Habari za Punde

JAMII IMETAKIWA KUPINGA UKATILI WA AINA ZOTE KUELEKEA SIKU YA WANAWAKE DUNIANI


Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Afya- Idara Kuu ya maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bw. Prudence Consntatine na kushoto ni Afisa Maendeleo ya Jamii Mkuu Bw. Erasto Chingoro (kulia) akitoa ufafanuzi wa baadhi ya maswali yaliyoulizwa na waandishi wa Habari kuhusu maandalizi ya Siku ya wanawake Duniani kwa mwaka 2020 katika kikao kilichofanyika Jijini Dar es salaam leo 

Na Mwandishi wetu Dar es salam
Serikali imeitaka jamii kuhakikisha inapinga ukatili wa aina zote ili kufikia malengo ya kuwa na kizazi chenye usawa kati ya wanawake na wanaume.
Akizungumza na waandishi wa Habari Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini katika Wizara ya Afya, Idara kuu ya maendeleo ya jamii Bw. Prudence Constantine mapema leo tarehe 21 Februari, 2020 jijini Dar es Salaam, amesema kuelekea maadhimisho ya siku ya Wanawake Duniani tarehe 08 Machi mwaka huu kauli mbiu imelenga kutengeneza jamii yenye usawa kati ya mwanaume na mwanaume.
”Katika miaka ya 1990 wanawake walikuwa wanafanya kazi nyingi, ujira kidogo, unyanyasaji, hawakupewa kipaumbele ikilinganishwa na wafanyakazi wanaume” amesema Prudence.
Amesema lengo la maadhimisho ya siku hiyo ni kutathmini utekelezaji wa afua za kufikia usawa wa jinsia na uwezeshaji wanawake kiuchumi, kijamii, kisiasa katika kufikia maendeleo jumuishi. Maadhimisho haya pia yanatoa fursa ya kuelimisha jamii kuhusu jitihada mbalimbali zilizofanywa na jamii, Serikali, Asasi za Kiraia, Sekta Binafsi na wadau wengine katika kukuza hali ya mwanamke wa kitanzania. Kadhalika, katika kuadhimisha Siku hii wadau wanapata fursa ya kubainisha upungufu na mbinu za utatuzi wa changamoto zilizopo.  
Bw. Prudence amesema Serikali imeendelea na jitihada za kuwawezesha wanawake kiuchumi kwa kuanzisha mfuko wa uwezeshaji kiuchumi ikiwa ni pamoja na mfuko wa maendeleo ya wanawake wenye masharti nafuu ambao umesaidia kutoa mikopo nafuu na mafunzo ya stadi za biashara kwa wajasiriamali wanawake.
“Wizara inahakikisha kutumia maadhimisho haya kwa kuandaa makongamano na majukwaa mbalimbali ili kujadili na kuibua kero zinazokwamisha maendeleo na Ustawi wa wanawake na kuyatafutia ufumbuzi ikiwemo matatizo ya maji na uchumi duni” amesema Bw. Prudence.
Ameongeza kuwa tangu mwaka 2015/16 hadi 2018/19 Serikali imetoa fedha kiasi cha Tsh. Bilioni 28.8 ambayo imesaidia vikundi vya wanawake 13,691 na kufanya idadi ya wanawake wajasiriamali walionufaika na fedha hizo kufikia 883,724 ukilinganisha na wanawake 12,842 kwa mwaka 2013/14.
Aidha, Serikali imewezesha wanawake wajasiriamali kushiriki katika maonesho ya biashara mbalimbali za Kitaifa na Kimataifa kwa mwaka 2017/18 ambapo wanawake wajasiriamali 1,183 kutoka katika Mikoa yote 26 wamenufaika na fursa hiyo kushiriki.

Naye Afisa maendeleo ya jamii Mkuu kutoka wizara ya Afya idara kuu ya maendeleo ya jamii amebainisha kilele cha maadhimisho kitakuwa na mabanda ya huduma na maonesho ya bidhaa kutoka kwa wanawake wajasiriamali na wadau mablimbali ili kuonesha kazi zinazofanywa na wanawake katika kujiletea maendeleo jumuishi. Kadhalika, kutakuwa na shuhuda za wanawake jasiri ambao wanafanya kazi zilizodhaniwa kuwa ni za wanaume ili kuhamasisha wazazi na wasichana kufanya kazi za aina zote.

Kuelekea maadhimisho hayo pia, kutakuwa na msafara wa kutokomeza ukatili wa kijinsia utakaopita katika maeneo ya mikoa kadhaa hapa nchini ili kuhimiza upatikanaji wa huduma za kiuchumi na kijamii kwa wanawake. Huduma hizi ni pamoja na upimaji wa afya ya akinamama, elimu ya biashara na ujasiriamali, kupinga ukatili wa kijinsia, msaada wa kisheria, mabadiliko ya tabia nchi na ushiriki wa jamii katika nafasi za uwakilishi na vyombo vya kutoa maamuzi.

Maadhimisho ya siku ya Wanawake Duniani Kitaifa yatafanyika Mkoani Simiyu tarehe 08 Machi, 2020 na kauli mbiu ni “Kizazi cha usawa kwa maendeleo ya Tanzania ya sasa na baadaye” inayosisitiza kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa uwepo wa usawa wa kijinsia katika kufikia malengo ya maendeleo endelevu.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.