Habari za Punde

SHIRIKA LA UNICEF KUSHIRIKIANA NA TANZANIA KUWEKEZA KWA WATOTO

Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb), akifurahi baada ya kukabidhiwa jarida linalohusu watoto na Mwakilishi Mkazi wa wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Watoto (UNICEF) nchini Tanzania, Bi.  Shalini Bahuguna, jijini Dodoma.
Ujumbe kutoka Tanzania ukiongozwa na Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb) (watatu kushoto), wakati wa kikao na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Watoto (UNICEF) nchini Tanzania Bi. Shalini Bahuguna (katikati), jijini Dodoma.
Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Isdor Mpango (katikati), na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Watoto (UNICEF) Tanzania Bi. Shalini Bahuguna (watatu kushoto), wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wajumbe wa mkutano kutoka Wizara ya Fedha na Mipango na UNICEF, jijini Dodoma.
 (Picha na Peter Haule, WFM).

Na. Peter Haule na Josephine Majura, WFM, Dodoma
Serikali ya Tanzania na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF), wamekubaliana kuongeza jitihada katika uwekezaji kwa watoto ili kuwa na kizazi chenye uwezo na maarifa yatakayosababisha taifa kufikia malengo yaliyojiwekea kwa kuwekezqa kwa watoto ilikuwa na kizazi kitakachokuwa na mchango mzuri katika maendeleo ya taifa.
Hayo yamebainishwa jijini Dodoma na Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, alipokutana na kufanya mazungumzo na Mwakilishi Mkazi wa UNICEF nchini Tanzania, Bi. Shalini Bahuguna.
Dkt. Mpango alisema kuwa, ni muhimu kuwekeza katika teknolojia ya kisasa yakiwemo matumizi ya simu za mkononi kufikisha elimu stahiki kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kuwekeza katika maendeleo ya watoto hususani lishe bora kuanzia wakati wa ujauzito.
“Tusipowekeza kwenye lishe bora kwa watoto tutapata taifa la wananchi ambao hawana uwezo mkubwa wa kufikiri, kufanya biasharana na kushiriki kikamilifu katika michezo,”, alieleza Dkt. Mpango
Alisema kuwa ipo mikoa ambayo inazalisha chakula cha kutosha lakini ina watoto wenye lishe duni kiwango cha utapiamlo hivyo wamekubaliana na UNICEF kusaidiana kuhakikisha elimu ya lishe bora kwa watoto inapelekwa kwa wananchi ili kusaidia kizazi cha kesho chenye tija kwa taifa na Dunia kwa ujumla.
Dkt. Mpango alisema kuwa ni muhimu pia kulinda na kushughulikia tatizo la watoto wa mitaani kwa kuwa na program kama Serikali ya kuzuia idadi ya watoto wanaozurura mitaani na pia waliopo waweze kurejeshwa mashuleni na kwenye utaratibu mzuri kwa kuwa hiyo ni nguvu kazi ya taifa ambayo haiwezekani kuendelea kuachwa mtaani.
Vilevile alisema kuwa ni lazima kuhakikisha watoto wenye ulemavu wanasimamiwa vizuri na kuendeleza vipaji vyao kwa kuwa wapo wanaofichwa majumbani, ni vema jamii ibadili mtazamo na kuwaona kama binadamu wengine wanaohitaji huduma stahiki kutoka kwa wananchi na Serikali yao.
Aidha ameyataka mashirika yasiyo ya Serikali (NGO) kuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha haki za watoto wakiwemo wanaonyanyaswa zinapatikana kwa kuwafikia kwa kutoa elimu.
Kwa upande wake Mwakilishi Mkazi wa UNICEF nchini Tanzania, Bi. Shalini Bahuguna, ameipongeza Serikali ya Tanzania kwa jitihada zake za kuwekeza kwa watoto na kuwapatia Lishe bora.
Alisema Serikali ya awamu ya tano ina maono ya kuwa na miundombinu bora, viwanda na kuongeza ukusanyaji wa mapato, mambo ambayo yatafikiwa kwa kuwekeza kwa watoto hasa katika lishe bora na Shirika lake lipo tayari kushirikiana na Tanzania katika kufikia lengo hilo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.