Naibu Waziri Wizara
ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe.Juliana Shonza (katikati) akitoa
maelekezo kwa Mkurugenzi wa Benchmark Production Madam Ritha Paulsen(hayupo
pichani) kuhakikisha ndani ya mwezi mmoja anamlipa mshindi wa kwanza wa
mashindano hayo ya Bongo Star Search kwa mwaka 2019 Bw.Meshack Fukuta, mbele ya
waandishi wa habari (hawapo pichani) Aprili 08,202 Jijini Dodoma,kulia ni Afisa
Utamaduni Bw.Mfaume Said kutoka hiyo na kushoto ni Mshindi wa kwanza wa
shindano la Bongo Star Search mwaka 2019 (BSS) Bw.Meshack Fukuta.
Baadhi ya waaandishi
wa Habari wakifuatilia maelekezo ya Naibu Waziri Wizara ya Habari, Utamaduni,
Sanaa na Michezo Mhe.Juliana Shonza kwa Mkurugenzi wa Benchmark Production
Madam Ritha Paulsen (hayupo pichani) kuhakikisha ndani ya mwezi mmoja anampatia mshindi wa kwanza wa mashindano
Bongo Star Search ya mwaka 2019 zawadi yake ya milioni 50 leo Aprili 08,202
Jijini Dodoma.
Na Shamimu Nyaki
– WHUSM 08/04/2020, Dodoma.
Naibu Waziri wa Habari,
Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe.Juliana Shonza ametoa mwezi mmoja kuanzia Aprili
08, 2020 kwa Kampuni ya Benchmark Production inayoendesha mashindano ya Bongo
Star Search chini ya Mkurugenzi wake Madam Ritha Paulsen kumlipa kiasi cha
Shilingi milioni 50 mshindi wa kwanza wa mashindano hayo kwa mwaka 2019,
Bw.Meshack Fukuta.
Naibu Waziri
ametoa maelekezo hayo leo Jijini Dodoma baada ya kupokea barua kutoka kwa
familia ya mshindi huyo iliyoeleza kutokutekelezwa kwa ahadi hiyo kwa takriban
miezi minne sasa ilioanisha utaratibu wa malipo hayo kuwa milioni 30 ni kwa
ajili kutengeneza kazi za muziki na matangazo kwa kipindi cha mwaka mmoja na
milioni 20 ni ya kukabidhiwa mkononi ambapo Mhe. Naibu Waziri amesisitiza
makubaliano yote yalioanishwa kufanyiwa kazi.
“Mimi kama mlezi
wa tasnia ya Sanaa ambaye pia nilikua mgeni rasmi siku ya fainali nimesikitishwa
sana na malalamiko haya, hivyo naitaka kampuni ya Benchmark kutekeleza ahadi
hiyo na wasipofanya hivyo ndani ya muda huo, Serikali haitasita kufungia
mashindano hayo”, alisema Mhe.Shonza.
Mhe. Naibu
Waziri ameongeza kuwa Wizara iliwasiliana na uongozi wa Benchmark kuhusu
malalamiko hayo mbapo Kampuni hiyo ilieleza kuwa imeshindwa kumlipa msanii huyo
kutokana na viongozi wa Kampuni iliyodhamini shindano hilo ya Startimes kuwepo nchini China na kushindwa kusafiri
kuja nchini kutokana na uwepo wa ugonjwa wa Corona.
Hata hivyo
Mhe.Naibu Waziri ameleeza kuwa Wizara iliwasiliana na uongozi wa Startimes
ambao umekiri kuwa umeshalipa fedha kwa Kampuni ya Benchmark tangu mwezi Januari
2020.
Aidha, Mhe.Shonza ameitaka kampuni hiyo kuhakikisha
inamtengenezea msanii huyo wimbo bora pamoja na kuufanyia matangazo ya kutosha
katika kipindi cha miezi miwili kuanzia leo pamoja na kuwasilisha nakala ya mkataba wa
washiriki waliofikia hatua ya kumi bora ndani ya wiki moja kuanzia leo machi
08,2020.
Katia hatua nyingine
Mhe.Shonza ameliagiza Baraza la Sanaa na Taifa (BASATA) kusimamia utaratibu wa
uaandaji wa mashindano mbalimbali
ikiwemo kuwepo kwa mikataba kati ya wasanii na wanaondesha
mashindano au shughuli yoyote ya sanaa
na wasanii pamoja na kuhakikisha ahadi wanazopewa washindi ikiwemo zawadi zinakuwepo na zinakabidhiwa kwa wahusika mara
baada ya mashindano.
Kwa upande wake
Bw.Meshack Fukuta mshindi wa shindano hilo kwa mwaka 2019 ameishukuru Serikali
kwa namna ambavyo imechukua hatua katika malalamiko yake ambapo ameahidi
kufanya juhudi katika Sanaa yake ili kuitangaza nchi vizuri ndani na nje ya
nchi pamoja na kujipatia kipato kupitia kipaji hicho.
No comments:
Post a Comment