Habari za Punde

WAZIRI WA AFYA UMMY MWALIMU ATHIBITISHA UWEPO WA MGONJWA WA KWANZA WA CORONA NCHINI

Na Avila Kakingo, Globu ya jamii
WAZIRI wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu amesema kuna mtu mmoja mwenye umri wa miaka 46 ameainika kuwa na virusi vya Corona Covid 19 ambaye aliwasili nchini na ndege ya Rwandan air  akitokea nchini ubelgiji.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam Waziri Ummy amesema kuwa  mtu huyo ambaye ni mwanamke raia wa Tanzania aliondoka nchini, Machi 3, 2020,ambapo kati ya Machi 5 hadi Machi13 alitembelea nchi za Swiden  na Denmark na kurudi tena Ubelgiji na kisha alirejea nchini Machi 15,2020 saa 10 jioni.

"Msafiri huyo alipita uwanja wa ndege wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA)  akafanyiwa ukaguzi, na maafisa wetu wa Afya na kuonekana kutokuwa na homa na baadae alianza kujisikia vibaya akiwa hotelini na kwenda hospitali ya Rufaa ya Mkoa ya Maunt Meru Arusha," amesema Waziri Ummy.

Hata hivyo Waziri Ummy amesema kuwa sampuli zilichukuliwa na kupelekwa maabala ya Taifa ya Afya ya Jamii iliyopo jijini Dar es Salaam kwaajili ya uchunguzi.

"Vipimo vya maabala vimethibitisha kuwa mtu huyu anamaambukizi ya ugonjwa Corona- Covid 19 mgonjwa  anaendelea vizuri na matibabu." Amesema Waziri Ummy.

Waziri Ummy ametowatoa hofu wananchi na kwamba serikali  inaendelea kuchukua hatua madhubuti za kuhakikisha ugonjwa huo unadhibitiwa ili usisambae nchini.

Aidha serikali inashirikiana na Shirika la Afya Duniani (WHO) na wadau katika kuendelea kutekeleza mikakati kukabiliana na ugonjwa huo.



Ummy amewataka Wananchi kuchukua tahadhari, ya kujikinga na ugonjwa huu kama tunavyowapatia taarifa na elimu mara kwa mara kupitia njia mbalimbali.

Kwa nchi za Afrika Mashariki  nchi ya Kenya ilikuwa ya kwanza kutoa taarifa ya Uwepo wa mgonjwa wa Corona na kutokana na kuendelea kusambaa kwa ugonjwa huo tayari serikali ya nchi hiyo imefunga shule zote na kuzuia mikusanyiko isiyo ya lazima.

Pia nchi nyingine ambayo ugonjwa huo umeingia ni Rwanda na leo imeripotiwa kuingia Tanzania.

Hata hivyo ugonjwa huo kwa mara ya kwanza ulilipotiwa kutokea nchini China na baadae ulisambaa katika nchi mbalimbali duniani na tayari Shirika la Afya Duniani limetangaza ugonjwa huo kuwa janga la dunia.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.