Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya
Afya- Idara Kuu ya maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bw. Prudence
Consntatine na kushoto ni Afisa Maendeleo ya Jamii Mkuu Bw. Erasto Chingoro
(kulia) akitoa ufafanuzi wa baadhi ya maswali yaliyoulizwa na waandishi wa
Habari kuhusu maandalizi ya Siku ya wanawake Duniani kwa mwaka 2020 katika
kikao kilichofanyika Jijini Dar es salaam leo
Na Mwandishi wetu
Dar es salam
Serikali
imeitaka jamii kuhakikisha inapinga ukatili wa aina zote ili kufikia malengo ya
kuwa na kizazi chenye usawa kati ya wanawake na wanaume.
Akizungumza
na waandishi wa Habari Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini katika Wizara
ya Afya, Idara kuu ya maendeleo ya jamii Bw. Prudence Constantine mapema leo
tarehe 21 Februari, 2020 jijini Dar es Salaam, amesema kuelekea maadhimisho ya
siku ya Wanawake Duniani tarehe 08 Machi mwaka huu kauli mbiu imelenga
kutengeneza jamii yenye usawa kati ya mwanaume na mwanaume.
”Katika miaka ya 1990 wanawake
walikuwa wanafanya kazi nyingi, ujira kidogo, unyanyasaji, hawakupewa
kipaumbele ikilinganishwa na wafanyakazi wanaume” amesema
Prudence.
Amesema lengo la maadhimisho ya
siku hiyo ni kutathmini utekelezaji wa afua za kufikia usawa wa jinsia na
uwezeshaji wanawake kiuchumi, kijamii, kisiasa katika kufikia maendeleo
jumuishi. Maadhimisho haya pia yanatoa fursa ya kuelimisha jamii kuhusu
jitihada mbalimbali zilizofanywa na jamii, Serikali, Asasi za Kiraia, Sekta
Binafsi na wadau wengine katika kukuza hali ya mwanamke wa kitanzania.
Kadhalika, katika kuadhimisha Siku hii wadau wanapata fursa ya kubainisha upungufu
na mbinu za utatuzi wa changamoto zilizopo.
Bw. Prudence amesema Serikali
imeendelea na jitihada za kuwawezesha wanawake kiuchumi kwa kuanzisha mfuko wa
uwezeshaji kiuchumi ikiwa ni pamoja na mfuko wa maendeleo ya wanawake wenye
masharti nafuu ambao umesaidia kutoa mikopo nafuu na mafunzo ya stadi za
biashara kwa wajasiriamali wanawake.
“Wizara inahakikisha kutumia
maadhimisho haya kwa kuandaa makongamano na majukwaa mbalimbali ili kujadili na
kuibua kero zinazokwamisha maendeleo na Ustawi wa wanawake na kuyatafutia
ufumbuzi ikiwemo matatizo ya maji na uchumi duni” amesema Bw. Prudence.
Ameongeza kuwa tangu mwaka
2015/16 hadi 2018/19 Serikali imetoa fedha kiasi cha Tsh. Bilioni 28.8 ambayo
imesaidia vikundi vya wanawake 13,691 na kufanya idadi ya wanawake
wajasiriamali walionufaika na fedha hizo kufikia 883,724 ukilinganisha na
wanawake 12,842 kwa mwaka 2013/14.
Aidha, Serikali imewezesha wanawake
wajasiriamali kushiriki katika maonesho ya biashara mbalimbali za Kitaifa na
Kimataifa kwa mwaka 2017/18 ambapo wanawake wajasiriamali 1,183 kutoka katika
Mikoa yote 26 wamenufaika na fursa hiyo kushiriki.
Naye Afisa maendeleo ya jamii Mkuu kutoka wizara
ya Afya idara kuu ya maendeleo ya jamii amebainisha kilele cha maadhimisho kitakuwa
na mabanda ya huduma na maonesho ya bidhaa kutoka kwa wanawake wajasiriamali na
wadau mablimbali ili kuonesha kazi zinazofanywa na wanawake katika kujiletea
maendeleo jumuishi. Kadhalika, kutakuwa na shuhuda za wanawake jasiri ambao
wanafanya kazi zilizodhaniwa kuwa ni za wanaume ili kuhamasisha wazazi na
wasichana kufanya kazi za aina zote.
Kuelekea maadhimisho hayo pia, kutakuwa na msafara wa
kutokomeza ukatili wa kijinsia utakaopita katika maeneo ya mikoa kadhaa hapa
nchini ili kuhimiza upatikanaji wa huduma za kiuchumi na kijamii kwa wanawake.
Huduma hizi ni pamoja na upimaji wa afya ya akinamama, elimu ya biashara na
ujasiriamali, kupinga ukatili wa kijinsia, msaada wa kisheria, mabadiliko ya
tabia nchi na ushiriki wa jamii katika nafasi za uwakilishi na vyombo vya kutoa
maamuzi.
Maadhimisho ya siku ya Wanawake Duniani Kitaifa
yatafanyika Mkoani Simiyu tarehe 08 Machi, 2020 na kauli mbiu ni “Kizazi cha
usawa kwa maendeleo ya Tanzania ya sasa na baadaye” inayosisitiza kuelimisha
jamii kuhusu umuhimu wa uwepo wa usawa wa kijinsia katika kufikia malengo ya
maendeleo endelevu.
No comments:
Post a Comment