Habari za Punde

Serikali yaimarisha usikivu wa TBC kwa asilimia zaidi ya 73.


Na.Shamimu Nyaki-WHUSM, Dodoma
Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) ni chombo cha Habari cha Umma chenye wajibu wa kuhabarisha kuelimisha pamoja na kueleza mikakati ya Serikali katika kuleta maendeleo kwa wananchi.

Katika kuhakikisha yote hayo yanafanyika Serikali inafanya juhudi kubwa za kuimarisha usikivu wa Shirika hilo katika mikoa yote ya Tanzania ili wananchi wapate taarifa sahihi zilizokusudiwa tena  kwa wakati.

Moja ya mikakati ambayo Serikali imeweka katika kuimarisha usikivu wa Shirika hilo ni kubadilisha mitambo ya zamani na kuweka mipya na kuhamisha mitambo kutoka sehemu ambayo mawimbi ya FM hayafiki na kuipeleka maeneo ya vilima vilivyopo juu zaidi ambapo wataalamu wameona kuwa ndio maeneo sahihi yatakayosaidia kupeleka mawimbi ya redio na televisheni kuwafikia wananchi nchi nzima.

Shirika hili chini ya uongozi wake Mkurugenzi Mkuu Dkt. Ayoub Ryoba linaendelea kuweka mipango na mikakati ya kuhakiksha wananchi wanapata habari ambapo matarajio ni kukakikisha usikivu wa redio unzifikia wilaya 117 nchi nzima.

Serikali imefanya mageuzi makubwa katika kuhakikisha usikivu unaimarika ambapo umeongezeka kutoka Wilaya 87 mwaka 2017 sawa na asilima 54 hadi wilaya 102 mwaka 2019 ambapo pia imejenga vituo vitano ambavyo tayari ujenzi wake umekamilika na vimeanza kutumika. Wilaya za mpakani ndizo zimenufaika na ujenzi huo ikiwemo Rombo, Kibondo, Tarime, Kankonko, Longido eneo la Namanga, Nyasa hadi Mbambabay.

Yapo ameneo ambayo usikivu ni hafifu hali ambayo imeilazimu Serikali kuweka mitambo ya redio katika ameneo yenye changamoto hiyo ambayo katika mikao mitano ya Lindi, Katavi, Njombe, Simiyu, Songwe ambapo nguvu hiyo pia inaelekezwa katika mikoa ya Unguja na Pemba..

Hivi karibuni Naibu Waziri wa Habari Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Juliana Shonza amesema kuwa TBC inaendelea na mpango wa kupanua usikivu maeneo yote ya nchi ili wananchi wengi wapate manufaa ya shirika lao ambapo amesema lengo la Serikali ni kuiwezesha TBC Redio kufikia usikivu nchi nzima kama ambavyo TBC Televisheni inaonekana kupitia visimbuzi na satellite vyote zilizosajiliwa nchini.   

Ni dhahiri ziara ya Waziri wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe aliyoifanya hivi karibuni katika mikoa ya Tanga, Kilimanjaro, Arusha, Manyara na Singida ilikuwa ni muendelezo wa ziara za kikazi ambayo ilikuwa na lengo la kuona na kujiridhisha kuhusu usikivu wa TBC katika maeneo hayo na hatua zilizochukuliwa na shirika hilo katika kutatua changamoto zinazowakabili ili kuhakikisha matangazo ya redio yanawafikia wananchi wote inavyotakaiwa kwa wakati ikiwa ni haki yao ya msingi ya Kikatiba ya kupata taarifa za Serikali.

Akiwa katika Mkoa wa Tanga Dkt. Mwakyembe alisema kuwa Serikali inaendelea kuboresha usikivu wa matangazo ya Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC) kwa kuimarisha mitambo ya kurushia matangazo katika kituo cha Mnyusi kilichopo Hale wilaya ya Korogwe na Kwemashai wilaya ya Lushoto mkoani Tanga.

Dkt. Harrison Mwakyembe alisema kuwa usikivu wa TBC Taifa mwaka 2015 ulikuwa ni asilimia 54 ambapo kwa sasa baada ya Serikali kuboresha vituo hivyo usikivu umefikia kiwango cha asilimia 73 na inatarajiwa ifikapo mwishoni mwa mwaka 2020 utafikia zaidi ya asilimia 90.

Katika Mkoa wa Kilimanjaro Waziri Mwakyembe alitembelea kituo cha TBC Taifa Mabungo kilichopo wilayani Moshi kinachorusha matangazo katika masafa ya FM 87. 9 Mhz na TBC FM katika masafa ya 90.0 Mhz pamoja na kituo cha Tarakea kilichopo katika Wilaya ya Rombo ambacho matangazo ya TBC Taifa yanapataikana kupitia masafa ya 87.9Mhz na TBC FM inarusha kupitia 90.0 Mhz.

