MAMLAKA ya
Maji Zanzibar (ZAWA) na Wizara ya Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati zimeagizwa
kufanya jitihada za kusambaza maji safi na salama katika mwezi Mtukufu wa
Ramadhani katika maeneo ambayo wananchi hawapati huduma hizo ipasavyo.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed
Shein,
ametoa agizo hilo katika risala ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani aliyoitoa kupitia
vyombo vya habari, ikiwa ni utaratibu wake aliouweka kila ukikaribia mwezi huo
Mtukufu kila mwaka.
Katika risala yake hiyo, Rais Dk. Shein alisema kuwa kama
kawaida yake katika risala zake zote kama hizo ambazo huzitoa kila mwaka hutoa
agizo hilo kwa taasisi hizo husika kwa kuhakikisha kuwa zinawapelekea maji
wananchi katika yale maeneo ambayo hawapati maji vizuri agizo ambalo amelirejea
tena mwaka huu.
Aidha, Rais Dk. Shein aliwataka wananchi wote wa Zanzibar
wa dini na madhehebu mbali mbali kuendeleza utamaduni wa tangu kale na dahari
wa kupendana, kusaidiana, kuheshimiana na kuvumiliana na kutoa wito kuendeleza
utamaduni huo ambao ni miongoni mwa misingi inayofanya kuishi kwa amani na
utulivu nchini.
Aliongeza kuwa wale ambao hawahusiki na ibada ya funga,
hapana shaka kama kawaida yao wataendelea kutumia busara na kuonesha ustaarabu
kwa kujiepusha na mambo yasiyowapendeza wananchi wenzao wanaotekeleza ibada hii
ya funga.
Vile vile, Rais Dk. Shein alitoa wito kwa vyombo vya ulinzi
kuimarisha doria za ulinzi katika maeneo mbali mbali hasa kwa wakati ambao watu
wengine watakuwa katika shughuli za ibada.
Kadhalika, Rais Dk. Shein aliwakumbusha madereva wazingatie
sheria za usalama wa barabarani ili kupunguza tatizo la kuongezeka kwa ajali za
barabarani katika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.
Rais Dk. Shein pia, alitumia fursa hiyo kuwaagiza
wafanyakazi wa Jiji la Zanzibar na Manispaa zake, Mabaraza ya Miji na
Halmashauri za Wilaya waongeze bidii katika kusimamia usafi wa Jiji la Zanzibar
na miji mingine, masoko pamoja na nidhamu ya kufanya biashara.
Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein aliwahimiza wauzaji wa
bidhaa mbali mbali kuzingatia matumizi bora ya mvua za Masika zinazoendelea kwa
kudumisha usafi na kuimarisha nidhamu katika masoko na maeneo maalumu
yaliyotengwa kwa shughuli za biashara.
Aidha, Rais Dk. Shein aliwahimiza Waumini wa Dini ya
Kiislamu kuzielekeza nafsi zao katika kufanya mambo ya kheri waliyohimizwa na
Mola Mtukufu katika Qurani na Hadithi za Mtume Muhammad (S.A.W) ili kuweza
kupata rehma na kufaidika na fadhila kubwa za mwezi Mtukufu wa Ramadhani.
“Ni wajibu wetu tuzichunge ndimi zetu kwa kujiepusha
kusengenya, kutoa kauli mbaya pamoja na kufanya vitendo vinavyoweza kuzusha
fitna na hasada ndani ya jamii”, alisema Dk. Shein.
Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein aliwataka wananchi wakati
wote kuwa makini kwa yale mambo wanayoangalia na kuyasikiliza katika redio na
televisheni pamoja na yale wanayoyaandika katika mitandao ya kijamii kupitia
simu za mikononi.
Alisisitiza haja ya kujitathmini juu ya aina ya taarifa na
picha wanazoziingiza katika mafaili ya simu zao za mikononi na kuwataka
kujidhatiti katika kuyashinda matamanio yote ya nafsi yanayoweza kuzibatilisha
funga zao.
Katika risala hiyo pia, Rais Dk. Shein alitoa pongezi za
dhati kwa Mwenyekiti wa Kamisheni ya Kupambana na Maafa ya Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar
pamoja na wajumbe wote.
Kadhalika, Rais Dk. Shein alitoa pongezi kwa Mwenyekiti wa
wa Kamati ya Kupambana na Maradhi yanayosabaishwa na virusi vya COVID 19 ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaaliwa Majaaliwa, Waziri Mkuu wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na wajumbe wote kwa kufanya kazi kwa
pamoja na kwa uzalendo.
Vile vile Rais Dk. Shein alitoa shukurani kwa viongozi
wengine mbali mbali wa Serikali, dini, jamii na wananchi wote kwa jumla kwa
kuziunga mkono juhudi za Serikali katika kupambana na maradhi hayo.
Shukurani za dhati alizitoa Rais Dk. Shein kwa madaktari na
wataalamu wa afya ambao tangu yalipoanza maradhi hayo wamefanya juhudi kubwa ya
kutoa elimu kwa wananchi pamoja na kuwapatia huduma mbali mbali kwa wale wote
walioathirika au kuonesha dalili za maradhi hayo.
Rais Dk. Shein pia, aliwapongeza wafanyabiashara na
wananchi ambao wameanza kuchangia kwenye Akaunti zilizofunguliwa kwenye Benki
ya PBZ na CRDB katika kukabiliana na COVID 19 na kuwashukuru wale wote
waliochangia kwa kutoa vifaa maalum na nyenzo mbali mbali ambazo zitasaidia
mapambano dhidi ya COVID 19.
“Tuzingatie ule usemi maarufu wa Kiswahili usemao “Kutoa ni
moyo si utajiri”. Wazee wetu walitueleza tangu kale na dahari maneno yao
yaliyojaa hekima ya kuwa “Haba na haba hujaza kibaba”. Serikali ipo tayari
kupokea chochote kilicho haba, ili kwa pamoja tujaze kibaba kupitia mfuko
maalum”,alisisitiza Dk. Shein.
Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alisema kuwa
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na wahusika mbali mbali inapanga kuongeza
kiwango cha taaluma ili wale ambao wanaonekana hawajazingatia vizuri elimu na
taarifa zilizotolewa nao waweze kuelimika zaidi.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment