Habari za Punde

WAKALA WA VIPIMO WATOA MSAADA WA MADAWATI


Na: Thomas Valentine, Maelezo                                                                                      
Baada ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli kuruhusu shule zote kufunguliwa tarehe 29 mwezi huu wakati akifunga Bunge la 11 Jijini Dodoma, shule ya Sekondari King’ongo iliyopo katika kata ya Saranga wilaya ya Ubungo Jijini Dar es Salaam imepokea msaada wa madawati 50 na viti 50 yenye thamani ya shilingi milioni 24 kutoka kwa Wakala wa Vipimo (WMA).

Akizungumza katika hafla hiyo ya kukabidhi madawati katika shule hiyo Jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Ufundi Wakala wa Vipimo Bi. Stella Kahwa amesema kwamba mchango huo ni sehemu ya utekelezaji na dhamira ya Wakala wa Vipimo kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuboresha elimu.

“Huu ni mchango wetu kama wakala wa vipimo katika kuhamasisha, naamini watoto watasoma katika mazingira mazuri na wataweza kusoma vizuri zaidi na kufanya vizuri zaidi katika masomo yao na mitihani ya kata na ya taifa.” Amesema Kahwa.

Makabidhiano yamehudhuriwa na Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa Bi. Tatu Pambe ambaye amesema madawati hayo 50 na viti 50, yataboresha mazingira ya kujifunzia kwa wanafunzi na kutoa wito kwa wadau wengine kuunga mkono zoezi hilo kwani tatizo la uhaba wa madawati katika shule hiyo ni changa moto sana.

“Kwanza tunashukuru Serikali kupitia Wakala wa Vipimo kwa kuweza kutuwezesha kwa ajili ya madawati.

Shule yetu ya sekondari kuna madarasa mengi lakini tatizo ni madawati, lakini kupata madawati 50 na viti 50 tunashukuru sana.” Amesema Tatu.

Naye mwalimu mkuu wa shule ya Sekondari King’ongo Bw. Joseph Msangya ameipongeza Wakala wa Vipimo kwa msaada huo wa madawati na kusema kuwa msaada huo utasaidia kupunguza changamoto ya madawati kwani mahitaji ya madawati ni mengi shuleni hapo.

Mkuu wa shule hiyo amesema ongezeko la madawati utasaidia katika kuongeza ufaulu wa masomo kwa wanafunzi kutokana na kusoma katika mazingira mazuri.

“Shule yetu ina wanafunzi 1,052 kwa hiyo uhitaji tunao ni mkubwa sana. Tuna madarasa matatu ambayo hayana kiti wala meza, lakini tunashukuru Wakala wa Vipimo kwa mchango wao baada ya kuona na kuguswa kwa hili na pia tunawaomba wada wengine ambao wameguswa kwa namna moja au nyingine kutusaidia maana mahitaji yetu ni mengi.”Amesema Msangya.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.