Akiwa mkoani Arusha Dkt.Mwakyembe alitembelea eneo la Themi ambalo ndio mitambo ya TBC imewekwa ambayo inarusha matangazo yake kupitia masafa ya 89.9 Mhz kwa FM na 87.7 Mhz pamoja na kituo cha cha Namanga kilichopo katika Wilaya la Longido.

Hata hivyo usikivu umeendelea kuimarishwa katika mikoa ya Singida pamoja na Manyara ambayo pia Waziri mwenye dhamana ya habari alifanya ziara ya kikazi katika mikoa hiyo kukagua hali ya usikivu na kupokea taarifa kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa TBC Dkt. Ayoub Ryioba ambaye alitoa taarifa kuwa mkoa wa Singida ulikua na changamoto ya usikivu baada ya mtambo kuharibika ambapo tayari Serikali imechukua hatua ya kutafuta mitambo mingine.

Dkt. Ryoba amesema kuwa mitambo miwili ya Khts 2 sawa na Wats 2000 imeshawasili nchini tayari kwa kufungwa katika eneo la Mikumbi Mkoani hapo ili kuongeza usikivu katika maeneo mengi ya mkoa huo ambao matarajio ni kuimarisha usikivu kwa zaidi ya asilimia 70 mwishoni mwa mwaka huu.

“Hizi jitihada kubwa kwa Serikali za kuhakikisha kuwa inatekeleza  Ibara ya 18 d ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoeleza kuwa kila mwananchi ana haki ya kupata taarifa sahihi, hivyo ni jukumu la Serikali kuweka mazingira bora kwa vyombo vya habari kutoa habari bila changamoto zozote  na kuzifikisha kwa walengwa kwa usahihi na kwa wakati” alisisitiza Dkt. Mwakyembe.

Aidha, Dkt. Mwakyembe alipata pia fursa ya kutembelea mkoa wa Manyara ambapo tayari Serikali imeanza kuhamisha mitambo ya Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) kutoka katika jengo la Mkoa wa Manyara kupeleka katika eneo la Gitsmii ambalo lina mwinuko utakaosaidia kuimarisha usikivu katika mkoa huo ambao nao una kabiliwa na changamoto ya kutosikika vizuri kwa matangazo ya TBC katika maeneo mengi.

Waziri Mkwayembe alisema kuwa Serikali inafahamu changamoto ya usikivu wa TBC Manyara ndio maana wataalam wamekuja na suluhisho la changamoto hiyo ya kuhamisha mtambo kupeleka eneo ambalo wameona litarahisisha upatikananji wa wa matangazo vizuri.

Katika ziara yake katika mikoa hiyo, Waziri amejionea changamoto ya miundombinu mibovu ya kufika eneo la mitambo ambapo alitoa maagizo kwa mikoa hiyo kushirikiana na TANROADS, TANESCO pamoja na Idara ya Maji kutatua changamoto hizo za barabara pamoja na umeme ili kuhakikisha wanaweka miundombinu rafiki kwa ajili ya ulinzi wa mali ya umma kwa manufaa ya wananchi na taifa kwa ujumla.

Dkt. Mwakyembe alieleza kuwa barabara za kuelekea kituo cha Gitsmii Manyara, Mnyusi Hale pamoja na kwemashai Lushoto zinapaswa kujengwa kwa lami au zenge kwakuwa sehemu hizo zina miinuko mikali pamoja kona nyingi, ambapo vituo vya Namanga Wilayani Longido, Mbungo Moshi na Themi Arusha vinahitaji barabara ya lami pia.

Hata hivyo Wakuu wa Mikoa hiyo wameahidi kutekeleza maagizo hayo ambayo ni kipaumbele kwa wananchi ili waweze kupata matangazo ya redio yao kwa kuwa ina lengo la kuhabarisha, kuelimisha, kuonya pamoja na kuburudisha na wameunga mkono jitihada za Serikali za kuimarisha usikivu katika maeneo yao.

Kwa upande wao Mkuu wa wilaya ya Longido Frank Mwaisumbe na Agnes Hokororo wilaya ya Rombo wamesema kuwa kwa sasa TBC imekuwa chanzo kikuu kwa wananchi wa wilaya zao kupata taarifa  za maendeleo ya nchi zao tofauti na hali ilivyokuwa miaka ya nyuma ambapo wananchi walikuwa wakipata taarifa kutoka nchi za jirani

Wananchi katika mikoa ambayo Waziri Dkt. Mwakyembe alitembelea wamesema kuboreshwa miundombinu kufika maeneo ambayo TBC imesimika mitambo yake ya kurusha matangazo ikiwemo barabara, umeme na maji itasidia pia kuboresha maisha yao kiuchumi na kijamii na itasaidia kuwa kiunganishi kikubwa katika kuleta maendeleo ya kaya zao pamoja na Taifa.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.