Habari za Punde

KAIMU KATIBU MKUU DKT.ALLY POSSI: BAKITA ONGEZENI MATUMIZI YA KISWAHILI KATIKA MTANDAO


Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni , Sanaa na Michezo Dkt.Ally Possi (kulia) akipokea zawadi ya Kamusi Kuu ya Kiswahili  iliyoandaliwa na Baraza la Kiswahili la Taifa kutoka kwa Katibu Mtendaji  Baraza la Kiswahili la Taifa  Dkt.Selemani Sewangi leo Jijini Dar es Salaam alipotembela ofisi hiyo kwa lengo la kufuatilia utekelezaji wa majukumu.

Na. Anitha Jonas – WHUSM,Dar es Salaam.
Kaimu  Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dkt.Ally Possi  amewataka wafanyakazi  wa Baraza la Kiswahili Taifa kuwa wabunifu  wa miradi itakayoliletea taifa matokeo chanya katika kutangaza lugha ya Kiswahili kwenye nyanja za Kimataifa .

Dkt.Possi ametoa kauli hiyo leo Jijini Dar es Salaam  alipotembelea  ofisi  za baraza hilo kwa  lengo kupata taarifa za utekelezaji wa mpango mkakati wake pamoja na kufahamu malengo ya taasisi hiyo katika kipindi cha kwanza kwa  mwaka wa fedha 2019/2020.

“Nawapongeza kwa mradi huu mzuri wa Kongoo sababu kazi mnayofanya yakuingiza maneno tabribani billion  moja ya Kiswahili katika mtandao  itasaidia  sana kukuza na kusambaza  lugha hii kwani sasa dunia imejikita zaidi katika tehama na shughuli nyingi zinafanyika kwa njia ya  mtandao hivyo uhifadhi wa maneno hayo ya Kiswahili katika mfumo huu ni hatua nzuri,”Dkt.Possi.

Akiendelea kuzungumza katika ziara hiyo Kaimu Katibu Mkuu huyo aliendelea kusisitiza kuwa BAKITA ni taasisi muhimu kwa taifa na wizara ipo tayari kwa kuwawezesha kufanikiwa kutekeleza majukumu yake ya kuweza kufanikisha lugha  hiyo inasonga mbele sababu kukua kwa lugha hiyo ni ufahari kwa  Tanzania na haswa  kama waasisi wa kutumia hugha hiyo.

Pamoja na hayo nae Katibu Mtendaji wa BAKITA Dkt.Selemani Sewangi  alitoa maombi Kaimu Katibu Mkuu huyo ya kuomba wizara iwasaidie katika kutangaza katika wizara mbalimbali kuwa wanauza Kamusi Kuu ya lugha ya Kiswahili iliyoandaliwa na baraza hilo yenye maneno mengi  kwani  uandaaji wa kamusi za Kiswahili ni moja ya majukumu yao.

“Tungependa  baraza lianze  kutoa mafunzo ya ukalimani kwa wahitimu wa chuo kikuu na wadau mbalimbali sababu tumeona kuna ombwe kubwa  la wataalamu wa lugha  wanaoweza kufanya kazi ya ukalimani hivyo tungeomba kupatiwa fedha ili kuweza kufanikisha kununua vifaa vya kutoa mafunzo hayo,”alisema Dkt.Sewangi.

Halikadhalika Dkt.Sewangi aliwashukuru  uongozi wa wizara kwa kuwapa ahadi ya kushughulikia suala ya baraza hilo kupata kiwanja cha kujenga ofisi ndani ya Jiji la  Dodoma ambapo ndiyo Makao Makuu ya Ofisi za Serikali .

Mbali na hayo nae mmoja wa wafakakazi wa baraza hilo ambaye ni  Mfasiri Mkuu Bibi. Vidah Mutasa  alitoa neno la shukrani baada kumalizika kwa kikao hicho cha kiongozi huyo wa wizara na wafanyakazi wa baraza kwa kuahidi kuchapa kazi na kuhakikisha wao kama mabalozi wa lugha hiyo wanahakikisha inasonga mbele.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.