekiti wa Baraza la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali Bw. Nicolaus Zachariah .
Na Mwandishi Wetu Dar es Salaam
Bodi ya Uratinu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali nchini imeliagiza Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kukutana ili kuhakikisha wanatatua changamoto za uendeshaji wa Baraza hilo kikamilifu na kutoa taarifa kwa Bodi ndani ya siku 14 jinsi walivyoshughulikia changamoto hizo, ikiwa ni pamoja na kuwasilisha taarifa ya utekelezaji ya Baraza hilo.
Agizo hilo limetolewa leo jijini Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Bodi hiyo Dkt. Richard Faustine Sambaiga wakati akizungumza na wajumbe wa Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali katika kikao  kilicholenga kutoa maelekezo mahsusi kwa Baraza ili kukitaka chombo hicho kuzingatia matakwa ya kisheria katika uendeshaji wake.
Dkt. Sambaiga ameliagiza Baraza hilo kufanya mapitio ya Kanuni  ya Sheria ya marekebisho Na. 11/2005 na Sheria ya marekebisho Na.3/201 ili kuweza kukidhi mapendekezo ya mapitio ya Kanuni hizo na kuwasilisha kwenye Bodi ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ndani ya siku 30 ili kuondoa mkwamo wa kiutendaji wa majukumu ya Baraza la NGOs nchini.
Pia  Dkt. Sambaiga ameliagiza  Baraza hilo kujielekeza kwenye matakwa ya muda wa kisheria wa kuwa kiongozi wa Baraza hilo ambao ni miaka mitatu toka kuteuliwa kwa Baraza mwaka 2016, na hivyo kuelekeza kuanza kwa mchakato wa uchaguzi wa Baraza jipya ndani ya siku 30.

“Nalielekeza Baraza kupitia upya uwakilishi wa wajumbe wa Mikoa na makundi maalum hasa ikizingatiwa ipo Mikoa mipya na makundi ambayo hayana wawakilishi kwani kumekuwa na changamoto kubwa ya uwakilishi wa wajumbe kutoka mikoani” alisema.

Aidha Dkt. Sambaiga amewataka Viongozi wa Baraza la Taifa kuzingatia uwasilishaji wa taarifa yake ya utekelezaji wa kazi zake kwa  Bodi ili kutosababisha Bodi kushindwa kutekeleza majukumu yake ya kisheria kama yalivyoainishwa kwenye kifungu 7(1) (j) cha Sheria ya Mashirika yasiyo ya Kiserikali kinachoitaka Bodi kupokea kujadili na kupitisha taarifa za Baraza hilo.

Dkt. Sambaiga amelitaka Baraza kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Sheria ikiwemo kutetea maslahi ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kwa kuwa jukwaa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali na kuhakikisha wanakuwa  mwavuli wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali katika masuala yote yanayohusu uratibu na kutandaa kwa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali; na

“Nawasihi viongozi wa Baraza Kutunga na kusimamia utekelezaji wa Kanuni za Maadili kwa lengo la kuwezesha Mashirika Yasiyo ya kiserikali kujiongoza kwa  kufuata misingi ya kimaadili yenye uwazi na uwajibikaji.”

Mweyekiti wa Bodi ya Mashirika Yasika ya Kiserikali ameleza  kuwa maelekezo anayoyatoa yanalenga kuhakikisha kuwa Baraza la Mashirika ya NGOs linatekeleza kazi zake kikamilifu, kuimarisha uratibu wa sekta ya NGOs, kuondoa chanagmoto za uendeshaji wa NGOs hivyo Bodi ikalazimika kutoa maagizo thabiti kuboresha uendeshaji wa kazi za NGOs nchini.

Dkt Simbaiga amelieleza Baraza la Taifa la NGOs kuwa ulegevu wa kiutendaji ndani ya Baraza la NGOs unakwamisha utendaji wa kazi za Bodi ya NGOs amabzao wamekasimiwa kuzitekeleza kwa mujibu wa sharia, kanuni na taratibu. 
Naye Mwenyekiti wa Baraza la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali Bw. Nicolaus Zachariah ameshukuru kwa hatua iliyochukuliwa na Mwenyekiti wa Bodi ya NGOs ya kukutana na wajumbe wa Baraza la NGOs na kujadili masuala yenye chanagamoto katika uendesjai wa majukumu ya Baraza. Baraza la NGOs limepokea maelekezo ya Bodi na kukiri kuyafanyia kazi maagizo yote kwa pamoja kama yalivyowasilishwa na Bodi ya NGOs.

Aidha, Baraza la NGOs limeaomba kuendelea kupata ushauri wa kitaalam na msaada wa kisheria ili kuhakikisha kuwa maalekezo yote yanatekelezwa katika muda uliokubainishwa.   

Bodi ya Uratibu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali iliyoanzishwa  chini ya Kifungu cha 6 (1) cha Sheria ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali Na. 24 ya Mwaka 2002 kwa lengo la kuwakilisha Sekta ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ikiwa na jukumu la kusimamia uratibu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali nchini ikiwemo uendeshaji wa Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.